ZATUC yahimiza wafanyakazi kutambua sheria za kazi, ajira

NA MWANDISHI WETU

SHIRIKISHO la Vyama vya Wafanyakazi Zanzibar (ZATUC), imesema kuna umuhimu kwa wafanyakazi kujua sheria za kazi ili ziweze kuwasaidia katika utekelezaji wa majukumu yao pamoja na kuwaongoza pale wanapotaka kudai haki zao.

Katibu Mkuu wa chama hicho, Khamis Mwinyi Mohammed (pichani), alisema hayo alipokuwa akizungumza na gazeti hili katika kikao cha kujadili haki za wafanyakazi na utekelezaji wake kilichoandaliwa na Shirika la msaada la kimataifa la Actionaid katika ukumbi Kitengo cha kudhibiti Malaria, Mwanakwerekwe.

Alisema asilimia kubwa ya wafanyakazi hawajui sheria hizo jambo ambalo husababisha kuleta mkanganyiko mkubwa baina yao na waajiri pale kunapobidi kudai baadhi ya haki zao.

“Wafanyakazi wanakabiliwa na changamoto nyingi ikiwemo upataji wa haki zao, kwani asilimia kubwa wanashindwa kutofautisha haki za msingi na nyenginezo jambo ambalo husababisha kuleta malalamiko ndani ya taasisi mbalimbali,” alisema.

Sambamba na hayo alisema kutokana na hali hiyo wamekuwa wakifanya jitihada mbalimbali ikiwemo kuwapatia elimu wafanyakazi hao ili waweze kufahamu sheria hizo na kuzifanyia kazi ili kuona kila mfanyakazi ananufaika nazo.

Aidha Mwinyi alitumia fursa hiyo kuzitaka taasisi mbali mbali kuona umuhimu wa kuwapatia taaluma wafanyakazi wao ili kila mmoja aweze kuzifanyia kazi.

Kwa upande wa Mratibu wa shirika la Actionaid, Baker Khamis, alisema wameamua kutoa mafunzo hayo ili kuondosha baadhi ya changamoto zinazowakwaza wafanyakazi kutokana na kutofahamu sheria za kazi. 

Alisema wataendelea kutoa elimu hiyo kwa wafanyakazi wa kada mbalimbali ili ziweze kuwasaidia katika utekelezaji wa majukumu yao.

Alisema wafanyakazi wanakabiliwa na changamoto nyingi ikiwemo taratibu za mikataba hazifuatwi, mishahara midogo na mambo nyengine hivyo kupitia mafunzo hayo yatasaidia kuweza kufahamu sheria izo.

Kwa upande wa washiriki wa mkutano huo walisema wafanyakazi wengi wanazikosa haki zao makazini mwao kwa kuwa hawajui sheria na hatua za kufuata ili waweze kupata haki hizo.

Miongoni mwa washiriki hao Haji Maktuba Haji, kutoka taasisi ya watembeza watalii alisema kuna mahitaji makubwa ya kutolewa elimu hiyo kwa wafanyakazi ili kuwaondoshea changamoto mbali mbali wanazokuta nazo. 

“Tumekuwa tukikutana na changamoto mbali mbali ikiwemo ya upatikanaji wa haki kutokana na wengi wetu kushindwa kufuatia sheria na taratibu zilizowekwa,” alieleza Haji.  

Kwa upande wa mwanasheria Jambia Jambia, ambae aliyekuwa mkufunzi wa mafunzo hayo, alisema sheria za kazi zimetungwa ili kusaidia kila mmoja kufahamu wajibu na majukumu yake pamoja na kuondosha migogoro ndani ya sehemu za kazi. 

Mafunzo hayo ya siku moja yamewashirikisha wafanyakazi kutoka taasisi mbali mbali za serikali na binafsi yaliandaliwa na Actionaid kwa lengo la kujenga uelewa na uwezo wa wafanyakazi kuzitambua sheria za kazi na ajira.

 

 

 

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango