TASAF kujenga wodi ya akina mama, maabara zahanati ya Mkambarani

NA JAMES MWANAMYOTO, MOROGORO

NAIBU Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Deogratius Ndejembi, (pichani) ameiahidi Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa, kwamba kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Jamii Tanzania (TASAF) serikali itajenga wodi ya kuwahudumia akina mama wajawazito na maabara katika zahanati ya kijiji cha Mkambarani ili wananchi hao wapate huduma bora za afya.

Ndejembi ametoa ahadi hiyo ikiwa ni utekelezaji wa maelekezo ya kamati hiyo iliyoelekeza Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) kujenga jengo la kina mama kwa ajili ya kuwapatia huduma stahiki, ikiwa ni pamoja na kujenga maabara itakayotoa huduma bora na vipimo wananchi wa Mkambarani.

Amesema, kutokana na maelekezo yaliyotolewa na kamati ofisi yake itajenga wodi ya akina mama ili kuwe na faragha wakati wa kuwahudumia akina mama wajawazito.

Kuhusu maelekezo ya ujenzi wa maabara, Ndejembi ameihakikishia kamati na wananchi wa kijiji hicho kwamba maabara itakayojengwa itawaondolea adha wananchi hao ya kusafiri umbali mrefu kufuata huduma na kuingia gharama kubwa.

Ameongeza kuwa, lengo la serikali kujenga zahanati ya Mkambarani ni kuwasogezea karibu huduma za afya wananchi wa eneo hilo ikizingatiwa kuwa, walengwa wa TASAF watanufaika pia na huduma zinazotolewa na zahanati hiyo na hatimaye kuwa na afya bora itakayowawezesha kupambana na umaskini kupitia ruzuku ya TASAF wanayoipata.

Akitoa maelekezo kwa serikali kwa niaba ya kamati yake, Mwenyekiti wa Kamati hiyo Humphrey Polepole, amesema Kamati imelazimika kutoa maelekezo ya ujenzi wa Wodi ya akina mama na maabara kama sehemu ya kulinda utu wa wananchi hususani akina mama wanaofuata huduma ya uzazi katika zahanati ya Mkambarani.  

Aidha  Polepole amesema, wodi ya akina mama ikijengwa itaongeza usiri na faragha wakati wa kuwahudumia wajawazito tofauti la ilivyo sasa ambapo hakuna usiri wa kutosha wala faragha pindi akina mama wanapohudumiwa.

Kuhusiana na maelekezo ya ujenzi wa maabara, Polepole ameeleza kuwa, kamati yake imepata fursa ya kuitembelea zahanati ya Mkambarani na kubaini kuwa hakuna maabara inayokidhi mahitaji ndio maana kamati yake imeielekeza Serikali kujenga maabara itakayokidhi kutoa huduma stahiki kwa wananchi wa kijiji cha Mkambarani.

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa imemaliza ziara ya kikazi ya siku tatu mkoani Dar es Salaam, Pwani na Morogoro iliyolenga kukagua utekelezaji wa miradi inayotekelezwa na taasisi zilizo chini ya Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora.

Picha na maelezo yake:

BAADHI ya wananchi wa Kijiji cha Mkambarani, Morogoro wakimsikiliza Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa, Humphrey Polepole (hayupo pichani) wakati wa ziara ya kikazi ya kamati hiyo iliyolenga kukagua utekelezaji wa miradi ya TASAF kijijini hapo.

MMOJA wa wanufaika wa TASAF wa Kijiji cha Mkambarani, Mzee Abdallah Kinyaku, akitoa ushuhuda wa namna alivyonufaika na TASAF kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa wakati wa ziara ya kikazi ya kamati hiyo iliyolenga kukagua utekelezaji wa mpiradi ya TASAF kijijini hapo.


Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango