Skuli ya Upendo yapongezwa kutoa mwanafuzi bora kitaifa

Yatoa wanafunzi watatu bora kitaifa mitihani STD 4, Veronica Mwendesha ashika nafasi ya kwanza Zanzibar

NA MWINYIMVUA NZUKWI

VIONGOZI wa jimbo la Bububu, wilaya ya Magharibi ‘A’, Unguja, wameeleza kuwa wataendelea kutoa kipaumbele kwa maendeleo ya jamii ikiwemo elimu ili kupata taifa linalojitegemea kwa wataalamu.

Kauli hiyo imetolewa na Diwani wa wadi ya Dole, Juma Wiliam Sungwa, kwa niaba ya Mwakilishi wa jimbo hilo Mudrik Ramadhan Soraga, katika hafla ya kuwapongeza wanafunzi wa skuli ya maandalizi na msingi, Upendo iliyopo shehia ya Kizimbani Unguja, iliyotoa mwanafunzi bora kitaifa katika mitihani ya darasa la nne iliyofanyika mwaka uliopita Zanzibar.

Alisema mafaniko ya skuli hiyo kutoa wanafunzi watatu katika nafasi tano za juu kitaifa katika mitihani hiyo ni ya kupongezwa na inapaswa kuungwa mkono na kila mmoja miongoni mwa wananchi wa jimbo hilo.

Alifafanua kuwa licha ya kuwa skuli hiyo kumilikiwa na taasisi binafsi, bado serikali na viongozi hao wanapaswa kuisadia kutokana na mchango inaoutoa katika ujenzi wa taifa la wasomi watakaoitumikia Zanzibar.

“Kutoa wanafunzi watatu katika nafasi tano za juu kitaifa sio mafanikio ya kupuuzwa, lazima tujivunie kuwa na mwanafunzi bora kitaifa lakini kujipanga kuhakikisha watoto wetu wanafikia malengo yao,” alisema Sungwa.

Akizungumzia changamoto zinazoikabili skuli hiyo na nyengine ndani ya jimbo hilo, Sungwa alisema zitapatiwa ufumbuzi hatua kwa hatua kwa kushirikiana na manispaa ya Magharibi ‘A’, Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali pamoja na wadau wengine wa elimu wa ndani na nje ya jimbo hilo.

“Hili la upungufu wa vitabu vya kiada na ziada vinavyofuata mtaala wa SMZ, tunalichukua pamoja na zile changamoto nyengine na katika muda mfupi ujao tutalipatia ufumbuzi,” alisema diwani huyo.

Akizungumza katika hafla hiyo iliyoambatana na utoaji wa zawadi kwa wanafunzi waliofanya vyema na wengine wa skuli hiyo, mdhamini wa skuli hiyo, Younggum Park (Mama Park), alipongeza juhudi za wazazi na walezi wa skuli hiyo kwa kutoa kipaumbele cha elimu kwa watoto wao.

“Katika baadhi ya maeneo, watu hawaipi elimu kipaumbele cha kwanza kwa watoto wao hasa wasichana, lakini watu wa eneo hili wamekuwa tofauti, ninawapongeza sana,” alieleza Mama Park.

Akisoma risala ya skuli hiyo, mwalimu Ezekiel Jackson, alieleza kuwa mwaka 2020, skuli hiyo iliyoanzishwa mwaka 2016, imetoa wanafunzi watatu katika nafasi ya kwanza, nafasi ya tatu na ya nne katika mitihani ya darasa la nne kitaifa.

“Kwetu haya ni muendelezo wa mafanikio, kwani katika mwaka 2019 tulifanikiwa kutoa mwanafunzi alieshika nafasi ya kwanza kitaifa katika mitihani ya darasa la nne kiwilaya, kimkoa na kitaifa kama ilivyokuwa katika mwaka 2020,” alieleza mwalimu huyo.

Ezekiel aliwataja wanafunzi waliopata ufaulu huo kuwa ni Veronica Paulo Mwendesha alieshika nafasi ya kwanza, Christina Kurwa alieshika nafasi ya tatu na Sleyum Rashid Said, alieshika nafasi ya nne ambap skuli hiyo ilifaulisha wanafunzi 22 kwa daraja ‘A’, wawili daraja ‘B’ na mmoja daraja ‘C’.

Hivi karibuni akizungumza katika hafla ya kuwapongeza wanafunzi waliofaulu michepuo katika skuli ya Langoni Msingi, Mkurugenzi Msaidizi Elimu, manispaa ya Magharibi ‘A’, mwalim Ahmed Abdulmajid aliyataja matokeo hayo kuwa ni mafanikio ya kujivunia na yanayohitaji kuendelezwa.

“Katika mitihani iliyopita, wilaya yetu ilishika nafasi ya kwanza katika mitihani ya darasa la nne na zaidi ya wanafunzi watatu walitokea katika nafasi 10 bora katika kiwilaya na kimkoa, haya ni mafanikio makubwa hasa kwa watoto wa maeneo haya,” alieleza.

Akielezea mikakati ya baadae, Mwalimu Mkuu wa skuli hiyo Elia John Maleso, alisema ni kuendelea kufanya vyema hivyo aliwaomba wananchi kuendelea kushirikiana na kuwapongeza viongozi hao wa jimbo kwa kutambua mafanikio ya skuli hiyo.

“Lengo letu ni kushika nafasi ya kwanza kila mwaka na kwa kuzingatia kuwa mwaka huu tutakua na darasa la sita, niwaombe wazazi waendelee kuwasaidia watoto wao kufaulu michipuo na kujenga msingi bora wa maisha yao,” alieleza mwalimu Elia.

Katika mahafali hayo mbali ya zawadi ya vifaa vya skuli, mwanafunzi Veronica Paulo Mwendesha na wenzake walikabidhiwa zawadi mbali mbali zilizotolewa na madiwani wa jimbo la Bububu na Mama Park anaeidhamini skuli hiyo.

 

PICHA.

MWANAFUNZI Veronica Paulo Mwendesha, akipandisha bendera kuashiria heshima aliyoipa skuli ya Awali na Msingi Upendo na wilaya ya Magharibi 'A' katika mitihani hiyo.


DIWANI wa wadi ya Dole, jimbo la Bububu Juma Wiliam Sungu akipanda mti katika eneo la skuli ya Awali na Msingi Upendo, wilaya ya Magharibi 'A' wakati wa hafla ya kuwapongeza wanafunzi vyema katika mitihani ya darasa la nne kitaifa.

MWANAFUNZI Veronica Paulo Mwendesha, akipanda mti wa ukumbusho katika eneo la skuli ya Awali na Msingi Upendo baada ya kutokea wa kwanza kitaifa katika mitihani ya darasa la nne kitaifa.

MWANAFUNZI Veronica Paulo Mwendesha, akiwa pamoja na wazazi wake wakati wa sherehe za kuwapongeza kwa kufanya vyema kwenye mitihani ya darasa la nne kitaifa.

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango