Wanahabari endelezeni uzalendo, kuhamasisha amani – RC Kitwana

NA ASYA HASSAN

MKUU wa Mkoa wa Mjini Magharibi, Idrissa Kitwana Mustafa, amesema vyombo vya habari vina wajibu mkubwa wa kuendelea kushajiisha jamii juu kuongeza mshikamano, kutunza amani na kuvumiliana.













MKUU wa mkoa wa Mjini Magharibi Idrissa Kitwana akifungua semina hiyo. Kushoto ni Mwenyekiti wa ZPC, Abdalla Mfaume.

Ameeleza hayo wakati akifungua mafunzo ya siku mbili kwa waandishi wa habari yenye lengo la kuwajengea uwezo wa kuandika habari zinazohamasisha amani, umoja, mshikamano na mtangamano wa kijamii baada ya uchaguzi yaliyofanyika Kidongo Chekundu, Zanzibar.

Mafunzo hayo yaliyoandaliwa na Klabu ya Waandishi wa Habari Zanzibar (ZPC) kwa kushirikiana na Shirika la Internews Tanzania, ni sehemu ya utekelezaji wa mradi wa kukuza amani katika jamii.

Waandishi wa habari wanachama wa ZPC wakiwa katika mafunzo ya uandishi wa kuhamasisha amani.

Alisema amani, umoja na mshikamano ni muhimu katika nchi yoyote kwani ndio msingi wa maendeleo na kuchochea ukuaji wa uchumi.

Alisema, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi, anasisitiza amani, utulivu na mshikamano wa jamii katika kujenga nchi yenye maendeleo, hivyo vyombo vya habari vinapaswa kuandaa habari na vipindi vitakavyoimarisha umoja na mshikamano wa wazanzibari badala ya kuwagawa.

"Hakuna kitu muhimu na chenye thamani zaidi ya uzanzibari na umoja wetu, kwani huo ndio msingi imara utakaochochea kasi ya maendeleo ya nchi yetu,” alisema.

Waandishi wa habari, wanachama wa ZPC wakifuatilia uwasilishaji mada katika mafunzo ya uandishi wa kuhamasisha amani.

Alisema nchi isiyokuwa na amani haiwezi kupata maendeleo, hivyo ni lazima amani iwepo kwa kila kundi katika jamii.

Akitolea mfano wa nchi zilizoingia katika machafuko, Kitwana alisema zimeingia katika migogoro kutokana na sababu mbali mbali ikiwemo uchochezi uliofanywa na waandishi wa habari, hivyo aliwataka waandishi wa habari kujifunza makosa ya wenzao.

Aliwapongeza waandishi wa habari kwa kazi kubwa waliyoifanya wakati wa uchaguzi mkuu kwa kutoa taarifa ambazo zilichangia kupatikana kwa amani na upendo miongoni mwa jamii.

"Dhima hii ni yetu sote na mlifanya kazi hii kwa kuamini kwamba nanyi mnahusika katika ujenzi wa amani kwani kazi hii ilikuwa tuifanye sisi viongozi wa siasa katika majukwaa yetu,” alisema.

Aidha aliishukuru ZPC kwa kuandaa mafunzo hayo na kuwashajiisha wanachama wake kuona umuhimu wa kuhamasisha amani, utulivu na mshikamano wa kijamii katika maeneo yao.

"Naamini kama mtatumia kalamu zenu na midomo yenu vizuri na kuongeza hamasa ya kuwaona ya kuhakikisha wazanzibari wanabaki katika hali ya amani na utulivu, bila shaka mtakuwa mnathibitisha uzalendo wenu," alisema.

Akizungumzia ushirikiano kati ya ofisi yake na waandishi wa habari, aliwasisitiza watumishi walio chini yake kutoa ushirikiano kwa waandishi wa habari wanapokwenda kufuata taarifa kwao.

Alisema mtumishi yeyote ambaye hatotoa ushirikiano kwa wandishi wa habari na kuficha taarifa atashughulikiwa.

Aliwashauri Wanahabari na vyombo vya habari kuibua changamoto zinazotokea katika jamii kwa lengo la kuisaidia serikali ya awamu ya nane kufikia malengo yake.

Mapema Mwenyekiti wa ZPC, Abdalla Abdulrahman Mfaume, alisema mafunzo hayo yanayofadhiliwa na shirika la Internews ni muhimu katika ujenzi wa jamii yenye mshikamano na umoja.


MWENYEKITI wa ZPC, Abdallah Mfaume, akitoa maelezo ya kumkaribisha mgeni rasmi katika mafunzo ya kuhamasisha amani, uvumilivu wa kisiasa na utamaduni wa kupokea maoni tofauti.

Mapema mtoa mada, Ali Nassor Sultan, alisema waandishi wa habari wana wajibu wa kuhamasisha ujenzi wa jamii yenye mshikamano.

Hata hivyo, aliwahimiza wanapoandika habari zao wasipuuze mawazo mbada kutoka makundi mengine katika jamii.

MWANDISHI wa habari mwMWANDISHI wa habari mwandamizi Ali Sultan (aliesimama) akiwasilisha mada ya maadili ya uandishi wa habari na uandishi wa habari za amani (peace journalism).

Katika mafunzo hayo ambayo ni sehemu ya utekelezaji wa mradi wa kujenga amani, uvumilivu wa kisiasa na utamaduni wa kupokea maoni tofauti unaotekelezwa na ZPC kwa ufadhili wa Internews, mada mbalimbali ziliwasilishwa ikiwemo ya wajibu wa vyombo vya habari katika kudumisha amani na umoja wa kitaifa baada ya uchaguzi.

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango