Ayoub ataja vipaumbele Kaskazini Unguja, apiga marufuku ‘vigodoro’


MWASHUNGI TAHIR, MAELEZO 

MKUU wa Mkoa Kaskazini Unguja, Ayoub Mohammed Mahmoud, ameeleza kuwa serikali ya huo umelenga kukuza sekta ya utalii kwa kuvitangaza na kuviendeleza vivutio vya utalii vilivyomo mkoani humo.

Ayoub alieleza hayo ofisini kwake Mkokotoni, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuzungumzia utekelezaji wa kazi za serikali ya mkoa huo katika kipindi cha miaka mitano ijayo.

Alieleza kuwa mkoa huo una vivutio vingi na maeneo ya mahoteli na mikahawa mikubwa, fukwe zinazovutia na maeneo ya kihistoria ambayo wageni na wenyeji wanapasa kuyajua.

Aliongeza kuwa pamoja na kuimarisha sekta hiyo, katika kipindi cha miaka mitano pia mkazo zaidi utawekwa katika ukuzaji wa sekta zinazokuza ustawi wa jamii zikiwemo za kilimo, mifugo, maji safi na salama, elimu, afya, miundombinu ya barabara na michezo.

“Pia kwa kuzingatia mipango ya serikali kuu, serikali ya mkoa itaendelea kuhamasisha ujenzi wa viwanda vipya na kuviendeleza vilivyopo ili kukuza ajira lakini pia wakulima wetu wapate soko la mazao wanayozalisha,” alieleza Ayoub.

Alisema hatua hiyo itaimarisha uzalishaji wa mazao mbali mbali yakiwemo ya mananasi na mboga mboga ili wakulima wapate kuepukane na hasara katika mazao yao wanayolima kila msimu.

Sambamba na hayo alisema serikali ya mkoa kwa kushirikiana na serikali kuu, imejipanga kudhibiti vitendo vya udhalilishaji, matumizi ya dawa za kulevya na rushwa kwa kutovifumbia macho kwani vinarudisha nyuma maendeleo ya taifa.     

Aidha Ayoub aliahidi kulisimamia suala la kilimo cha umwagiliaji maji, kuimarisha ufugaji na kuweka mazingira kuwa katika hali ya usafi. 

Sambamba na hayo, katika kuimarisha maadili, amepiga marufuku ya upigaji ngoma za vigodoro pamoja na khanga moja katika maeneo ya mkoa huo kwa kuwa zinaenda kinyume na mila, silka na utamaduni wa Zanzibar.

 “Kuanzia leo si ruhusa kwa wakaazi wa mkoa huu na wananchi kutoka sehemu nyengine  kuja kupiga ngoma na kucheza ngoma hizo kwani zimekosa  maadili”, alisema Ayoub.

Katika taarifa yake hiyo ayoub pia alipongeza juhudi za rais wa Zanzibar na mwenyekiti wa baraza la mapinduzi, dk. Hussein ali mwinyi na kuahidi kutekeleza maagizo yote aliyoyatoa ili kuongeza ufanisi.

Hivyo aliwataka watendaji wa mkoa huo kuacha kufanya kazi kwa mazowea badala yake kujidhatiti kufanya kazi kwa bidii, maarifa na weledi ili kuongeza tija katika utoaji wa huduma kwa wananchi.

 

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango