Bodi yatakiwa kutokuwa chanzo cha migogoro

NA MWANDISHI WETU

WAJUMBE wa Bodi ya Uhaulishaji Ardhi Zanzibar, wametakiwa kutokuwa chanzo cha migogoro ya ardhi na badala yake kuwa watatuzi wa migogoro hiyo kuwa mujibu wa sheria zilizopo.

Akizungumza na Wajumbe bodi hiyo ofisini kwao Forodhani, Waziri wa Wizara ya Ardhi na Maendeleo ya Makaazi, Riziki Pembe Juma, amesema kufanya hivyo kutasaidia kuondoa migogoro ambayo inaongezeka siku hadi siku.


Amesema miongoni mwa sheria zinazofanyiwa kazi imebainisha kila kitu ili kuhakikisha haki zinapatikana kwa wahusika wakiwemo wananchi wa hali ya chini, hivyo si vyema kufanya kazi kwa utashi wao binafsi.

“Sheria zilizopo zinaelekeza mambo yote yanayotakiwa na yasiyotakiwa kufanyiwa kazi, hivyo sio vyema kufanya kazi kwa utashi binafsi badala yake mfanye kazi kwa mujibu wa sheria zilizopo na sio kuwakandamiza wananchi ambao sisi ndio wanaotutegemea,” amesema Pembe.

Ameongeza kuwa ipo haja ya kukaa pamoja kati ya wajumbe wa bodi hiyo na kamisheni ya ardhi ili kuzifanyia mapitio na marekebisho sheria zenye mapungufu ili kuona zinakidhi mahitaji.

Nao Wajumbe wa Bodi hiyo, walisema kuwa miongoni mwa vikwazo wanavyokabiliana navyo ni baadhi ya wananchi kuuza maeneo kwa zaidi ya mtu mmoja hali inayopelekea kutomtambua mmiliki halali.

Wakati huo huo, Waziri Pembe, ameiagiza Kamisheni ya Ardhi kumpatia hati halali ya umiliki wa ardhi wa ekari moja iliyopo Jumbi, wilaya ya Kati Unguja Ali Talib baada ya kujiridhisha kuwa mmiliki halali wa eneo hilo.

Aidha amemtaka Saleh Karama aliedaiwa kuvamia eneo hilo na kuanzisha gereji kuhamia katika eneo jengine alilopangiwa kihalali.

Amesema, serikali imeamua kuyafatilia maeneo yote yenye migogoro ili kufahamu wamiliki halali na kila mwananchi apate haki yake kisheria.

Nae, Mmiliki wa eneo hilo, Ali Talib, ameishukuru serikali kupitia wizara hiyo kwa kummilikisha eneo hilo ambalo analimiliki tokea mwaka 2003 na kuiomba wizara kuyapatia ufumbuzi maeneo yote yenye migogoro ili wananchi waishi kwa amani.

Mkuu wa Kitengo cha eka na ardhi za kilimo, Omar Ameir Pandu, amesema ni vyema wananchi kufata sheria zilizopo za matumizi ya eka za kilimo na kuacha tabia za kuzitumia kwa shughuli za makaazi.

Ziara ya Waziri Pembe, ilikuwa na lengo la kuangalia maeneo mbali mbali yenye migogoro ambapo alitembelea Jumbi wilaya ya Kati, Kianga, Chuini na Kama wilaya ya Magharibi ‘A’, Unguja.

 

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango