Hemed Mgeni Rasmi maadhimisho uhuru wa habari Z’bar

NA MWANDISHI WETU

MAKAMU wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Hemed Suleiman Abdullah, anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika maadhimisho ya siku ya uhuru wa habari kitaifa yatakayofanyika mwishoni mwa wiki hii katika ukumbi wa Sheikh Idriss Abdulwakil, Zanzibar.

Akizungumza katika mkutano wa waandishi wa habari, Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya maadhimisho hayo, Dk. Mzuri Issa Ali, (wa pili kulia) alieleza kuwa maadhimisho hayo yatafanyika Jumapili Mei 30, 2021 na zaidi ya watu 250 wakiwemo waandishi wa habari, wadau wa habari na wawakilishi wa taasisi za umma na asasi za kiraia wanatarajiwa kuhudhuria.

Alieleza kuwa maadhimisho hayo yataambatana na uwasilishaji wa mapendekezo ya mswada ya sheria mpya ya habari Zanzibar ulioandaliwa na wadau wakiwemo waandishi wa vyombo mbali mbali vya binafsi, serikali na mashirika ya habari.

“Mswaada huo ambao umebeba miongozo na maazimio ya habari kikanda, kimataifa na kuzingatia mazingira ya Zanzibar, umekamilika na unategemewa kukabidhiwa rasmi kwa Mhe. Makamu wa Pili akiwa ndiye Mtendaji Mkuu wa shughuli za Serikali nchini,” alieleza Dk. Mzuri.

Aliongeza kuwa mswada huo unapendekeza kufuta sheria namba 5 ya Magazeti ya mwaka 1988 na vifungu vya sheria nyengine vinavyooana navyo ambavyo vimepitwa na wakati na pia haviweki mazingira mazuri kwa sekta ya habari na wanahabari kufanya kazi vizuri.

Alisema shughuli nyengine ni utoaji wa tuzo za uandishi wa umahiri na weledi kwa waandishi wa habari ambao waliwasilisha kazi zao katika kamati ya maandalizi ya maadhimisho hayo.

Alizitaja tuzo zitakazokabidhiwa kuwa ni ya tuzo ya uandiahi wa habari za uchumi wa buluu iliyopewa jina la tuzo ya Dk. Mwinyi, tuzo ya uandishi wa habari za serikali ya umoja wa kitaifa, inayoitwa tuzo ya Maalim Seif na tuzo ya habari za jinsia ijulikanayo kama tuzo ya Mama Maryam Mwinyi.

Aidha Dk. Mzuri, alizitaja tuzo nyengine kuwa ni tuzo ya habari za rushwa na uhujumu uchumi (tuzo ya ZAECA) ambayo itatolewa pia kwa  kwa mshindi wa pili na wa tatu na tuzo ya habari za Kodi (tuzo ya ZRB) ambapo jumla ya kazi 52 zimewasilishwa.

alieleza kuwa kazi hizo zitatangazwa na kuoneshwa ili iwe kujenga uelewa na hamasa kwa waandishi wa habari kufanya kazi nyingi zitakazowasilishwa katika maadhimisho ya mwaka unaofuata kwa vile tuzo hizi zinatarajiwa kuwa endelevu.

Pia Mzuri alizishukuru taasisi na wadau mbali mbali waliojitokeza kuunga mkono maandalizi ya maadhimisho hayo na kuwaomba wadau wengine kujitokeza kushirikiana na taasisi zinazoandaa maadhimisho hayo.

Alizitaja taasisi zinazoshirikiana kuandaa maadhimisho hayo kuwa ni pampoja na Baraza la Habari Tanzania (MCT) Ofisi ya Zanzibar, Jumuiya ya Waandishi wa Habari za Maendeleo (WAHAMAZA), Klabu ya Waandishi wa Habari Zanzibar (ZPC), Klabu ya Waandishi wa Habari Pemba (PPC), Idara ya Mawasiliano na Mafunzo ya habari ya Chuo Kikuu cha taifa Zanzibar (SUZA) na Chama cha waandshi wa habari Tanzania (TAMWA) ofisi ya Zanzibar

Maadhimisho ya siku ya Uhuru wa Habari Kimataifa huadhimishwa Mei 3 ya kila mwaka lakini Zanzibar taaisisi zinazoratibu na kuandaa maadhimisho hayo ziliakhirisha ili kupisha mwezi mtukufu wa Ramadhani.

KATIBU wa Kamati ya maandalizi ya maadhimisho ya siku ya uhuru wa habari, Imane Duwe (kulia), akifafanua jambo katika mkutano wa wandishi wa habari kuhusu maadhimisho hayo yanayotarajiwa kufanyika Jumapili Mei 30, 2021.

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango