Ayoub ahimiza wazazi, walezi kushirikiana kuinua elimu

NA MWANDISHI WETU

MKUU wa mkoa wa Kusini Unguja, Ayoub Mohammed Mahmoud

WAZAZI na walezi wamehimizwa kuzidisha mashirikiano na walimu ili kuimarisa kiwango cha elimu na ufaulu wa watoto wao.

MKUU wa Mkoa wa Kusini Unguja, Ayoub Mohammed Mahmoud, ametoa wito huo wakati wa mahafali ya kwanza ya wananfuzi wa kidatoncha pili wa skuli ya sekondari Ghana iliyopo katika shehia ya Ghana, wilaya ya Kati mkoani humo.

Alisema ushirikiano kati ya pande mbili hizo ni nyenzo muhimu katika kutatua changamoto zinazowakabili wanafunzi pamoja na kufanikisha malengo ya walimu ambayo ni kuongeza ufaulu wakati wa mitihani ya taifa.

Alisema, kamati ya maendeleo ya elimu ya shehia hiyo imefanya kazi kubwa ya kuhakikisha inaanza ujenzi wa madarasa mengine mapya ili kusudi kuhamasisha wengine kuchangia ujenzi wa madarasa hayo.

Hivyo, aliwataka wananchi kuchangia miradi ya kijamii ikiwemo ujenzi wa madarasa katika skuli hiyo na kuahidi kuwa atawashauri wamiliki wa viwanda vya kokoto,viwanda vya matofali na mashimo ya kifusi waliopo mkoani humo kuchangia ujenzi wa skuli hiyo ili iendeleze ujenzi wa madarasa hayo.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa kamati ya maendeleo ya elimu katika shehia ya Ghana, Ali Mohammed Othman alisema kamati yake imefanikiwa kuongeza mwamko juu ya masuala ya elimu kuongeza ufaulu wa wanafunzi.

Alisema katika skuli yao waliweka kambi za wanafunzi wanaotarajiwa kufanya mitihani ya taifa pamoja na kuanzisha ujenzi wa vyumba vya madarasa mapya na kuongeza nafasi za kujisomea.

Nae mfanyabiashara, Said Nassir Bopar, katika hatua ya kuunga mkono juhudi za serikali za kuinua sekta ya elimu, aliahidi kuisaidia skuli hiyo mabati 150 kwa ajili ya kuezekea mabanda yaliyojengwa kwa nguvu za wananchi.

“Sambamba na mabati hayo, pia nitawapatia kompyuta tano ili ziongeze ufanisi kwa walimu na wanafunzi katika mitihani yao na kazi za kila siku,” alieleza Bopar.

Asilimia 79.29 ya wanafunzi wote wa kidato cha pili waliofanya mitihani ya taifa katika skuli hiyo, walifaulu na kuendelea na kidato cha tatu huku skuli hiyo ikikabiliwa na changamoto za uhaba na uchakavu wa majengo na kukosekana kwa hati miliki za maeneo ya skuli hiyo.

 


Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango