Ushirikiano wa vioingozi, wananchi kuimarisha maridhiano

NA MWANDISHI WETU

WANANCHI wa mkoa wa Kaskazini Unguja, wameeleza kuwa ushirikiano uliopo kati ya viongozi wakuu wa serikali ya Mapinduzi Zanzibar umeimarisha maelewano baina ya wananchi hivyo ipo haja ya kuendelezwa.

Wakizungumza na mwandishi nwa habari hizi hivi karibuni, walieleza kuwa hali hiyo inatokana na kuundwa kwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK) inayohusisha vyama vya CCM na ACT Wazalendo baada ya uchaguzi mkuu wa oktoba 28 mwaka uliopita.

Mkaazi wa shehia ya Bumbwini Mafufuni, Haji Nyange Makame, alieleza kuwa hali hiyo imeongeza kuaminiana miongoni mwa viongozi na wananchi katika shehia yao.

“Kabla ya uchaguzi, ilikuwa vigumu kumuona viongozi wa CCM na vyama vyengine wakakaa pamoja katika kazi za kisiasa au kijamii lakini siku hizi huwezi kumjua nani CCM nani ACT kama mgeni nao,” alieleza Nyange.

Nae Mwanaacha Hamid Said wa Kilimani Tazari, alieleza kuwa hali ya ushirikianbo imeongezeka na kupongeza utamaduni ulioanzishwa na viongozi wa serikali kukutana na wananchi kila siku za Ijumaa.

“Tunawaona Makamu wa wa Kwanza, Makamu wa Pili na Rais Mwinyi (Dk. Hussein Ali Mwnyi) kila Ijumaa wanakutana na wananchi na kutoa ujumbe wa maridhiano, umoja na amani. Hili ni jambo linalowanyima nguvu watu wasiopenda umoja wa Wazanzibari waishi kwa amani,” alieleza mama huyo.

Wananchi hao na wengine, waliwaomba viongozi wa ngazi za chini kufuata mwenendo wa viongozi hao ili kupata nafasi ya kukutana na kutatua changamoto zinazowakabili wananchi katika maeneo yao.

Hivi karibuni akiwa katika ziara mkoani humo, Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Othman Masoud Othman, alipotembelea wagonjwa na kuzungumza na wananchi wakiwemo wanachama wa chama cha ACT Wazalendo alisisitiza haja ya wazanzibari kuendeleza hali ya amani na utulivu iliyopo.

Ziara hiyo iliyoandaliwa na chama hicho, ni sehemu ya utamaduni uliokuwa ukitekelezwa na aliyekuwa Mwenyekiti wa chama hicho, marehemu Maalim Seif Sharif Hamad.

Akizungumza na wananchi hao kwa wakati maeneo tofauti, Othman alieleza kuwa Zanzibar inahitaji kuendelea na umoja ili kuharakisha maendeleo kwa wananchi wake

Alisema hakuna njia nyengine itakayoleta maendeleo bila kuwepo mashirikiano, upendo na umoja miongoni mwa Wazanzibari.

“Nimeweka ahadi ya kuwatumikia Wazanzibar wakati wowote ili kuendeleza yale  yaliyoanzishwa na kuleta tija katika muendelezo wa kuyaimarisha zaidi maridhiano ya kisiasa ya Zanzibar,” alisema Othaman.

Alisema anayo imani kwamba   anaweza kuwatumikia watu wote nchini bila ubaguzi na kufanya kazi kwa moyo ili kuona malengo ya umoja wa kitaifa yanafikiwa. 

“Umoja na upendo ndio silaha pekee itakayodumisha amani katika taifa letu, inapendeza zaidi kuona watu wakitembeleana na kusaidina kwa wale wanaohitaji msaada,” alieleza Makamu wa Rais.

Sambamba na hilo aliwashauri wananchi wa Zanzibar kurudisha utamaduni wa kufutari pamoja kama ilivyokuwa zamzni katika hasa mwezi mtukufu wa Ramadhani, kwani kufanya hivyo kunaongeza mapenzi baina ya aliyenacho na asienacho.

“Kuna watu wengi wanaofunga lakini huwa hawana futari, kama tukiurudisha utamaduni kuftari pamoja ndugu na majirani utaendelea basi utaleta faida kubwa miongoni mwa jamii,” alieleza Othman. 

Katika  ziara yake, Othman alifika kuwafariji wagonjwa katika vijiji vya Chaani, Matemwe , Nungwi,  Kendwa,  Kilimani Tazari, Mahonda, Bumbwini Mafufuni na Kiomba Mvua vya mkoa wa Kaskazini Unguja.

Pichani: MAKAMU wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Othman Masoud Othman (kulia), akizungumza na mzee Mussa Hassan Hassan ambae ni mgonjwa wa muda mrefu alipofika nyumbani kwa mzee huyo kumjulia hali. (PICHA NA OMKR).

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango