Dk. Mwinyi asema Tanzania inataka dunia yenye amani

NA RAJAB MKASABA, IKULU

JAMHURI ya Muungano wa  Tanzania, ikiwemo Zanzibar,  zinashirikiana na mataifa mbali mbali katika kudumisha amani, kutafuta suluhu ya migogoro, kuimarisha usalama na maendeleo.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi alieleza hayo katika hotuba yake wakati alipoungana na viongozi kadhaa duniani kwa njia ya mtandao kujadili njia za kuimarisha umoja na mshikamano ambapo mada kuu ilikuwa ni “Kuimarisha umoja na kudumisha amani katika rasi ya Korea.

Mjadala huo ambao umefanyika kwa njia ya mtandao kutokana na uwepo wa maradhi ya corona, ambapo Dk. Mwinyi aliimpongeza Dk. Hak Jan Han mwanzilishi wa taasisi ya “Universal Peace Federeration” kwa kumpa fursa ya kuungana na viongozi wengine katika mjadala huo.

Katika mjadala huo ambapo miongoni mwa mambo yaliyozungumzwa ni kuwataka  viongozi wa dunia  siyo tu  kuzungumiza matatizo ya kuzuka kwa maradhi ya COVID 19, bali pia, kuwa na fikra mpya za kuondokana na matatizo yaliyopo na badala yake kuwa wamoja katika hali ya usalama na amani duniani.

Dk. Mwinyi alisema kuwa ingawa  kijiografia  rasi ya Korea iko mbali na Afrika, lakini ikumbukwe kwamba licha ya umbali huo, Afrika inashiriki kikamilifu katika kurejesha amani katika eneo hilo.

Alisema kwa bahati  mbaya, licha ya juhudi zilizochukuliwa na Jumuiya za Kimataifa, eneo hilo bado  limebaki na mivutano ambayo  inatishia usalama  katika eneo la Kusini  Mashariki ya Bara la Asia.

“Hatuwezi kuendelea kubaki tunautizama tu mgogoro huo, ambapo baadhi ya wakati unajulikana kuwa ni ‘mgogoro uliosahauliwa, kuendelea kwa mgogoro huo ni kuleta athari nyingi kwa amani na usalama wa dunia”, alisema.

Alitoa pongezi kwa Dk. Han Ja Han, kwa kukusanya timu ya wataalamu kutoka pande mbali mbali za dunia ili waje na rai mpya  zenye lengo la kurejesha  hali ya amani na usalama  ili kuwa na Korea  iliyoungana.

Akizungumzia hali ya  kisiasa  ya  Zanzibar  na historia yake, Dk. Mwinyi alimpongeza marehemu Seif Sharif Hamad, kwa kukubali kuungana naye katika kuunda serikali ya Umoja wa Kitaifa baada ya uchaguzi mkuu.

Alieleza alivyofarajika kwa uamuzi huo wa kuunda Serikali ya Umoja wa Kitaifa ambapo ni miongoni mwa  mafanikio aliyoyapata ndani ya kipindi kifupi cha miaka mitano atakachokuwepo madarakani.

Dk. Mwinyi alisema kuwa lengo lake ni kuona kuwa  kuna Zanzibar ambayo watu wake  ni wamoja na  inapiga  hatua za haraka za maendeleo.

Alisisitiza kwamba Zanzibar imedhamiria kutumia vizuri rasilimali zake na fursa iliyopo kijiografia ya kuwepo eneo la kimikakati  na muhimu katika kuendeleza sekta mbali mbali za kiuchumi.

Alifahamisha kuwa serikali  anayoiongoza imejidhatiti kuimarisha na kukuza fursa za uwekezaji  na kutoa upendeleo maalumu kwa wawekezaji wanaowekeza kisiwa cha Pemba ili kukuza maendeleo katika  kisiwa hicho.

Aidha, alisema kuwa Zanzibar ina fursa na rasilimali nyingi za kuendeleza uchumi imara utakaoweza  kukuza ajira, kupunguza umasikini na  hatimae  kupata maendeleo ya haraka.

Aliongeza kuwa Zanzibar imedhamiria kuendeleza uchumi wa buluu kwa kushirikiana na  nchi  wanachama  wa jumuiya ya nchi zinazopakana na bahari ya Hindi (IORA) ambazo nazo kwa upande wao zimepanga kuendeleza uchumi  huo.

Dk. Mwinyi alieleza kwamba serikali itahakikisha katika utekelezaji wa mipango ya maendeleo inashirikiana na washirika wa maendeleo ili kufikia malengo yake ya kukuza ajira, kuimarisha sekta ya elimu, afya, na miundombinu  kwa kuzingatia  Dira ya Maendeleo ya Zanzibar ya Mwaka 2050.

Dk. Mwinyi alimuunga mkono Dk. Hak Jan Han, pamoja na wanachama na marafiki wote wa taasisi ya “Universal Peace Federation” na Jumuiya zake katika kuimarisha amani na kuharakisha maendeleo.

 

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango