Tumejipanga kuzikabili changamoto za wakulima wa mwani - Waziri

NA MWANDISHI WETU, PEMBA

IMEELEZWA kuwa mashirikiano ya wadau mbali mbali na serikali yatachochea kasi ya kuzitafutia ufumbuzi changamoto zinazowakabili wakulima wa mwani na zao hilo kwa ujumla.

Akifungua mafunzo ya wakufunzi wa wakulima wa mwani katika ukumbi wa Shirika la Biashara la Taifa Zanzibar (ZSTC), Wawi Pemba, Waziri wa Kilimo, Umwagiliaji, Maliasili na Mifugo, Dk. Soud Nahoda Hassan, alieleza kuwa kupitia dhana ya uchumi wa bluu zao hilo litaimarishwa ili kuongeza uzalishaji.


Waziri wa Kilimo, Umwagiliaji, Mliasili na Mifugo, Soud Nahoda Hassan akifungua mafunzo ya wakufunzi wa wakulima wa mwani.

Alisema changamoto nyingi zinatokana na mabadiliko ya tabia nchi, zimeathiri kwa kiasi kikubwa shughuli za kilimo hicho lakini wataalamu wameendelea kufanya utafiti wa kuzikabili ikiwa ni pamoja na uzalishaji wa mbegu zenye uwezo wa kukabiliana na mabadiliko ya hali ya hewa na maradhi.

“Juhudi zote hizo zinafanyika ili kuinua kipato na hali za wakulima, hivyo niwatie moyo serikali itaendelea kushirikiana na wadau kama REPOA (Taasisi ya Utafiti wa Sera na Maendeleo na Umaskini Afrika) katika kufikia malengo,” alisema Nahoda.

Aidha dk. Nahoda alieleza kuwa mipango ya serikali kujenga kiwanda cha kusarifu zao hilo itasaidia kutanua soko na kuongeza bei ya zao hilo jambo litakalokuza uchumi wa wakulima hao na Zanzibar kwa ujumla.

“Mahitaji ya kiwanda kinachojengwa ni tani 30,000 wakati uzalishaji kwa sasa ni chini ya tani 20,000 kwa mwaka hivyo ipo haja ya kutafuta mbinu za kuongeza uzalishaji utakaokidhi mahitaji ya kiwanda lakini pia kusafirisha nje,” aliongeza Dk. Nahoda.

Washiriki wa mafunzo ya wakufunzi wa wakulima wa mwani wakifuatilia mafunzo.

Awali akitoa taarifa kuhusiana na mafunzo hayo, katibu mkuu wa wizara ya biashara na maendeleo ya viwanda, Juma Hassan Reli, alisema yamelenga kuwajengea uwezo wakulima kuzalisha mwani katika maji makubwa kinyume na ilivyo sasa.

Alisema katika mafunzo hayo wakufunzi hao ambao wanatoka katika maeneo mbali mbali ya kisiwa cha pemba, watapatiwa mbinu za uzalishaji na namna ya kujikinga na madhara yanayotokana na uzalishaji wa mazao hayo.

Aidha aliongeza kuwa, pamoja na mafunzo, wizara yakle imeandaa sera ya mwani ambayo imelenga kuimarisha uzalishaji, kuongeza thamani na bei ya zao hilo.

“Kwa sasa ZSTC (Shirika la Biashara la Taifa) linanua mwani wa cotonee kwa shilingi 1,800 kwa kilo hivyo kupitia mafunzo haya tunaamini uzalishaji utaongezeka na kupata ziada ya tani 12,000 ambazo zitauzwa kwa wanunuzi wengine,” alieleza Reli.

Aliongeza kuwa hatua hiyo inawahakikishia wakulima wa mwani soko la uhakika na kuishukuru REPOA kwa kufanya tafiti za maendeleo ya zao hilo lakini pia kuwajengea uwezo wakulima na wadau wengine wa zao hilo kukuza uchumi.

Akizungumza na waandishi wa habari kando ya mafunzo hayo, Waziri Mstaafu wa Biashara na Viwanda, Balozi Amina Slaum Ali, aliipongeza serikali ya awamu ya nane kwa kuendeleza programu za maendeleo ya sekta ya mwani ambayo alisema imekuwa na mchango mkubwa kwa wananchi hasa wanawake.

Viongozi wa meza kuu wakiongozwa na Waziri wa Kilimo, Umwagiliaji, Maliasili na Mifugo (wa tatu kutoka kulia) Soud Nahoda Hassan wakiwa katika mafunzo hayo. Wa kwanza ni Balozi Amina Salum Ali, Waziri Msataafu wa Biashara na Viwanda.

“Kwa muda mrefu kilimo cha mwani kinafanywa na wanawake, wakati umefika kwa vijana wakiume na wananume kushiriki katika kilimo hiki na kuchangamkia fursa zinazopatikana kwani soko lipo na serikasali ipo tayari kusaidia,” alisema Balozi Amina.

Akitoa shukrani kwa niaba ya washiriki wengine wa mafunzo hayo, mkulima fatma Muhammad makame wa makangale, aliishukuru serikali na wadau mbali mbali kwa kuwapatia mafunzo hayo na mengine ambayo yamewawezesha kujikwamua kiuchumi.

“Mafunzo ya mara kwa mara yametujengea uwezo wa kusarifu mwani na kuzalisha bidhaa za chakula na matumizi ya nyumbani badala ya kuuza kama ulivyo kwa wafanyabiashara ambako bei ilikuwa sio nzuri sana,” alisema mkulima huyo.

Mafunzo hayo ya siku saba yatafanyika kwa nadharia na vitendo ambapo wakufunzi hao watajifunza njia mbali mbali za uzalishaji wa mwani katika maji makubwa, namna bora ya utunzaji na kuliongezea thamani zao hilo.

Baada ya kufungua mafunzo hayo, Dk. Nahoda akiambatana na maafisa wa taasisi ya REPOA walitembelea eneo lililotengwa kwa ajili ya kiwanda cha kusarifu mwani liliopo Chamanangwe, wilaya ya Wete, mkoa wa Kaskazini Pemba. 

 

  

 

 

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango