Soraga aitaka ZBS kuzingatia maslahi ya umma, kudhiti ubora


NA MWAJUMA JUMA

KAIMU Waziri wa Biashara na Maendeleo ya Viwanda, Mudrik Ramadhan Soraga, (pichani) amewataka watendaji wa Taasisi ya Viwango Zanzibar (ZBS), kuweka mbele maslahi ya nchi wanapofanya ukaguzi wa bidhaa na  kuacha mapatano na wafanyabiashara  kwa bidhaa zisizokuwa haina ubora.

Akizungumza na watendaji wa taasisi hiyo iliyopo Amani viwanda vidogo vidogo alisema kuwa ZBS ni taasisi inayosimamia viwango na watendaji wake wanapaswa kuwa makini na kutambua kuwa wanapaswa kuwa mstari wa mbele kulinda afya za wananchi na mazingira.

“Katika hali ya kawaida nchi ya kisiwa inakuwa kama chambo kwa kuingizwa kila kitu, ikiwa bidhaa zinaingizwa pasi na kufuata utaratibu matokeo yake utakuta bidhaa hatarishi kwa afya za watu zinazagaa mitaani,” alieleza.

Soraga ambae pia ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Kazi, Uwekezaji na Uchumi, alisema kuna baadhi ya wafanyabiashara wanaingiza bidhaa ambazo hazina viwango hivyo ipo haja kuhakikisha wanakuwa wakali katika usimamizi maeneo yao ya kazi.

“Tusije tukashawishika tukaacha uzalendo wetu nyuma kwa sababu tu mtu ametoa shilingi mbili tatu, tutakua hatuwatendei haki wananchi wetu ambao sisi kama watoa huduma wametuamini kwamba ndio walinzi wao,” alisema.

Alisema kuwa katika kuona umuhimu huo ameona ni vyema akakutana na watendaji hao kuwasikiliza ili kuhakikisha bidhaa zinazoingizwa nchini zinakidhi viwango na salama kwa matumizi ya binadamu na rafiki kwa mazingira.

Aidha alieleza kuwa ana imani na wafanyakazi wa ZBS na kwamba wanatambua jukumu lao la kuhakikisha kwamba wanalinda na bidhaa ambazo zinaingizwa zinakuwa na viwango bora kwa afya za wananchi ambao wamewaamini sana.

Aidha alitaka ufafanuzi juu ya viwango kwa bidhaa zilizotumika kwa vifaa vya umeme vinavyoingizwa nchini kwa wingi hasa zile ambazo zimepigwa marufuku tangu 1998.

Hata hivyo alisema kuwa licha ya kuwa na changamoto lakini wamekuwa wakitekeleza vyema majukumu yao na wao kama Serikali watahakikisha wanaweka vitendea kazi ili waweze kufanya Kazi kwa ufanisi.

Alisema vifaa vya maabara hasa vya ‘microbiology’ ni muhimu kwa sababu kutegemea mtu wa pili katika upasishaji sio mzuri kwani wanatakiwa wazisimamie wenyewe hasa kwa vile huwezi kujuwa huko unakopeleka na mtu anaetakiwa ahakikiwe anaukaribu gani na huko.

Awali Mkurugenzi Mkuu wa ZBS, Rahima Ali Bakari, alisema tasisi hiyo ina changamoto kadhaa ikiwemo ya kutokuwepo kwa mfumo wa ukaguzi bandarini utakaoiwezesha taasisi hiyo kujua mapema bidhaa zinazoingizwa ili kuzifanyia ukaguzi kabla ya kuruhusiwa kuingia nchini.

Alisema kuwa mfumo ambao upo kwa sasa sio shirikishi na watendaji wa Shirika hilo wamekuwa wakiifanya taasisi yao kuwa ni ya mwisho wakati wao ZBS wanatakiwa kuwa wa mwanzo kujuwa kabla ya bidhaa kuweza kutolewa.

Aliitaja changamoto nyengine kuwa ni kutokuwa na fursa ya kufanya ukaguzi katika maeneo ya uwanja wa ndege kutokana na kutokuwepo kwa eneo licha ya kufuatilia upatikanaji wa eneo hilo bila ya mafanikio.

Aidha alisema kuwa Idara ya maendeleo ya viwango wameshakuwa na viwango 328 ambavyo vimeshatangazwa kuwa na viwango 29 vilivikabidhiwa kwa Waziri wa biashara na viwanda ya awamu ya saba kwa kutangaza ambapo kukamilika kwake kutaifanya Zanzibar kuwa na viwango 357 ikiwemi ni viwango vya chakula na kilimo, kemikali, uhandisi mitambo na viwango vya mazingira.

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango