Wizara yajipanga kuongeza ufanisi awamu ya pili TASAF


NA MWANDISHI WETU

SERIKALI ya Mapinduzi Zanzibar imesema itahakikisha utekelezaji wa awamu ya pili ya mradi wa kunusuru kaya maskini unaofadhiliwa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii Tanzania (TASAF) unaangalia mahitaji ya walengwa na wanaostahiki kupatiwa huduma zikiwemo za fedha taslimu.

Hatua hiyo imeelezwa itawezekana kwa kuwashirikisha wakaazi wa vijijini na shehia husika ili kupatikana kwa walengwa wanaokusudiwa kuingia katika mpamgo huo.

Waziri  wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais, Sera, Utatibu na Baraza la Wawakilishi, Dk. Khalid Salum Mohamed, alieleza hayo wakati akizungumza na wajumbe wa Kamati ya kusimamia Ofisi za Viongozi Wakuu wa Serikali katika ukumbi wa wizara hiyo Vuga, mjini Zanzibar.

Alisema utekelezaji huo unalenga kuimarisha maisha ya kaya maskini kupitia mradi huo yanatimia na watendaji wanaosimamia jukumu hilo wanatimiza   masharti na vigezo vilivyowekwa katika kuzifikia kaya hizo.

Alisema, eneo jengine ambalo litakalosimamiwa ipasavyo ni kuona miradi inayoekezwa ndani ya jamii iwe yenye mahitaji ya watu wa maeneo husika na kuleta manufaa ndani ya jamii.

Alisema, miradi inayofadhiliwa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) inalazimika kuzingatia sheria na kufuatia miongozo iliyowekwa na serikali badala ya maslahi binafsi ya viongozi wa majimbo au watendaji wa serikali.

“Lazima viongozi na watendaji wanaosimamia miradi ilyopo chini ya TASAF wafuate sheria na taratibu zilizopo bila ya kujali ama kuangalia maslahi binafsi ya viongozi,” alieleza waziri huyo.

Akizungumzia fedha za mfuko wa jimbo, Dk. Khalid, alisema ofisi yake haitokuwa na muhali badala yake itahakikisha inasimamia sheria na taratibu zilizowekwa kuhakikisha fedha hizo zinaleta tija kwa umma.

“Nitakuwa mkali na kufuatilia kwa karibu matumizi ya fedha za mfuko wa jimbo kwani zinatolewa kwa ajili ya kuimarisha huduma za jamii hivyo viongozi lazima tuheshimu sheria zilizopo,” alisema.

Nae Mratibu wa TASAF Ofisi ya Makamu wa Pili, Khalid Hamrani, alisema wa awamu ya pili ya mradi huo, utawashirikisha ipasavyo  watendaji wa ofisi hiyo na ambae atabainika kwenda kinyume ma utaratibu atachukuliwa hatua za kinidhamu na kisheria.

Alisema hatua hiyo imekuja baada ya kubaini kuwepo kwa changamoto zilizojitokeza katika mradi uliomalizika kwa kuorodheshwa watu wengine ambao waliokuwa sio walengwa.

“Waajiriwa wa serikali katika ofisi yetu ndio tutakaowatumia na asiewajibika vyema sheria itachukua mkondo wake ikiwa ni pamoja na kukatwa mshahara pale itapobainika ametoa fedha kwa mtu ambae sio mlengwa,” alisema.

Alifahamisha kuwa mradi huo ambao unatarajiwa kuanza kutekelezwa Febuari mwaka huu tayari uhakiki umeshafanywa na hata hivyo zoezi la kushirikishwa jamii katika utambuzi wa walengwa litasimamiwa ipasavyo.

Alifahamisha miongoni mwa mambo mengine yatakayotekelezwa katika mradi huo awamu hii ni kutumia teknolojia kuwatambua ili kuthibiti watu wasio walengwa.

Alisema utafiti uliofanywa umebaini Zanzibar kulikuwa hakuna wanufaika hewa ndani ya mradi huo isipokuwa kulikuwa na idadi kubwa ya walengwa wasiostahiki hali iliyochangiwa na wasimamizi wa walengwa wa mradi huo (SMC).

Alisema watu wengine waliobainika katika utafiti huo ni kuandikishwa watu wasio na sifa ya kuingia katika mradi huo.

Mapema Mwakilishi wa jimbo la Ziwani, Suleiman Makame Ali, alimuomba Dk. Khalid kusimamia kwa karibu mradi huo hasa ikizingatiwa wapo baadhi ya masheha wamekuwa wakitumia fursa hiyo kwa kuingiza familia au watu wakatibu na wale walengwa wakaendelea kukosa kuitumia fursa hiyo.

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango