'Zanzibar Matibabu Card' yashinda tuzo ya WSIS

NA MWANDISHI MAALUM, USWISI

WIZARA ya Afya Zanzibar imetunukiwa tuzo ya kimataifa ya ‘World Summit on the Information Society’ (WSIS) kutokana na mafanikio ya utekelezaji wa mfumo wa matibabu kwa njia ya kadi maalum ya kidijitali ijulikanayo kama Zanzibar Matibabu Card’, ambao umewezesha utoaji wa huduma bora za afya kwa wananchi kupitia teknolojia.

Hafla ya kukabidhi tuzo hiyo ilifanyika Geneva, Uswisi na kuhudhuriwa na Waziri wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano wa serikali ya Jamhuri ya Muungano wa tanzania, Jerry Slaa, Balozi wa Tanzania Geneva, Abdallah Possi, pamoja na wajumbe kutoka Mamlaka ya Serikali Mtandao Zanzibar (e-GAZ) na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA).

Akipokea tuzo hiyo kwa niaba ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Waziri wa Afya Zanzibar, Nassor Ahmed Mazrui,  alisema mpango huo ni uthibitisho wa dhamira ya taifa kutumia teknolojia kuboresha maisha ya wananchi.

Alieleza kuwa mfumo huo umeunganisha vituo vyote vya afya vya umma na taarifa za matibabu za wagonjwa kwa njia ya kidijitali, hatua inayochochea uwazi, ufanisi na usawa katika sekta ya afya.

“Mpango huU unawezesha upatikanaji na utoaji wa huduma za afya katika eneo lolote, ukiwa mfano wa kuigwa kwa nchi za kipato cha chini na cha kati zinazolenga kufikia mpango wa Huduma za Afya kwa wote (UHC) kupitia mifumo ya kidijitali”, alisisitiza Mazrui.

WAZIRI wa Afya Zanzibar, Nassor Ahmed Mazrui, akizungumza baada ya kupokea tuzo ya kimataifa ya ‘World Summit on the Information Society’ (WSIS) kwa niaba ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar iliyotolewa mjini Geneva, Uswisi, hivi karibuni. Kulia ni Waziri wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jerry Slaa. 

Akizungumzia hatua hiyo, Mkurugenzi wa Programu wa PharmAccess, Faiza Abbas, alisema mradi huo umedhihirisha uwezo wa uvumbuzi wa kidijitali katika kufanikisha huduma bora za afya na kuziba pengo la usawa.

Alibainisha kuwa mfumo huo unaunganisha moja kwa moja rekodi za matibabu kupitia mifumo mbalimbali kama SHAMS-EMR, NSK-EMR na ZanEMR kwa ngazi tofauti za huduma nchini na hivyo kusaidia usimamizi bora wa afya ya jamii.

Faiza alieleza kuwa mafanikio ya mradi huo yamewezeshwa na ushirikiano wa karibu baina ya PharmAccess, UNICEF, ZEDCo, NSK Tanzania na Hospitali ya Saifee.

Alisema kuwa ushirikiano huo umesaidia kuhakikisha mfumo huo wa kidijitali unalingana na sera za taifa na umeunganishwa na kitambulisho cha Mzanzibari mkaazi (ZanID) pamoja na vyeti vya kuzaliwa, hatua inayolenga uendelevu wa mpango huo kwa miaka mingi ijayo.

Kwa mujibu wa Faiza, Kadi ya Matibabu Zanzibar ni mfano bora unaoonyesha namna ambavyo matumizi ya teknolojia yanaweza kuimarisha utoaji wa huduma za afya kwa wote na kusaidia nchi za kipato cha chini na cha kati kufikia huduma jumuishi za afya kwa wote (UHC).

Tuzo hiyo ya WSIS imekuja wakati ambapo serikali nyingi duniani zinatafuta mifumo ya afya yenye usawa na inayostahimili changamoto mbalimbali.

Mpango wa ‘Zanzibar Matibabu Card’ tayari umesajili zaidi ya wananchi milioni 1.7, huku miundombinu ya kidijitali ikiruhusu hospitali na vituo vya afya vya jamii kushirikiana taarifa za wagonjwa kwa wakati halisi.

Comments

Popular posts from this blog

Airtel Foundation yazindua mpango wa udhamini wa masomo kwa vijana

ZAMECO yakerwa na video ya udhalilishaji mtandaoni