Kunambi ashukuru mchango wa NMB kuimarisha huduma za jamii


NA SHADYA SAID, WMA

MKUU wa wilaya ya Magharibi ‘A’, Suzan Peter Kunambi, ameshukuru mchango unaotolewa na sekta binafsi katika maendeleo ya huduma za jamii wilayani humo katika nyanja tofauti.

Alieleza hayo wakati akitoa shukrani baada ya kupokea msaada wa mabati 200 na vitanda 30 kwa ajili ya skuli na vituo vya afya wilayani humo kutoka kwa benki ya NMB, hafla iliyofanyika katika skuli ya Msingi Mbuzini.

Alisema  msaada wa mabati  unakwenda kutatua changamoto ya uhaba wa madarasa katika skuli ya Mbuzini  na  skuli ya Mtoni Kigomeni kwani baadhi ya madarasa yamekuwa yakihitaji kuezekwa ili kukamilisha ujenzi wa madarasa ulioanza mwaka 2017.

“Kuchelewa kukamilika kwa madarasa haya kumesababisha wananfunzi kusoma nje ya madarasa na vitanda hivi vinakwenda kuongeza maeneo ya kupumzikia na kujifungulia katika vituo vyetu vya afya jambo ambalo ni la kushukuriwa sana,” alisema Kunambi.

Aidha aliziomba taasisi nyengine kuiga mfano wa benki hiyo ambayo ilisema imekuwa mstari wa mbele kusaidia jamii na makundi yenye uhitaji jambo linaloongeza kuaminika kwake katika jamii.

Akikabidhi msaada huo wenye thamani ya zadi ya shilingi milioni 30, Meneja wa biashara wa benki ya NMB Zanzibar, Abdalla Duchi, alisema benki hiyo imekuwa mdau mkubwa kwa serikali katika kuunga mkono  juhudi za maendeleo.

Alieleza kuwa misaada inayotolewa na benki hiyo maeneo mbali mbali nchini ni sehemu ya mpango wa benki hiyo kurudisha sehemu ya faida wanayoipata kwa jamii ili kuimarisha huduma na ustawi wa jamii.

“Fedha zinazotumika kama msaada katika shughuli za maendeleo kama haya, asilimia 100 zinatokana na faida ya kibiashara lakini pia kuthibitisha ukaribu wetu kwa jamii hivyo kuna umuhimu wa kujiunga nasi kwani faida inayopatikana inawarudia na kuwanufaisha wao wenyewe,” alieleza Duchi.

Akitoa maneno ya shukrani kwa niaba ya walimu na watoa huduma za afya wilayani humo, Daktari Dhamana wa kituoa cha afya Bumbwisudi, Dk. Said Fadhil, alisema vifaa vililivyotolewa vitatumika kama vilivyokusudiwa kupunguza changamoto ya uhaba wa vifaa unaowakabili kwa muda mrefu sasa.

Alieleza kuwa kwa muda mrefu baadhi ya vituo vya afya na hospitali za wilaya hiyo zimekuwa zikikabiliwa na changamoto ya vifaa jambo linalozorotesha huduma na kupelekea wananchi kufuata huduma maeneo ya mbali.

“Tumefarajika sana na msaada huu, kwani sisi kwenye afya tumekuwa na mahitaji ya vitanda vya kujifungulia na vifaa vyengine kwenye vituo vyetu hivyo msaada huu unakwenda kupunguza changamoto hiyo,” alieleza Dk. Said.

Katika hafla ya makabidhiano hayo, DC Kunambi aliambatana na viongozi mbali mbali wa wilaya, manispaa ya magharibi ‘A’ na kamati za skuli na afya, alikabidhiwa mabati 200 na vitanda 30 ikiwa ni mwendelezo wa misaada ya benki hiyo kwa huduma za jamii ambapo wiki iliyopita NMB ilikabidhi msaada wa shilingi milioni 25 kwa sekta za elimu na afya za mkoa wa Kusini Unguja.

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango