Wazazi wasiozingatia elimu za watoto wao kukiona


NA MWANDISHI WETU

MKUU wa Mkoa wa Kusini Unguja, Rashid Hadidi Rashid, (pichani) amewaagiza masheha wa mkoa huo, kuzidisha mashirikiano na kutoa taarifa za wazazi wasioshughulikia maendeleo ya elimu ya watoto wao.

Alieleza kuwa hatua hiyo itasaidia kuimarisha kiwango cha ufaulu mkoani humo ambacho kwa muda mrefu kipo chini.

Hadidi alitoa agizo hilo skuli ya Ukongoroni wakati akizungumza na wazazi, walezi, walimu na wanafunzi wa skuli hiyo.

Alisema imebainika kuwa baadhi ya wazazi wanapuuza upatikanaji wa elimu kwa watoto wao kwa kushirikisha na masuala ya ukataji kuni, kujiingiza katika ajira za watoto ikiwemo za kupara samaki na kupelekea watoto hao kushindwa kuhudhuria skuli kwa wakati, kuwa watoro na kutodurusu masomo yao.

Alifahamisha kuwa kutokana na hali hiyo inayofanywa na baadhi ya wazazi kunachangia kwa kiasi kikubwa kurudisha nyuma juhudi za serikali juu ya mikakati iliyojiwekea.

Hivyo aliwataka masheha hao kuwafichua wazazi hao wanaopuuza juhudi hizo ili kuweza kuleta matokeo mazuri kwa watoto hao sambamba na kuwa na viongozi waliokuwa imara baadae.

Aidha aliwasisitiza wazazi hao kuthamini juhudi zinazochukuliwa na serikali katika kuimarisha sekta ya elimu na  kuwasisitiza walimu wa mkoa huo kuongeza bidii ya ufundishaji.

“Acheni tabia ya kuzitumia changamoto zinazowakabili kama ni kigezo cha kushindwa kufaulisha na kupata matokeo mazuri ya wanafunzi wa mkoa wetu,” alisema Hadid.

Nao wazazi na walimu wa skuli ya Ukongoroni, walisema miongoni mwa sababu  zinazochangia kwa kutofanya vizuri mitihani yao ya taifa hasa kwa wanafunzi wa kidato cha nne ni kuwepo kwa mazingara ya imani za kishirikina.

Walisema kutokuwepo kwa mfumo na sera ya elimu inayoeleweka pamoja na matumizi mabaya ya simu za mikononi na utandawazi unachangia kukosekana kwa matokeo chanya.

Akizungumza katika kikao hicho, Katibu Tawala Mkoa wa Kusini Unguja, Salum Kassim Ali, alisema serikali ya mkoa huo imejipanga kuwapa zawadia walimu watakaofaulisha wanafunzi kwa kiwango cha juu katika mitihani kwa daraja la kwanza katika masomo yao.

Alieleza kuwa wanafunzi watakaopata alama ‘A’ hasa kwenye masomo ya sayansi, watapatiwa zawadi ya fedha taslimu shilingi laki tano kila mmoja kama motisha ya kuwafanya waongeze bidii katika masomo yao.

 

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango