Waandishi wahimizwa kuepusha migogoro


NA ASYA HASSAN

WAANDISHI wa habari wametakiwa kujikita katika uandishi wa habari zenye mnasaba wa kuleta amani katika jamii kwa lengo la kuepusha migogoro inayoweza kusababisha vuruga ndani ya jamii.

Hayo yalisemwa na Meneja Mkaazi wa shirika la Search for Common Ground, Hussein Sengu, alipokwa katika mafunzo ya usuluhishi na ujenzi wa amani yaliyowashirikisha waandishi wa habari kupitia mradi wa dumisha amani unaosimamiwa na shirika hilo.

Aliseama waandishi wa habari ni watu watakao weza kuifanya jamii kuwa na Amani ama kuisababisha kuingia matatani hivyo ni vyema kuzitumia kalamu na midomo yao kwa uweledi na ufanisi ili kuona Amani iliyopo inazidi kuimarika.

Meneja huyo alisema lengo la mafunzo hayo nikuwajengea uwezo waandishi wa habari juu ya namna ya kuripoti habari zenye mlengo wa kuleta amani katika jamii na sio kuongeza tofauti ziliyopo ndani ya maeneo yao.

Sambamba na hayo alisema jamii imekuwa ikikabiliwa na matatizo tofauti hivyo ni vyema waandishi kuandaa mazingira mazuri yatakayosaidia kuleta busara kwa jamii kuweza kupambanua na kuchanua njia sahihi ya kuzitua ili kuondosha tofauti zao.

“Jamii imekuwa ikikabiliwa na migogoro kisiasa hususani kipindi cha uchaguzi, migogoro ya ardhi na hata migogoro ya kijamii kama ya udhalilishaji wa kijinsia, hivyo vyombo vya habari vina wajibu wa kuhakikisha vinaripoti habari zenye malengo ya kuleta amani katika jamii,” alisema.

Hata hivyo alifahamisha kwamba endapo masuala hayo yasiposhughulikiwa ipasavyo yanaweza kuvuruga mfumo mzima wa amani iliyopo hapa nchini na kuleta athari kwao na taifa kwa ujumla.

Mkufunzi wa mafunzo hayo, Kelvin Pesambili, alisema waandishi wa habari wanapaswa kushiriki kikamilifu katika eneo hilo ili kuona jamii inafika wakati inakaa pamoja na kuacha tofauti zao.

Kwa upande wao, baadhi ya waandishi walioshiriki mafunzo hayo waliahidi kuwa mstari wa mbele kusaidia wananchi hususani pale kunapotokezea migogoro ili waishi kwa amani.

Mradi wa dumisha amani Zanzibar ni mradi wa miaka miwili, ambao unaendeshwa na taasisi ya Search for Common Ground kwa kushirikiana na The Foundation for Civil Society ya Tanzania, chini ya ufadhili wa Umoja wa Ulaya (EU).

 

 

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango