UNDP kushirikiana na SMZ kuendeleza miradi ya uchumi


NA MWANDISHI WETU, DAR ES SALAAM

WAZIRI wa Nchi Afisi ya Rais Fedha na Mipango, Jamal Kassim Ali (pichani), amefanya mazungumzo na Mwakilishi Mkaazi wa Shirika la  Mpango wa Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP), Christine Musisi na kujadiliana namna shirika hilo litakavyosaidia miradi ya maendeleo ya kukuza uchumi wa Zanzibar.

Mazungumzo hayo yamefanyika jana, katika Ofisi ya Uratibu wa Shughuli za SMZ zilizopo katika ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais, jijini Dar es Salaam. 

Jamal alisema Serikali ya Mapinduzi Zanzibari itaendelea kushirikiana na washirika wa maendeleo wa ndani na nje ikiwemo UNDP, kusaidia uwajibikaji na utendaji kazi wa serikali kwa ufanisi kama alivyoagiza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Zanzibar wa  awamu ya nane Dk. Hussein Ali Mwinyi.

Alisema Zanzibar imejipanga katika kuimarisha uwajibikaji na utendaji kazi kwa wafanyakazi wake ili kuhakikisha nchi inafikia malengo yaliyowekwa wa uchumi wa buluu.

Aliongeza kusema kwamba, shirika hilo litasaidia katika uchumi wa buluu katika kuandaa sera na kujengea uwezo watendaji katika fani mbali mbali ili kufikia azma hiyo ya serikali.

Alifafanua kuwa, UNDP imeweka nguvu zake katika kusaidia Baraza la Wawakilishi la Zanzibar vifaa vya kisasa na kuwajengea uwezo ili liendane na mfumo wa mawasiliano wa sayansi na teknolojia pamoja na kuzijengea uwezo Halmashauri za Zanzibar kivifaa na kiutendaji.

Sambamba na hilo wataendelea kuimarisha mahakama za Zanzibar kwa kuvipatia nyezo za kufanyia kazi kwa ufanisi na kwa haraka zaidi katika kutoa maamuzi.

Jamal alieleza kuwa Dk. Mwinyi, ameruhusu kuanzishwa kwa mahakama maalumu ya udhalilishaji wa watoto na wanawake ili kupambana na kuondosha masuala hayo katika jamii.

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango