Wazazi wekezeni kwenye elimu za watoto wenu - Mbunge

NA MWANDISHI WETU

MBUNGE wa Jimbo la Dimani, Mustapha Mwinyi Kondo, amewataka wazazi na walezi wa wanafunzi wa skuli ya Msingi Kisauni kuwekeza zaidi katika elimu za watoto wao badala ya mambo mengine yasiyo na tija kwa maisha yao ya sasa na baadae.

Mustapha alieleza hayo wakati wa sherehe za kuwaaga walimu wa waliostaafu na kuwapongeza wanafunzi waliofaulu michipuo katika mitihani yao ya taifa ya darasa la sita mwaka 2020.

Katika sherehe hizo zilizofanyika katika skuli hiyo iliyopo wilaya ya Magharibi ‘B’ Unguja, Mbunge huyo alieleza kufanya hivyo pia kutachangia maendeleo ya skuli hiyo wakati msaada unapohitajika ili watoto wao kufanya vizuri katika masomo yao.

Alisema licha ya serikali kutoa elimu bila ya malipo lakini wazazi wanapaswa kuchangia baadhi ya misaada ya kielimu inapohitajika pale uongozi wa skuli unapowataka wazazi na walezi kutoa misaada yao katika kutatua baadhi ya changamoto zinazoikabili Shule hiyo.

Alisema baadhi ya wazazi na walezi ni wagumu kuchangia maendeleo ya skuli na wapo tayari kugharamika katika shughuli nyengine za kijamii kama harusi wakati elimu ni msingi wa maisha kwa watoto wao.

“Baadhi yetu (wazazi na walezi) wanafanya sherehe za harusi kwa gharama kubwa lakini huwa wagumu kuchangia skuli kwa ajili ya maendeleo ya watoto wetu huwa wagumu,” alisema Mbunge huyo.

Alisema kuwa walimu wanajukumu kubwa la kuwasimamia wanafunzi ili kufanya vizuri katika masomo yao na kuwa na watalamu bingwa hapo baadae.

“Tunafahamu kuwa walimu mna changamoto nyingi ikiwemo mishahara midogo mnayopata lakini changamoto hiyo isiwe sehemu ya kutoonesha bidii zenu katika kutoa elimu kwa watoto wetu,” alisema.

Akisoma risala kwa niaba ya Walimu wenzake, Mwalimu Maryam Masoud, alisema licha ya mafanikio yaliyopatikana yakiwemo ya kuongezeka kwa ufaulu kwa baadhi ya wanafunzi, skuli hiyo inakabiliwa na upungufu wa madarasa hali inayopelekea msongamano wa wanafunzi madarasani hadi kufikia wastani wa wanafunzi 120.

Alisema hali hiyo ya wingi wa wanafunzi madasani linashusha ufanisi katika utendaji kwa Walimu na wanafunzi wakati darasa moja linahitajika kuwa na wastani wa wanafunzi 45.

Aliitaja changamoto nyengine kuwa ni uchakavu wa madarasa ambayo baadhi ya madasa yamejaa vumbi kutokana na kuvunjika kwa saruji iliyowekwa sakafuni jambo ambalo linahatarisha afya za walimu na wanafunzi.

Kwa upande wake Kaimu Mwalimu Mkuu wa Skuli hiyo, Ahmada Haji, alisema walimu waliostaafu ni waaandaaji wazuri wa wanafunzi wa ambao baadhi yao wamefanikiwa kufaulu vizuri mitihani yao ya taifa.

Mwalimu Ahmada pia aliwapongeza wanafunzi wa kike kwa kufanya vizuri zaidi katika mitihani yao ya taifa mwaka jana ikilingnaishwa na wanafunzi wa kiume na kuwahimiza wanafunzi wote kusoma kwa bidii na kuachana na vitendo viovu ambavyo vitawasababishia kutofikia malengo yao.

Skuli ya Kisauni Msingi iliyoanzishwa rasmi mwaka 1992 ikiwa na wanafunzi 325 (Wanaume 167 na Wanawake 162) kwa sasa ina wanafunzi 1,569 ambapo katika kipindi cha mwaka 2013 - 2020 imepasisha wanafunzi 35 wa mchipuo ambapo wanafunzi watatu wa kike waliofaulu michipuo mwaka 2020 walitununikiwa zawadi.

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango