Siku ya uhuru wa habari kuadhimishwa kimkakati Zanzibar

NA ASYA HASSAN

UMOJA wa Taasisi za Waandishi wa Habari Zanzibar, kupitia kamati maalum, unatarajia kuadhimisha siku ya uhuru wa vyombo vya habari kwa kutoa tunzo kwa waandishi watakaoandika habari zitakazotoa matokeo chanya kwa jamii na taifa kwa ujumla.

Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Farouk Karim, alieleza hayo jana katika mkutano na waandishi wa habari, katika ukumbi wa Idara ya Mawasiliano na Taaluma za Habari ya chuo kikuu cha Zanzibar (SUZA), Kilimani wilaya ya Mjini Unguja.

Alisema hatua hiyo itasaidia waandishi kuongezea ujuzi, kujiamini, kujituma na kuongeza ubora katika kazi zao.

Alifahamisha kwamba tunzo hizo ambazo zimeegemea katika maeneo makuu matano ambayo ni uandishi wa habari za uchumi wa buluu iliyopewa jina la ‘Dk. Hussein Mwinyi Award’, Uandishi wa Habari za Jinsia (Mama Mariam Mwinyi Award), Uandishi wa Habari za Serikali ya Umoja wa Kitaifa (Maalim Seif Award), Uandishi wa Habari za Rushwa na uwajibikaji (ZAECA Award) na Uandishi wa Habari za kulipa kodi (ZRB Award).

Alivitaja vigezo vitakavyotumika kupata tunzo hizo  ni pamoja na ubora wa kazi iliyowasilishwa, upekee wa mada, umuhimu wa kuzingatia uwiano usawa wa kijinsia, ubunifu wa mada husika na matokeo baada ya kutoka habari au kipindi hicho.

Mwenyekiti huyo alisema ni vyema waandishi hao kujituma na kuchangamkia fursa hiyo kwani itawasaidia katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku sambamba na fursa ya waandishi wa habari wa Zanzibar kuonesha uwezo wao, weledi na umahiri katika kazi zao.

Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo Dk. Mzuri Issa Ali, alisema wameamua kuweka tunzo hizo ili kuisaidia kukuza vipaji vya waandishi wa habari na kwamba hatua hiyo inalenga kukuza maslahi makubwa kwa nchi kutokana na kazi hizo kuonesha vitu mbali mbali ambavyo vikifanyiwa kazi vitaleta matokeo chanya kwa wananchi na taifa kwa ujumla.

“Kazi hiyo sio rahisi kwani tumejipanga na kuna majaji imara ili mtu aweze kushinda itapitiwa na kuangaliwa vitu mbalimbali, hivyo mtu akishinda atakuwa amefanya kazi na anahitaji kupata tunzo hiyo,” alisema.

Kwa upande wake Katibu wa kamati hiyo Salma Said, alisema malengo ya maadhimisho hayo ni kuongeza hadhi ya uandishi wa habari na thamani ya waandishi wa habari ikiwa ni pamoja na kuandika habari kwa ufanisi, kufatilia, kutafuta na zenye kiwango cha juu.

“Uamuzi huu unatokana na sisi kama viongozi wa taaisisi kukubaliana kuwa habari nyingi zinazoandikwa hazina viwango vizuri kiasi cha kuleta matokei makubwa,” aliongeza Salma.

Siku ya uhuru wa vyombo vya habari kimataifa huadhimishwa Mei 3 ya kila mwaka, lakini kutokana na siku hiyo kuangukia katika mwezi mtukufu wa Ramadhani, taasisi za Zanzibar zitaiadhimisha siku hiyo Mei 23, mwaka huu.

BAADHI ya wawakilishi wa taasisi za kihabari zinazoandaa maadhimisho ya siku ya uhuru wa habari duniani wakiwa katika picha ya pamoja baada ya kumalizika kwa mkutano wa waandishi wa habari jana. kutoka kushoto mstari wa mbele ni Salma Said (WAHAMAZA), Farouk Karim (ITV/RADIO 1), Dk. Mzuri Issa (TAMWA - Z'BAR) . Mstari wa nyuma ni Mwajuma Juma (ZPC), Imane Duwe (SUZA) na Shifaa Said (MCT - Z'BAR).

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango