Tuwafunzwe watoto wetu kuyapenda, kuyatunza mazingira - DC Msaraka

NA SALUM VUAI

MKUU wa Wilaya ya Mjini, Rashid Simai Msaraka, jana alizindua wiki ya maadhimisho ya siku ya mazingira duniani, huku akiihimiza jamii kuwajengea watoto mapenzi na muamko wa kupanda na kutunza miti.

Maadhimisho ya siku hiyo yanayofikia kilele chake tarehe 5 Juni, yanafanyika kwa harakati mbalimbali zinazohusisha uhifadhi wa mazingira ya nchi kavu na baharini.

Katika uzinduzi huo uliofanyika kwenye bustani ya Botanic iliyopo Migombani Wilaya ya Mjini, Msaraka aliongoza wananchi mbalimbali na wadau wa mazingira, katika shughuli ya kupanda miti kwa lengo la kulistawisha eneo hilo.

Akizungumza na wananchi wakiwemo wanafunzi wa skuli ya msingi Migombani, Mkuu huyo wa Wilaya alisema ni muhimu wazazi na walezi kuwarithisha watoto utamaduni wa kuyapenda mazingira kwa kujumuika nao katika upandaji miti mbalimbali ikiwemo ya matunda na kivuli.

Alisema miti ni rasilimali inayopaswa kuendelezwa kutokana na faida zake kwa jamii ambazo zinabaki kuwanufaisha watu na viumbe vyengine hata pale wanapoipanda na kuistawisha wanapokuwa wametangulia mbele ya haki.

Alisema kupanda miti na kuhifadhi mazingira ni sehemu ya ibada ambayo mtu akifanya anapata fungu kwa Mwenyezi Mungu, akitoa mfano wa kiongozi wa Waislamu Mtume Muhammad (S.A.W) ambaye wakati kukiwa na vita aliwasisitiza wafuasi wake wasikate miti ovyo au kuharibu mimea.

Alifahamisha kuwa, jamii inapowekeza kwa kuwarithisha watoto mambo yenye manufaa, ni kutafuta rehema za Muumba kwani hata miti iliyopo sasa imepandwa na watu wa kale ambao wameshafariki, lakini wanaofaidi ni kizazi cha sasa na wao wanapata thawabu.

Aliwapongeza vijana wa Shehia ya Migombani kwa hatua ya kujikusanya na kuunda jumuiya yenye lengo la kulibadilisha eneo la bustani ya Botanic, kutoka lilivyokuwa makao na maficho ya wahalifu na watumiaji dawa za kulevya, na kuligeuza kuwa eneo la kiuchumi na kupumzikia.

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango