Udhibiti wa migogoro utaimarisha amani, utulivu


NA ASYA HASSAN

IMEELEZWA kuwa utashi wa kisiasa na mafunzo ya mara kwa mara juu ya udhibiti wa migogoro utasaidia kuimarisha amani na utulivu nchini.

Meneja wa shirika la Search for Common Ground, Hussein Faraji Sengu, alieleza hayo hivi karibuni katika mahojiano na mwandishi wa habari hizi, ofisiani kwake kijangwani, Zanzibar.

Sengu alieleza kuwa iwapo makundi mbali mbali ya jamii yatajengewa uwezo, kuna uwezekano wa hali ya amani kuimarika na kuepuka mizozo.

Alieleza kuwa ipo mizozo inayoweza kuepukwa kwa wahusika kutambua haki na mipaka yao, hivyo kupitia mradi wa ‘Dumisha amani Zanzibar’, watakutana na makundi mbali mbali wakiwemo wanasiasa ili kuwajengea uwezo wa kutambua vichocheo vinavyoweza kuvuruga amani na utulivu.

“Tunaamini hatua hii itawafanya wanasiasa kujitambua na kuwasimamia vyema wanachama wao ili kuepuka migogoro inayotokezea baina yao kabla ya kuwa chanzo cha vurugu,” alieleza Sengu.

Alisema mfumo wa vyama vingi uliopo nchini, unaweza kuwa chanzo cha migogoro tofauti, hivyo kupitia utekelezaji wa mradi huo utaondosha tofauti zilizopo baina ya watu wenye itikadi tofauti hususani kipindi cha uchaguzi.

“Zanzibar ni nchi ya amani lakini kuna viashiria hutokezea hususani kipindi cha uchaguzi, hivyo kukutana na wanasiasa kutasaidia kupata mwamko na umahiri wa kujiepusha na migogoro inayojitokezea kipindi hicho kwa namna moja au nyengine,” alisema.

Aidha Sengu alisema wadau wa amani wana nafasi kubwa ya kudumisha amani na kuongeza kasi ya maendeleo ya nchi na jamii kwa ujumla.

Hata hivyo alifahamisha kwamba lengo la taasisi hiyo ni kuona wananchi wote wanakuwa wamoja na wanashirikiana katika kulipeleka mbele kudumu la maendeleo ya nchi yao.

Akizungumzia azma ya taasisi hiyo, iliyochangia kuundwa kwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa mwaka 2020, Katibu Mkuu wa chama cha Demokrasia Makini, Ameir Hassan Ameir, alisema kama wanasiasa watashirikishwa katika mipango ya nchi, watasaidia kuwaelewesha wafuasi wao juu ya namna bora ya kulinda na kushiriki katika maendeleo ya nchi yao.

Alieleza kuwa migogoro mingi inayojitokeza huchangiwa na mgawanyo mbaya wa rasilimali lakini pia matumizi mabaya ya madaraka hivyo kuna umuhimu wa jamii kujengewa uwezo kutambua misingi ya mgawanyo wa rasilimali.

“Kinapofika kipindi cha uchaguzi, kila chama lengo lake ni kupata uungwaji mkono ili kishike madaraka hivyo kuna haja kubwa ya sisi wanasiasa kujenga uelewa wa wanachama wetu, kuepuka mizozo ya kisiasa,” alieleza Ameir.

Kwa upande wake Msaidizi wa Sheria kutoka Jumuiya ya Wasaidizi wa Sheria Zanzibar (ZAPAO), Fatma Khamis Ali, alieleza kuwa mbali ya wanasiasa, mradi huo unapaswa kuwashirikisha Wasaidizi wa Sheria kwani wamekuwa wakifanya kazi kubwa ya kutatua migogoro katika jamii.

“Katika kazi zetu, tunakutana na aina mbali mbali za mizozo ambayo mengine chanzo chake ni ukosefu wa uelewa juu ya mambo ya utawala na uongozi sio kwa wanachama au wananchi tu hata kwa viongozi,” alisema Fatma.

Hivyo alisema ipo haja ya kutolewa kwa elimu ya uraia kwa wananchi wazijue haki zao ili wapate kutekeleza wajibu wao kulingana kwa lengo la kuimarisha amani na uwepo wa serikali ya umoja wa kitaifa.

Mradi wa ‘Dumisha amani Zanzibar’, unatarajiwa kutatua migogoro kwa kuwashirikisha wadau wakiwemo wanasiasa, asasi za kijamii na viongozi wa dini kuzuia vichocheo vya migogoro sambamba na kuwa na jamii yenye mwamko wa kuzuia na kutatua migogoro kabla ya kuleta madhara ili kudumisha amani .

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango