Waandishi watakiwa kutumia fursa kujiendeleza

NA ASYA HASSAN

WAANDISHI wa habari nchini wamesisitizwa kutumia fursa mbalimbali zinazotolewa ili kuwajengea uwezo, uelewa, kujitangaza ili kuongeza ufanishi katika kazi zao na maendeleo ya taifa kwa ujumla.

Hayo yameelezwa na Mwenyekiti wa klabu ya waandishi wa habari zanzibar (ZPC), Abdallah Abdulrahman Mfaume, alipokuwa akizungumza katika kikao cha pamoja cha wanachama na viongozi wa jumuiya hiyo kilichofanyika katika ofisi za klabu hiyo Kijangwani mjini Unguja.

Baadhi ya wanachama wa ZPC waliofanya na kuwasilisha habari za kukuza uelewa juu ya maradhi ya mripuko wakiwa katika kikao maalum kilichofanyika katika ofisi za klabu hiyo Kijangwani, Zanzibar.

Mfaume aliwasisitiza waandishi kutumia kalamu zao vizuri pamoja na kufuata sheria na maadili ya kazi zao ili kukuza ustawi wa jamii na kutunza amani iliyopo.

Alisema uandishi wa habari ni kada inayotegemewa kuchochea mabadiliko na maendeleo katika jamii hivyo waandishi wanapaswa kutambua wajibu wa kutunza amani na kutokuwa chanzo cha kuivuruga na kuisababisha nchi kuingia katika migogoro.

“Wakati tulionao waandishi tunatakiwa kujibiisha na kujifunza kila mara ili tuweze kuielimisha jamii, kuiasa na kuhimiza jamii juu ya mambo mbali mbali yanayowahushu hasa amani na utulivu,” alisema Mfaume.

Aidha Mwenyekiti huyo aliwataka wananchama hao kuacha tabia ya kukatishana tamaa, badala yake washirikiana na kusaidiana ili kuinya fani hiyo kuendelea kuwa na hadhi lakini pia tija kwa jamii nzima.

Awali Katibu Mkuu wa ZPC, Mwinyimvua Abdi Nzukwi aliwapongeza waandishi hao kwa kujitokeza na kutumia fursa mbalimbali zinazojitikeza ili zileta tija kwao na taifa kwa ujumla.

Alisema ni vyema kwa kila mwandishi akachangamkia fursa hizo kwani zinatoa nafasi ya kukukuza ujuzi wao lakini pia kusaidia jamii.

Alisema kupitia umoja wao, fursa nyingi hujitokeza hivyo ni vyema kwa waandishi kuzitumia kwa namna moja au nyengine kwani zinawasaidia kujitangaza na kuleta mabadiliko katika kutekeleza majukumu yao.

Alizitaja baadhi ya fursa hizo kuwa pamoja na mafunzo kwa wandishi wa habari na mashindano yanayolenga kuongeza uelewa wa jamii juu ya mambo mbali mbali lakini pia kujenga uwezo wa mwandishi binafsi.

“Mnaweza kuona mmefanya jambo la kawaida, lakini kazi za uandishi mlizozitoa kwenye vyombo vyenu zimekuwa na mchango mkubwa katika mabadiliko ya jamii yetu, tuendelee kuzifanya hata baada ya hapa,” alisisitiza Nzukwi.

Aidha Katibu huyo alitumia fursa hiyo kutambulisha mradi wa ujenzi wa amani, uvumilivu wa kisiasa na uwezo wa jamii kupokea tofauti za maoni unaofadhiliwa na shirika la internews na kuwaomba waandishi wa habari kuendelea kuandika habari zitakazoimarisha umoja miongoni mwa jamii.

Wakizungumza katika kikao hicho, wanachama hao waliomba viongozi hao kuendelea kutafuta fursa za mafuno kwa waandishi wa habari ili kuimarisha utendaji wao kulingana na wakati uliopo.

Walieleza kuwa, uandishi wa habari za magonjwa ya miripuko ikiwemo covid 19, umewapa nafasi ya kujua zaidi kuhusu maradhi hayo.

“Tunawashukuru kwa fursa hii lakini tunawaomba viongozi muendelee kutusaidia kwa kutuunganisha katika fursa mbali mbali zinazotokezea ili tuzidi kujielimisha, kujitangaza na kuongeza kipato”, alieleza mmoja ya wanachama hao.

Kikao hicho kilichofuatiwa na kikao cha kamati tendaji cha klabu hiyo, kilipitia kazi zilizofanywa na waandishi hao kupitia mpango wa kujenga uelewa wa jamii juu ya maradhi ya miripuko uliofadhiliwa na Shirika la Maendeleo la Sweden (SIDA) unaosimamiwa na Muungano wa Klabu za Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC). 

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango