Dk. Mwinyi ahimiza waumini kufanya hijja mapema

NA MWANDISHI WETU

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Mwinyi, amewataka waumini wa dini ya kiislamu kujipanga na kufanya ibada ya Hijja mapema badala ya kusubiri hadi baada ya kustaafu.

Aidha aliieleza kuwa serikali inaendelea na mikakati ya kuanzisha mfuko wa Hijja ili kuwafanya waumini wengi kutekeleza ibada hiyo ambayo ni nguzo ya tano ya Uislamu.

Dk. Mwinyi, aliyasema hayo jana alipokuwa akihutubia katika baraza la Eid el Fitri katika ukumbi wa Sheikh Idrissa Abdulwakil, Kikwajuni Mjini Unguja, baada ya waumini wa dini ya kiislamu kumaliza mfungo wa mwezi mtukufu wa Ramadhani.

Alisema Mahujaji wa Zanzibar wanapaswa kujiandaa mapema kuteleza ibada hiyo, badala ya kusubiri hadi mtu anapostaafu na ameitaka Kamisheni ya wakfu na Mali ya Amana, kukamilisha mapendekezo yaliotolewa ili kufanikisha mfuko wa Hijja Zanzibar.

Alisema ili kutekelelza vyema ibada hiyo na kuuendeleza mbele uislamu serikali imeamua kuanzisha mfuko huo utaowasaidia waislamu kufanya ibada hiyo kwa wakati mzuri na sio kusubiri wanapostaafu ndipo waende hijja.

Hata hivyo, alisema katika mwaka 2020, waislamu walishindwa kufanikisha ibada ya Hijja ya kwenda Makka nchini Saudi Arabia kutokana na zuio la ugonjwa wa Covid -19.

“Serikali inafuatilia kwa karibu jambo hili na inakusudia kuweka mazingatio maalum kwa mahujaji walioweka nia ya kutekeleza ibada hiyo mwaka huu, ili kuwawezesha kufanikisha jambo hilo na kukidhi masharti yatakayowekwa,” alieleza Dk. Mwinyi.

Sambamba na hayo alieleza kuwa hivi karibuni serikali itatoa taarifa za ziada ili kukidhi masharti yatakayowekwa na kuwaahidi mahujaji wa Zanzibar, kukaa tayari kwani serikali inafanya mawasiliano na serikali ya Saudi Arabia ili kuona vigezo vinavyovitakiwa kwa mahujaji vinafuatwa.

Akiendelea Rais Mwinyi, aliwataka viongozi na vyombo vya sheria nchini, kuingiwa na hofu ya Mungu kwa kuhakikisha wanatenda mambo mema katika uwajibikaji wao ili kuwasaidia wanyonge kupata haki zao.

“Uadilifu tukiuendeleza, utaimarisha utoaji wa haki, utaweka usawa katika kupata huduma na ni msingi muhimu wa sheria na utawala bora,” alisema.

 “Kwa hivyo, ili jamii yetu iondokane na vitendo mbalimbali vinavyowanyima haki miongoni mwetu na hasa wananchi wanyonge, viongozi sote, watumishi wa umma na watendaji katika vyombo vya sheria tuna wajibu wa kutekeleza majukumu yetu kwa uadilifu,” alisema Dk. Mwinyi.

Alisema katika kipindi cha mwezi mtukufu wa Ramadhani, wananchi wengi walionekana kubadili tabia kwa kuishi kufuata misingi ya uadilifu, jambo ambalo linahitaji kuendelezwa ili nchi iendelee kubaki ikiwa katika umoja, amani na utulivu.

Alisema huruma iliyooneshwa na wananchi wenye nacho kuwapa watu wanyonge, inahitaji kuendelezwa, kwani bado Zanzibar inakabiliwa na makundi ya wazee, wajane, yatima   wasiojiweza, walemavu, watoto waliotelekezwa, mafukara, na makundi mengine yanayohitaji misaada kutoka kwa wenye uwezo ili nao washerehekee sikukuu wakiwa na furaha.

Alisema inafurahisha kuona vijana wengi ndani ya mwezi huu, wameonyesha uwezo wao wa kusoma quraani katika mashindano mbali mbali yaliofanyika hapa nchini, jambo ambalo linahitaji kuendelezwa ili kuwafanya vijana wa Zanzibar kuwa wenye maadili mema.

Mapema akitoa hotuba ya baraza hilo, Juma Ngwali Juma, alisema suala la umoja ni jambo linalosisitizwa katika uislamu na vyema waumini wa dini hiyo wakaona umuhimu wa kuendeleza yale yote waliyojifunza katika mwezi wa Ramadhani.

Akimkaribisha Dk. Mwinyi, Waziri wa Nchi, ofisi ya Rais, Katiba, Sheria, Utumishi wa Umma na Utawala bora, Mwalimu Haroun Ali Suleiman, alieleza kuwa wananchi wa Zanzibar wameonesha utiifu wa hali ya juu wakati wa mwezi mtukufu wa ramadhani hali iliyopelekea kuimarika kwa hali ya amani na utulivu nchini.

Aidha alisema wananchi wengi walivutiwa na utaratibu alioufanya dk. Mwinyi wa kushirikia nnao katika matukio mbali mbali ya kiibada jambo ambalo linastawisha imani na mshikamano miongoni mwao.

“hali hii imaeongeza imani ya wananchi kwako (Dk. Mwinyi), kwani mbsali ya kuwafutarisha wananchi wa mikoa mitano ya Zanzibar kama ilivyokuwa kwa watangulizi wako, ulishiriki nao katika sala za tarawehe kwenye ,misikiti mbali mbali jambo lililowafanya waendelee kukuamini na kukuombea dua,” alieleza mwaliu Haroun.

Baraza hilo lilihudhuriwa pia na viongozi mbali mbali wa serikali zote mbili za Tanzania waliopo madarakani na waliostaafu, watendaji wa ngazi mbali mbali na mume wa rais wa jamhuri ya muungano nwa Tanzania, Maalim Hafidh Ameir.

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango