DC Kati awataka walimu kumaliza mitaala kuongeza ufaulu

NA MWANDISHI WETU

MKUU wa Wilaya ya Kati Unguja, Marina Joel Thomas, amewataka walimu wa skuli za sekondari Wilayani humo kuhakikisha wanamaliza mitaala kwa wakati ili wanafunzi wapate muda wa ziada wa kupitia masomo yao.

Marina alisema hayo katika hafla ya utoaji wa zawadi kwa walimu walioleta ufaulu mzuri kwa wanafunzi wa kidato cha pili mwaka 2020 iliyofanyika katika ukumbi wa Kituo cha walimu (TC), Dunga, wilaya ya Kati, mkoa wa Kusini Unguja.

Alisema hatua hiyo itasaidia kuongeza fursa kwa wanafunzi kufanya vizuri katika mitihani yao ya taifa.

“Kumaliza silabasi mapema kutawasaidia wanafunzi kupata muda mzuri wa kuyapitia masomo yao na kuongeza ufaulu katika mitihani yao ya taifa,” alisema Marina.

Mbali na hayo Marina alifahamisha kwamba serikali ya wilaya hiyo imekuwa ikifanya jitihada kuona kiwango cha ufaulu kwa wanafunzi kinaongezeka ili kupata wataalamu wa ndani waliobobea katika fani mbali mbali.  

Aidha aliwasisitiza walimu hao kuendelea kuwa na nidhamu ya kazi sambamba na kuwajibika ipasavyo na  kuwasimamia wanafunzi ili wahudhurie vipindi kikamilifu.

Akizungumzia suala la utoro kwa wanafunzi Mkuu huyo wa wilaya, aliwataka walimu na wazazi kushirikiana kufuatilia myenendo ya watoto wao ili kuleta ufanisi katika eneo hilo.

Kwa upande wake Afisa elimu Mkoa Kusini Unguja, Mohamed Haji Ramadhan, aliwashauri masheha na kamati za skuli kufatilia mwenendo na mahudhurio ya walimu ili kulimarisha maendeleo ya skuli zao.

Nao walimu waliopatiwa zawadi hizo waliwashauri walimu wenzao kutenga muda wa ziada kuwasaidia wanafunzi ili waweza kupata matokeo mazuri na kuleta mabadiliko katika maendeleo ya elimu skulini mwao.

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango