Andikeni habari zitakazotatua migogoro – Mfaume

KHAMISUU ABDALLAH NA MADINA ISSA

WAANDISHI wa habari nchini wameshauriwa kuwa sehemu ya utatuzi wa migogoro ili kuifanya jamii kuwa na mshikamano utakaosaidia kuondoa tofauti hasa za kisiasa na kuharakisha maendeleo ya nchi.

Mwenyekiti wa Klabu ya Waandishi wa Habari Zanzibar (ZPC), Abdalla Abdulrahman Mfaume, alieleza hayo jana wakati akifungua mafunzo ya uandishi wa habari za utatuzi wa migogoro na ujenzi wa amani kwa wanahabari wa vyombo mbali mbali yaliyofanyika katika ukumbi wa Kitengo cha Uzazi Shirikishi, Kidogochekundu Mjini Unguja.

Alisema Zanzibar inakabiliwa na migogoro mingi ikiwemo ya ardhi, kijamii, kiuchumi, kidini na kisiasa hivyo ikiachwa bila ya kuripotiwa katika vyombo vya Habari, itashindwa kupatiwa ufumbuzi.

Alisema kwa mujibu wa tathmini iliyofanywa, mara nyingi waandishi wa habari hujikita zaidi katika uandishi wa habari za siasa kipindi cha uchaguzi tu hali inayochangia uwepo wa migogoro hiyo.

“Ikiwa tutaripoti na viongozi wakasikia basi migogoro mingi iliyopo katika jamii inaweza kufuatiliwa na kutatuliwa na hili ndio lengo letu la kutoa mafunzo haya,” alibainisha.

Akizungumzia lengo la mafunzo hayo alisema ni kuhakikisha waaandishi wa habari, wanajengewa uwezo juu ya uandishi wa habari zitakazozuia na kutatua migogoro.

Mapema Katibu wa ZPC, Mwinyinvua Abdi Nzukwi, alisema mafunzo hayo ni sehemu ya utekelezaji wa mradi wa jenga amani yetu unaotekelezwa kwa pamoja na Search for Common Ground, Kituo cha huduma za sheria Zanzibar (ZLSC) na Kituo cha Msaada wa Sheria na Haki za Binadamu (LHRC).

“Mafunzo haya yana manufaa makubwa kwao na yatawasaidia kwa kiasi kikubwa katika majukumu yao ya kila siku hivyo ni vyema wakazingatia ili kuongeza weledi na maarifa yatakayosaidia kudhibiti na kutatua migogoro badala ya kuchochea,” alieleza Nzukwi.

Akiwasilisha mada ya dhana na vyanzo vya migogoro, Mwezeshaji wa mafunzo hayo, Ali Haji Mwadini, alisema kuna migogoro mbali mbali katika jamii, familia na sehemu za kazi inayosababishwa na uchache wa rasilimali, pesa, madaraka, ajira, makundi yenye dhana potofu.


Aidha Mwadini alibainisha kwamba Zanzibar imetoka katika migogoro hasa ya kiasiasa lakini kuundwa kwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa (GNU) mwaka 2010 imesaidia kuwaunganisha Wazanzibari na kuwa kitu kimoja.

“GNU (Serikali ya Umoja wa Kitaifa) ina manufaa makubwa kwa wananchi wa Zanzibar, hivyo vyombo vya habari vina jukumu la kuhakikisha umoja, mshikamano na maelewano yaliyopo yanaendelezwa,” alisema Mwadini ambae pia ni mhariri mtendaji wa shirika la magazeti ya serikali Zanzibar.

Hivyo, alibainisha kwamba ni vyema kwa wanahabari kuendelea kuelimisha jamii juu ya umuhimu wa serikali hiyo ambayo imetokana na maridhiano ya kisiasa yaliyofikiwa na vyma vya CCM na ACT - Wazalendo.

Baadhi ya wanahabari walioshiriki mafunzo hayo walisema, yana umuhimu mkubwa kwao katika kuelimisha na kuibua changamoto zinazoikabili jamii na kuelimisha umuhimu wa serikali ya umoja wa kitaifa ambayo ina manufaa makubwa katika taifa.

Bakari Masoud kutoka Plus Radio na Amina Mchezo wa Coconut FM, walisema wanahabari wana nafasi kubwa katika kuisaidia jamii kutatua migogoro na kuona jamii inafaidika kupitia uwepo wao.

Aidha walisema wanahabari ni daraja kutoka sehemu moja kwenda nyengine kwa kuwasemea wananchi ambao sauti zao ni ndogo na kuweza kufanyiwa kazi hivyo ni jukumu lao kutumia kalamu zao,sauti zao na vyombo vyao katika kutatua migogoro hiyo.

Walimpongeza muwezeshaji huyo kwa kuwakumbusha jukumu lao katika jamii katika kutatua migogoro mbalimbali ili kuona Zanzibar inaendelea kuwa na amani umoja na mshikamano na nchi inapiga hatua kiuchumi.

Mafuzo hayo ya siku tatu yameandaliwa ZPC kupitia mradi wa Jenga Amani Yetu unaotekelezwa na Search for Common Ground, Kituo cha Huduma za Sheria Zanzibar (ZLCS) na Kituo cha Msaada wa Sheria na Haki za Binaadamu (LHRC) yamefadhiliwa na Umoja wa Ulaya (EU).              


Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango