DC Suzan ataka waliokopa warudishe mikopo kwa wakati


NA MWANDISHI WETU

MKUU wa Wilaya ya Magharibi ‘A’, Suzan Peter Kunambi (pichani), amewataka wanaushirika wa kuweka na kukopa Kibweni (Kibweni Saccos) kurejesha mikopo kwa wakati ili kuendeleza ushirika huo.

Alisema hayo katika Skuli ya Bububu, wilayani humo alipofungua mkutano mkuu wa mwaka wa chama hicho na kusema umefika wakati kwa wanaushirika kutilia mkazo umuhimu wa kurejesha mikopo katika vyama vyao na faida inayopatikana iwanufaishe wote.

Alisema tabia ya wanachama kuchukua mikopo kisha kushindwa kurejesha kwa wakati inasababisha vyama vya ushirika kushindwa kujiendesha wenyewe na na hatimae kusubiri wahisani.

Kunambi alisema vyama vya ushirika ni muhimu katika maendeleo ya nchi na inasaidia kuinua uchumi kwa mwananchi mmoja mmoja hivyo aliwataka wanaushirika kuibua miradi ya maendeleo kuendeleza vyama hivyo.

Aidha aliwapongeza wana ushirika hao kwa kuanzisha ushirika imara ambao umekuwa mfano ndani ya wilaya hiyo na kuwahamasishana wananchi wengine kuingia katika ushirika huo ili kuongeza idadi ya wananchama na kuleta mabadiliko ya kiutendaji.

“Tunahaki ya kuwaelimisha na wengine waingie kwenye ushirika huu tupate maendeleo ya kweli kupitia vyama vya ushirika,” alisema.

Akizungumzia suala la udhalilishaji wa kijinsia, aliwataka wanaushirika hao kupiga vita vitendo hivyo katika jamii ili kuwanusuru watoto na wanawake dhidi ya vitendo hivyo.

Mapema Mrajis wa vyama vya ushirika Wilaya ya Magharibi ‘A’, Abulmajid Masoud Khalfan, alisema licha ya mafanikio yaliyopatikana kwa wanaushirika huo lakini elimu juu ya masuala ya mikopo inahitajika kwa wanachama wake pamoja na mbinu za kuendesha biashara ndogondogo na kubwa kwenye ushirika wao.

Nae Mwenyekiti wa ushirika huo, Abdurahman Khalfan, alisema wanakabiliwa na ukosefu wa kiwanja pamoja na jengo la kuendeshea ushirika wao hali inayosababisha kuendeleza harakati zao kwenye jengo la kukodi.

Hata hivyo walimuomba Mkuu huyo kuwapatia eneo ili wajenge ofisi ya kudumu na badala yake waondokane na usumbufu wanaoupata kwa kuazima jengo.

Akisoma risala Mjumbe wa kamati ya uongozi wa ushirika huo, Mboja Muhidini Masoud, alisema ushirika huo umepiga hatua kwa kukopeshawa mikopo kutoka shilingi 50,000 hadi kufikia shilingi 8,000,000 kwa mtu mmoja mmoja.

SACOS hiyo ilianzishwa mwaka 2007 na kupata usajili mwaka 2008 ilianza na wanachama 66 wanawake 55 na wanaume 11 na hadi sasa ina wanachama 108.

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango