Soraga awataka wajasiriamali kujengeana uwezo kibiashara


NA MWAMDISHI WETU

WAJASIRIAMALI wadogo wadogo na wafanyabiashara wametakiwa kutumia matamasha ya kibiashara kujengeana uwezo, umoja na kupeana taarifa zitakazoimarisha biashara nchini.

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais, Kazi, Uchumi na Uwekezaji, Mudrik Ramadhan Soraga ambae pia ni Kaimu waziri wa Biashara na maendeleo ya Viwanda, alieleza hayo alipokuwa akifunga tamsha la saba la biashara katika viwanja vya Maisara Suleiman, mjini Unguja.

Alisema iwapo wadau wa biashara wataendelea kuunga mkono matamasha hayo, mipango ya serikali kuwawezesha kutangaza biashara zao utafanikiwa na kuleta tija kwa jamii nzima.

Alieleza wizara yake ina mpango wa kuweka tamasha hilo mara mbili kwa mwaka ili kutanua wigo kwa wajasiriamali, wafanyabiashara na taasisi za umma pamoja na binafsi kutangaza biashara na huduma wanazozitoa kwa jamii.

Alisema kuwa wizara imefarajika na kupata matumaini makubwa kuona wanaendelea kushiriki katika maonyesho jambo alilosema litaendelea kuungwa mkono na wizara hiyo kufanikisha matamasha kama hayo.

“Nitumie fursa hii pia kuwaomba kusajili biashara na shughuli zenu kwa kutumia mifumo ya kidigitali iliyopo ili muweze kutambulika kisheria na kurahisisha ulipaji wa kodi ya serikali,” alieleza Soraga.

Aidha Waziri huyo alirejea wito wa kuwaomba wawekezaji kujitokeza na kuwekeza Zanzibar kwani Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi, ameahidi kupunguza kodi kwa wawekezaji na wafanyabiashara wa bidhaa wanazozalisha au kuzileta nchini.

Akimkaribisha Waziri huyo, Katibu Mkuu, Wizara ya Biashara na Maendeleo ya Viwanda, Juma Hassan Reli, alisema kuwa tamasha hilo limefana kutokana na ushirikiano wa wafanyabiashara na waandishi wa habari ambao wamelitangaza tamasha hilo lililofunguliwa na Makamu wa rais wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan.

“Tamasha hili limefanikiwa kwa zaidi ya asilimia 90 ambapo limewakutanisha wafanyabiashara mbalimbali pamoja na wanunuzi sambamba na kuwajengea uzoefu wafanyabiashara na mauzo yameongezeka.

Naye, Mkurugenzi Mtendaji wa Jumuiya ya Wafanyabiashara wenye Viwanda na Wakulima, Hamad Hamad, alisema nia njema ya serikali kwa wafanyabiashara kutaka kuwakuza wafanyabiashara hivyo waliahidi kuiunga mkono serikali ili kufanya kazi zao ipasavyo.

“Jambo la busara kuwekwa kwa wajasiriamali mbalimbali kwani wanaweza kubadilishana uzoefu wa biashara hizo kuweza kuwa na kiwango cha juu na kuweza kuuzika katika soko la ndani na nje ya nchi,” alieleza Hamad.

Nao baadhi ya washiriki wa maonyesho hayo, walieleza kuwa yamewapa nafasi ya kutangaza biashara na shughuli wanazozifanya jambo ambalo limeongeza ufanisi wa kibiashara.

Meneja wa Benki ya NMB kanda ya Zanzibar, Abdallah Duchi, alisema benki hiyo inawathamini wajasiriamali na wafanyabiashara wadogo wadogo hivyo itaendelea kuunga mkono jitihada zao wanazozifanya.

“Tumejipanga kutoa suluhisho la huduma za kifedha, kwa kuwa na mfumo bora zaidi wa ubadilishaji fedha na biashara ya kadi,” alieleza Duchi.

Aidha Duchi aliishukuru Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kuwaonesha fursa kupitia kwenye uchumi wa buluu, ambapo NMB wamekuwa na uzoefu wa biashara hizo.

Naye Meneja wa Zanzibar Cable Televisheni, Hafidh Kassim, aliahidi kushiriki kadri itakavyowezekana katika tamasha hilo ili iwe ni moja ya kuendelea kuwapatia wananchi habari kupitia vyombo vyao vya habari.

Katika tamasha hilo washiriki zaidi ya 360 wameshiriki katika tamasha hilo lililoanza Januari 5 hadi 15 mwaka huu ambalo ni sehemu ya maadhimisho ya miaka 57 ya mapinduzi ya Zanzibar yaliyofikia kilele chake Januari 12, mwaka huu katika viwanja vya Mnazi Mmoja.

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango