SIKU YA WANAWAKE DUNIANI
Samia ataka wadau kutathmini mafanikio yaliyofikiwa
- Asema agenda ya usawa wa jinsia inahitaji mashirikiano
- Aipongeza FAWE kuchochea kasi ya maendeleo ya elimu
NA MWANDISHI WETU
MAKAMU
wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amewataka
wadau wa masuala ya jinsia nchini kuitumia siku ya kimataifa ya wanawake
duniani kufanya tathmini na kuweka mikakati ya kusukuma mbele agenda ya
maendeleo ya jinsia badala ya kulalamika.
Ameeleza
kuwa kufanya hivyo kutachochea kasi ya mendeleo ya wanawake duniani kwani siku
hiyo inatoa fursa kwa serikali, taasisi zisizo za serikali na wadau kupima
utekelezaji wa harakati za kumjengea uwezo na kumkomboa Mwanamke na mtoto wa
kike.
Makamu
wa Rais alieleza hayo juzi usiku katika harambee iliyoandaliwa na Jumuiya ya
kuwawezesha wanawake Zanzibar (FAWE) ikiwa ni sehemu ya madhimisho ya siku ya
wanawake duniani inayofikia kilelele chake leo, iliyofanyika hoteli ya Serena
mjini Unguja.
Alisema
ili kuhakikisha mwanamke na mtoto wa kike anakuwa na sauti katika jamii na
taifa kwa ujumla, wadau hawana budi kushirikiana ili kuhakikisha maendeleo yao
katika nyanja za kiuchumi, kisiasa na kijamii yanafikiwa.
“Sote ni mashahidi kuwa karne hii ya 21 ni
karne ya sayansi na teknolojia inayoendeshwa na mapinduzi ya viwanda. Sasa ili
sote tuweze kunufaika na fursa mbali mbali za mapinduzi haya lazima
tushirikiane ili kuhakikisha hakuna kundi linaloachwa nyuma katika safari ya
maendeleo,” alisema Samia.
Aidha
aliipongeza FAWE kwa kuendelea na wajibu wa kumpigania mwanamke kwa miaka 23
tangu kuanzishwa kwake na kuwa chachu ya kuhakikisha kuwa wanawake na watoto wa
kike wa Zanzibar wanapata haki zao za msingi za elimu, uchumi na haki za
kijamii kwa usawa.
Alieleza
kupitia programu mbali mbali, FAWE wamesaidia wanafunzi wa kike zaidi ya 3,000
kutoka kwenye kaya maskini kufikia malengo ya kupata elimu toka mwaka 2001 hadi
sasa.
Samia
aliongeza kuwa kuna umuhimu mkubwa wa wanafunzi wa kike kujikita katika masomo
ya sayansi na teknolojia ili kuzalisha wataalamu wa kike watakaoweza kutumikia
uchumi wa viwanda katika sekta mbali mbali.
Alisema
kwa upande wa Zanzibar, Serikali inajipanga kujikita kwenye masuala ya uchumi
wa bluu unaohusisha sekta za mafuta na gesi, kilimo cha mwani, uvuvi wa bahari
kuu na uvuvi wa vizimba ambazo zitaimarisha kasi ya ujenzi wa viwanda
vitakavyoongeza thamani mazao ya baharini.
“Mtoto
wa kike hadi leo bado anakabiliwa na vikwazo mbali mbali ikiwemo mila potofu,
ndoa za umri mdogo na majukumu ya nyumbani na jambo la kusikitisha kwamba bado
tunaendelea kulalamika tu bila kuchukua hatua tiba za tatizo hilo,” alisema.
Aliongeza
kuwa serikali inaendelea kutoa elimu bure katika ngazi ya maandalizi, msingi
pamoja na kuimarisha mafunzo ya amali na elimu ya juu, sambamba na kuimarisha
hali ya skuli na kurejesha masuala yanayotakikana ili watoto kusoma na kufaulu
masomo ya sayansi.
Aidha
Samia alieleza kwa kipindi cha miaka tisa, bajeti ya sekta ya elimu imeongezeka
kwa asilimia 91.4 kutoka shilingi 93,468,089,000 mwaka 2010/2011 hadi kufikia
shilingi 178,917,149,000 mwaka 2019/2020 jambo linalothibitisha utayari wa
serikali kuwekeza katika elimu.
“Ongezeko
la bajeti limesaidia kuendeleza miundombinu ya elimu na kuboresha mazingira ya
kujifunza na kufundishia, kuweka vituo maalum vya masomo ya sayansi, kuongeza
idadi ya walimu, vitendea kazi ikiwemo vitabu pamoja na kuanzishwa skuli za
watoto wa kike peke yao (skuli ya Benbella),” alisema Makamu wa Rais.
Awali
Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali (WEMA), Simai Mohamed
Said, alisema jumuia hiyo inaendelea kujitolea kuhakikisha mtoto wa kike
anakuwa mstari wa mbele kuleta maendeleo ya taifa.
Alisema
katika kuhakikisha mtoto wa kike anapata taaluma za ujasiriamali kwa lengo la
kuhakikisha taifa linakuwa na vijana wasomi na shupavu katika nyanja zote jumuiya
hiyo mekuwa ikishirikiana na wizara yake kufanikisha ndoto za wanafunzi na
walimu.
Nae
Mwenyekiti wa FAWE Zanzibar, Dk. Mwatima Abdalla Juma, alisema wamekuwa mstari
wa mbele kumuinua na kumuendeleza mtoto wa kike, sambamba kuwahamasisha
ushiriki wa mwanamke katika uchumi kwa njia ya kuelimisha na kuwapatia fursa
mbali mbali za kujiendeleza kiuchumi.
Alisema
kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu Zanzibar, wamefanikiwa kuwarejesha watoto
wa kike masomoni baada ya kukata tamaa ya kuendelea na masomo kutokana na
sababu mbali mbali zikiwemo za kiuchumi.
Akitoa
ushuhuda kwa niaba ya wanafunzi wenzake, mmoja ya wanufaika wa program za
jumuiya hiyo, Amina Omar Kitwana, kutoka kijiji cha Matemwe, mkoa wa kaskazini
unguja, alisema FAWE imewasaidia kurudi masomoni na kujifunza kazi mbali mbali
za ujasiriamali ambazo zimewasaidia kuleta maendeleo kwa familia zao.
Siku ya
kimataifa ya wanawake dunia, huadhimishwa kila ifikapo Machi 8, ya kila mwaka
ambapo katika harambee hiyo, zaidi ya shilingi milioni 32 zilikusanywa kama
fedha taslimu na ahadi.
Comments
Post a Comment