Sadaka zinaimarisha amani, upendo kwenye jamii – Sheikh Kahalid

NA MWANDISHI WETU

OFISI ya Mufti wa Zanzibar imeeleza kuridhishwa kwake na sadaka zinazotolewa kwa watu wenye mahitaji maalum na watoto yatima, kwani inasaidia kuimarisha amani, upendo na kupunguza ukali wa maisha miongoni mwa jamii.

Katibu wa ofisi hiyo Sheikh Khalid Ali Mfaume, alitoa kauli hiyo alipokuwa akizungumza wakati wa zoezi la ugawaji wa vyakula vya futari iliyotolewa na taasisi ya Shura Muslim Charitable Organization katika ofisi za jumuiya hiyo, Kilimahewa, mjini Zanzibar.

Alisema Mweyezi Mungu aliyataja makundi ya mayatima, wajane na watu wasiojiweza kuwa miongoni mwa yanaopaswa kusaidiwa hivyo jumuiya hiyo imefanya jambo jema linalopaswa kuigwa na kila mwenye uwezo.

“Tumehimizwa na Allah (S.W) kuwashika mkono mayatima, masikini na wale wenye mahitaji maalum kwani kufanya hivyo sio kunawapunguzia ugumu wa maisha tu, bali huongeza upendo na kujenga amani katika jamii,” alisema Sheikh Mfaume.

Alisema jamii isiyokuwa na usawa, watu wake wanakosa utulivu wa nafsi na kuwa sababu ya kuoneana choyo na husda hivyo ipo haja kwa kila mmoja kujenga utamaduni wa kutoa sadaka kwa kadri ya uwezo alionao.

Aidha aliwashukuru wafadhili ya jumuiya hiyo, Umoja wa Nchi za Falme za Kiarabu (UAE) kwa kufadhili futari na shughuli za jumuiya hiyo ambayo imekuwa ikitoa misaada mbali mbali ikiwemo ya elimu kwa watoto mayatima.

Awali akizungumza katika zoezi hilo, Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo, Juma Ali Khamis, alieleza kuwa jumla ya msaada huo ni mwendelezo wa misaada inayotolewa na jumuiya yake kwa familia zinazolea watoto yatima, wazee na watu wanaoishi kwenye mazingira magumu.

Aliongeza kuwa kabla ya kutoa msaada wa futari kwa wananchi wa Unguja, walifanya hivyo katika maeneo mbali mbali ya kisiwa cha Pemba pamoja na kufutarisha katika maeneo ya Unguja ambapo zaidi ya watu 4,000 wamenufaika.

“Toka jumuiya yetu ilipoanzishwa mwaka 2014 tumekuwa na harakati zinazoyahusu makundi haya na kwa mwaka huu Alhamdulillah tulianza kwa kutoa sadaka ya vyakula vikavu kule Pemba na sasa tupo hapa Unguja,” alieleza maalim Juma.

Aliyataja maeneo yaliyofikiwa na idadi ya watu waliofikiwa kwenye mabano ni Msuka (200), Wingwi (300, Pandani (165), Shengejuu (700), Mvimbe Pandani (65) kwa upande wa kisiwa cha Pemba ambapo katika kisiwa cha Unguja familia 150 zimefikiwa.

Nae mmoja ya wanufaika wa sadaka hiyo anaetunza watoto saba mayatima wakiwemo wanawake wanne, aliwashukuru wafadhili waliofanikisha kupatikana kwa sadaka hiyo na viongozi wa jumuiya ya Shura kwa kuwapatia msaada huo ambao alisema utawasaidia kupunguza ugumu wa maisha.

“Tunashukuru vyakula hivi vitatusaidia kupata utulivu katika maswala ya chakula katika kipindi hiki cha ramadhani na kile kipato kdogo tulichonacho tutakitumia kwenye maswala ya mavazi ingawa bado tunaomba tusaidiwe na huko,” alieleza mama huyo ambaye hakutaka kutajwa jina gazetini.

Katika hafla hiyo zaidi ya familia 150 zinazoishi na watoto yatima, wazee wasiojiweza na wanaoishi kwenye mazingira magumu walipatiwa futari hiyo iliyojumuisha mchele, maharage, mafuta ya kula, sukari, unga wa ngano na tende.

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango