TASAF yaidhinishiwa 5.5b/- kukabili athari za UVIKO 19

NA MWANDISHI WETU, DAR ES SALAAM

MKURUGENZI Mtendaji wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii Tanzania (TASAF), Ladislaus Mwamanga, amesema mfuko huo umeidhinishiwa shilingi bilioni 5.5 kati ya fedha zilizotolewa mkopo wenye masharti nafuu kutoka Shirika la Fedha Kimataifa (IMF).

Mwamanga alieleza kuwa TASAF itazitumia fedha hizo kuondoa athari za kiuchumi zilizochochewa na mripuko wa UVIKO 19 kwa kaya 40,740 za walengwa wa TASAF, wenye uwezo wa kufanya kazi katika miradi ya jamii wanaoishi Mjini.

Alieleza hayo jana katika ofisi za jijini hapa, wakati akizungumza na wandishi wa habari katika ofisi za mfuko huo kuhusiana na Utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo kwa Ustawi wa Taifa na Mapambano dhidi ya UVIKO -19 kwa mpango wa kunusuru kaya za walengwa wa TASAF.

Alisema kupitia hizo kaya za walengwa wenye uwezo wa kufanya kazi wanaoishi katika maeneo ya mjini, watafanya kazi katika miradi ya jamii na kulipwa ujira wa wastani wa shilingi 135,000 kwa kila kaya ili kufufua au kuimarisha shughuli zao za kukuza uchumi wa kaya zao zilizoathirika zaidi kutokana na UVIKO 19.

Aliongeza kuwa, serikali imedhamiria kuwaondoa wananchi wake katika umaskini wa kipato kwa kuwapatia ruzuku za kujikimu, ajira za muda, na kuwaongezea ujuzi, maarifa na elimu ya ujasiriamali ili wakidhi mahitaji yao.

“Fedha zilizotengwa kwa ajili ya TASAF ambayo ni shilingi 5.5 zitaelekezwa katika utoaji wa ruzuku na utekelezaji wa miradi ya ajira za muda kwa kaya za walengwa ili kupata kipato ambacho kitaziwezesha kaya hizo kujikwamua kiuchumi na kupunguza athari za UVIKO - 19 na kuongeza rasilimali na miundombinu ambayo itatumia na Jamii yote katika Mitaa na Shehia,” alisema.

Alisema Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania inaendelea kuteleleza mipango na mikakati mbali mbali katika kupunguza umasikini wa Watanzania na inafanya jitihada za kupata fedha kutoka vyanzo vya ndani, mikopo na misaada kutoka kwa wadau wa maendeleo ili kuhakikisha watu wanaondokana na umasikini.

“Utoaji wa sehemu ya mkopo huo nafuu kwa ajili ya Mpango wa TASAF ni kielelezo tosha kwamba serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, inawajali wananchi wake hasa wale wanaoishi katika mazingira duni,” alisema Mwamanga.

Alisema Walengwa hao watatekeleza miradi ya ajira ya muda itakayochangia kuongeza upatikanaji wa chakula na kuboresha huduma katika sekta za afya, elimu, maji na hifadi ya mazingira.

Mwamanga alisema usimamizi utafanyika kuhakikisha miradi inatekelezwa kwa viwango na thamani ya fedha iliyotengwa, kwa ajili ya kusisimua uchumi wa kaya uliokuwa umedorora kutokana na UVIKO – 19.

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango