Waandishi watakiwa kuwasilisha kazi zenye ubunifu EJAZ

NA KHAMISUU ABDALLAH

KAMATI inayosimamia tuzo za umahiri wa uandishi wa habari Zanzibar imeeleza haja ya waandishi kuzingatia ubunifu na weledi katika kazi wanazoziwashilisha katika mashindano.

Kauli hiyo imetolewa na Makamu Mwenyekiti wa kamati hiyo inayoundwa na taasisi za habari Zanzibar, wakati wakitangaza msimu wa pili wa tuzo hizo kwa mwaka 2021/ 2022 kwa waandishi wa Zanzibar katika mkutano na waandishi wa habari uliofanyika katika ukumbi wa wa Wizara ya Utalii na Mambo ya Kale, Kikwajuni Zanzibar.

Alieleza kuwa ili kazi iweze kushinda, kuna haja ya mwandishi kufanya kazi ya ziada na kwamba upo umuhimu wa kuzingatia misingi ya taaluma na matokeo ya kazi ya mwandishi.

“Tunawashukuru wote walioshiriki na walioshinda katika msimu mwa kwanza na tunapoelekea msimu wa pili ipo haja ya kujiandaa na kujipanga kikamilifu ili kazi yako hata kama haikushinda basi iwe na matokeo,” alisema Dk. Mzuri ambae pia ni mkurugenzi wa TAMWA Zanzibar.

Akitangaza tuzo zitakazoshindaniwa kwa msimu wa pili, Katibu wa kamati hiyo, Imane Osmond Duwe, alisema tuzo hizo zitatolewa kama ni sehemu ya kuthamini kazi zinazofanywa na wandishi wa habari nchini.

Alisema tuzo hizo ni mwendelezo wa tuzo zilizotolewa Mei 30, mwaka huu ambapo katika msimu wa pili zimeongezeka na kufikia 11 badala ya tano za awali.

 Alizitaja tuzo hizo kuwa ni ya uandishi wa habari za uchumi wa buluu (tuzo ya Dk. Huseein Ali Mwinyi), tuzo ya uandishi wa habari za jinsia na udhalilishaji (tuzo ya Maryam Mwinyi) na tuzo ya uandishi wa habari za Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK) inayobeba jina la tuzo ya Maalim Seif Sharif Hamad.

Imane alizitaja tuzo nyengine kuwa ni ya uandishi wa habari za rushwa na uhujumu wa uchumi  (tuzo ya ZAECA), tuzo ya uandishi wa habari za kodi kwa maendeleo ya Bodi ya Mapato Zanzibar (ZRB), tuzo za uandishi wa habari za michezo, uandishi wa habari za uwajibikaji, uandishi wa habari za afya, uandishi wa habari za utalii, uandishi wa habari za mazingira na uandisihi wa habari wa haki za watoto.

“kamati inapenda kuwatangazia sekta za tuzo mwakani zimeongezeka kutoka tano hadi 11 ikiwa ni ongezeko la asilimia 100 la sekta za ushingani,” alieleza katibu huyo.

Aongeza kuwa habari zitakazowasilisha ziwe za uchunguzi ambazo zitakwenda kwa mfumo wa makala au habari za kawaida zilizoandikwa kwa upana ikiwa ni matokeo ya utafiti mpaka uliofanywa kuhusu masuala mbalimbali ya kisekta.

Hata hivyo alisisitiza kuwa kazi zitakazowasilishwa ziwe zimechapishwa katika magazeti au vipindi vilivyorushwa kwenye redio, televisheni za kawaida au za mtandaoni.

Akizungumzia vigezo vya kuzingatiwa wakati wa kuandaa au kuwasilisha kazi hizo, alisema ni pamoja na ubora wa kazi i, umuhimu wa kuzingatia uwiano sawa na jinsia na vyanzo vingi vya habari.

Vigezo nyengine ni ubunifu na upekee wa mada husika, matokeo baada ya kutoka habari au kipindi, uwasilishaji wa mada husika kimpangilio, ufasaha na mtiririko wa lugha, kuzingatia maadili ya uandishi weledi na matumizi ya takwimu.

Aliongeza kuwa kwa upande wa kipindi cha redio na televisheni kisizidi dakika 30 na picha na sauti ziwe katika ubora unaostahiki huku akitoa fursa kwa makala inayozungumzia sekta zilizoainishwa na taarifa zinazohusu Zanzibar zitakazorushwa na vyombo vya Tanzania bara.

Aliongeza kuwa kazi zitakazopokelewa ni zitakazotoka kuanzia Julai 2021 hadi Febuari 2022 hivyo aliwataka kukusanya kazi zao au kuandika katika maeneo hayo na kwamba zitaanza kupokewa kuanzia Machi 1 hadi 30, 2022.

“Tutambue kuwa sisi waandishi wa habari ni kiungo na muhimili muhimu katika kuhamasisha na kuleta maendeleo kwa ujumla katika taifa letu,” alibainisha.

Tunzo ya umahiri na weledi za uandishi wa habari Zanzibar kwa mwaka 2021/2022 ni miongoni mwa matukio muhimu yatakayoenda sambamba na na maadhimisho ya siku ya uhuru wa habari duniani ambayo huadhimishwa duniani kote kila ifikapo Mei 3 kila mwaka.

Kama ilivyo kwa mwaka huu, msimu wa pili wa tuzo hizo zinaandaliwa na taasisi mbali mbali ikiwemo Baraza la Habari Tanzania Zanzibar (MCT), Chama cha Waandishi wa habari Wanawake Zanzibar (TAMWA – Zanzibar), Klabu ya Waandishi wa habari Zanzibar (ZPC), ITV Zanzibar na Idara ya Mawasiliano na Taaluma za Habari Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar (SUZA) na jumuiya ya Waandishi wa Habari za Maendeleo Zanzibar (WAHAMAZA).

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango