Wizara ya habari kuwaendeleza watendaji wake

  •  Yapongeza utendaji wa vyombo vya habari

MWANDISHI WETU

WIZARA ya Habari, Vijana, Utamaduni, Sanaa na Michezo, imeeleza kuwa mwaka wa fedha 2021/2022, itaimarisha mazingira ya utendaji kazi kwa wafanyakazi wake ikiwemo utoaji wa vitendea kazi na stahiki zao kwa mujibu wa sheria.

Kauli hiyo imetolewa na Waziri wa wizara hiyo, Tabia Maulid Mwita (pichani), wakati akiwasilisha hotuba ya makadirio ya mapato na matumizi katika Baraza la Wawakilishi Chukwani, Juni 2, 2021.

Alisema mpango huo utaenda sambamba na kuwaendeleza wafanyakazi hao kwa kuwapatia mafunzo ili kutekeleza majukumu yao ya kila siku kwa lengo la kuongeza ufanisi na bidii ya kazi.

Aidha alisema wizara katika mwaka huo pia imejipangia maeneo muhimu ya utekelezaji, ikiwemo kuimarisha miundombinu ya habari kwa ajili ya uzalishaji wa vipindi, ununuzi wa maudhui, ufatiliaji wa habari, ununuz wa mitambo ya uchapaji.

Waziri Tabia alieleza kuwa kipaumbele chengine ilichojiwekea ni kuimarisha huduma za maendeleo ya vijana kwa kuanzisha mfuko wa mikopo kwa vijana na kuanzisha vituo vya vijana.

“Wizara pia imejipanga kuimarisha huduma za utamaduni kwa kujenga chuo cha utamaduni na kuanda mpango wa kuendeleza lugha ya Kiswahli na kufuatilia fursa ziliopo za mahitaji ya Kiswahili ndani na nje ya nchi,” aliongeza Tabia.

Tabia alieleza kuwa lengo  la kufanya hivyo ni kuongeza ajira na kukuza, kuhifadhi na kuendeleza utamaduni, sambamba na ubunifu kwa jamii ya Zanzibar ili haki na maslahi ya wasanii na wabunifu zipatikane.

Sambamba na hiyo alisema wataimarisha miundmbinu ya michezo pamoja na kuviwezesha vyama vya michezo kuendesha shughuli zao kwa mujibu wa sera, sheria ya baraza na mashirikisho ya kimataifa, kikanda na kitaifa na kuzisaidia timu za taifa na za watu wenye ulemavu.

Kuhusu programu ndogo ya usimamizi wa vyombo vya habari, utangazaji na uchapaji alisema wizara imetenga jumla ya shilingi 11,047,960,000 kwa lengo la kutoa matokeo ya muda mrefu na kuleta usimamizi bora wa vyombo vya habari na upatikanaji wa habari zenye maadili.

Aidha alisema wizara yake imepanga kuwajengea uwezo wafanyakazi wa mashirika na kampuni yaliyomo ndani ya wizara hiyo ili kuendana na kasi ya teknolojia inayokuwa kwa haraka duniani na kuleta ufanisi katika kazi zao.

Mbali na hayo alieleza pia wizara pia imepanga kuweka mazingira bora ya kazi kwa kuwapatia vifaa vya kisasa na vinavyokwenda na wakati.

Akiwasiliasha maoni ya kamati ya Ustawi wa Jamii kuhusu makadirio ya mapato na matumizi ya wizara hiyo kwa mwaka 2021/2022, Mjumbe wa kamati hiyo Zawadi Amour Nassor, alisema kamati inaishauri wizara kukiimarisha kitengo cha masoko cha shirika la Magazeti ya Serikali Zanzibar.

Alisema hatua hiyo itapelekea magazeti ya shirika hilo yaweze kuwafikia wananchi kwa haraka na kusomwa na watu wengi Zanzibar na Tanzania bara kwa ujumla.

Aidha alisema kamati imebaini usambazaji na utoaji wa gazeti la Zanzibar leo hauridhishi kutokana na kukosekana kwa masoko ya uhakika ndani ya Tanzania hali inayosababisha shirika kuzalisha magazeti lakini mengi yanabakia ofisini kwa kukosa soko.

Hata hivyo kamati iliiomba serikali ya awamu ya nane kuzitaka taasisi zote zinazodaiwa na Wakala wa Uchapaji (ZAGPA) kulipa madeni hayo haraka kwa upande wa Zanzibar na Tanzania bara kwani kufanya hivyo kutasaidia wakala kuondokana na ukakasi wa matumizi.

Katika mwaka wa fedha 2021/2022 wizara hiyo imeomba kuidhinishiwa jumla ya shilingi 70,893,081,000 ambapo kati ya hizo shilingi 14,424,100,000 ni kwa matumizi ya kawaida na shilingi 56,468,981,000 kwa utekelezaji wa miradi ya maendeleo.

 

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango