Waandishi andikeni habari zinazoepusha madhara 


NA MWAJUMA JUMA

WAANDISHI wa habari nchini wametakiwa kuongeza umakini katika utekelezaji wa majukumu yao ili kuepusha madhara kwa watu wengine.

Wito huo umetolewa na Mwenyekiti wa Klabu ya Waandishi wa Habari Zanzibar (ZPC) Abdallah Abdulrahman Mfaume, wakati akifungua mkutano wa kukusanya maoni ya kutengeneza kanuni za maadili ya uandishi wa habari na maudhui ya mitandaoni, uliofanyika katika ukumbi wa Dk. Ali Mohamed Shein, uliomo katika jengo la ZURA, Maisara Zanzibar.

Amesema katika uandishi na utangazaji wa habari kupitia vyombo habari mbali mbali, kuna haja ya kuzingatiwa kwa ustaarabu na utamaduni wa nchi badala ya kuiingiza usataarabu wa mataifa mengine sambamba na kuzihakikisha habari zinazitolewa.

“Kila nchi ina sheria na kanuni zinazosimamia maswala ya habari pamoja na yale masharti ya jumla ya kitaaluma, hivyo si vyema vyombo vyetu vikatumia kanuni za nchi nyengine na ndio maana taasisi zetu kama UTPC (Muungano wa Klabu za Habari Tanzania) zinaandaa kanuni kwa kushirikisha wadau wenyewe,” ameeleza Mfaume.

Aidha amesisitiza haja ya wanahabari hasa za mitandaoni kuepuka kutoa habari zinazowadhalilisha watu badala yake kujitahidi kupunguza madhara dhidi yaoHivyo alisema lazima wawe makini katika utoaji wa habari zao mbali mbali ili kuepusha udhalilishaji kwa wengine.

Washiriki wa mafunzo hayo walisema waandishi wa habari mwanapojiwekea miongozo na kuifuata katika kazi inasaidia na kurahisisha kazi zao za kila siku tofauti na kuwa na kutokuwa na muongozo kwa wote.

Mwandishi wa DW, Salma Said amesema pamoja na kufuatwa kwa maadili na miongozo inayotumia nchini, ipo haja ya kuzingatiwa kwa matamko na miongpozo ya kimataifa inayosimamia mwenendo wa habari nchini.

“Tukijiwekea na miongozo yetu inayosimamia maswala yetu, itaturahisishia zaidi katika kufanya kazi zetu bila ya migogoro au madhara kwetu, jamii na mamlaka zinazohusika,” amesema Salma.

Ameongeza kuwa katika mkutano huo, wamepata fursa ya kutoa maoni juu ya miongozo ambayo wanataaluma wenyewe wanataka yawemo kwenye kanuni ikiwemo kutoandika habari za kushitua ambazo zinaleta athari kwa watu wengine.

“Kimsingi mafunzo haya yalilenga kwa watu wa mitandao ya kijamii ambayo hutoa picha mbaya za kutisha hivyo katika mafunzo haya tumetoa maoni namna gani ya kuchapisha picha ambayo inatisha au haipaswi kutolewa na watu kuiona”, alisema.

Nae mwandishi, Haji Nassor kutoka mtandao wa ‘Pemba Today’ amesisistiza zaidi kufuata miongozo yao ambayo wamejiwekea na itawasaidia katika kazi zao bila ya kumuathiri mtu yeyote.

Amesema kwamba Zanzibar kumekuwa na tatizo la utoaji wa habari katika vyombo mbali mbali hasa zile za udhalilishaji ambazo huficha jina la mtoto aliyebakwa lakini hutajwa majina ya wazee wake au mahala anayoishi au kusoma.

“Kufanya hivyo humtambulisha mtoto jambo ambalo linalowafanya watoto kupata athari za kisaikolojia za muda mrefu, sambamba na kuwafanya wanyanyapaliwe na wenzao,” ameongeza.

Mapema Muwezeshaji katika mkutano huo kutoka Baraza la Habari Tanzania (MCT), Pili Mtambilike, alisema katika maandalizi ya kanuni hizo, mkazo mkubwa umewekwa kwenye mitandao ya kijamii kutokana na kuwepo kwa mwingiliano wa hali ya juu kati ya vyombo vya kawaida na vya mitandaoni.

“Tulipitia kanuni za maadili ya uandishi wa habari kwa vyombo vyote lakini tumejikita zaidi katika habari za kimtandao kutokana na kuwepo kwa muingiliano wa hali ya juu kati ya vyombo hivyo lakini hata vyombo vya kawaida vinajielekeza huko,” alisema.

Alisema wanatayarisha kanuni hizo ili kuhakikisha kwamba wanachama wao wanakuwa na miongozo ya kuwaongoza waandishi wa habari, jinsi ya kuandika habari zinazozingatia maadili na taaluma ya uandishi wa habari.

Akizungumzia mkutano huo, Katibu Mkuu wa ZPC, Mwinyimvua Nzukwi, alieleza kuwa mkutano huo ni sehemu ya utekelezaji wa mradi kukuza uhuru wa habari na upatikanaji wa taarifa unaotekelezwa kwa pamoja na Muungano wa Klabu za Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC) na Shirika la International Media Support la Denmark (IMS), kwa ufadhili wa Umoja wa Nchi za Ulaya (EU).

Alieleza kuwa pamoja na shughuli nyengine za mradi huo, klabu za waandishi wa habari kwa kushirikiana na wadau wengine wa habari, wametakiwa kuandaa kanuni ambazo zitatumika kusimamia mwenendo wa upashanaji habari nchini.

 

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango