NMB, Mambo ya kale wakubaliana kuimarisha utalii Zanzibar 

NA MWANDISHI WETU

WIZARA ya Utalii na Mambo ya Kale Zanzibar imetiliana saini makubaliano ya  kuimarisha shughuli za watembeza watalii na benki ya NMB kwa kutoa mafunzo ili kurasimisha shughuli zao waweze kukopesheka.

Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Fatma Mabrouk Khamis, alitia saini kwa niaba ya wizara hiyo huku Afisa Mkuu wa Biashara na Wateja Binafsi  Filbert Mponzi aliiwakilisha benki ya NMB.

Akizungumza wakati wa hafla ya kusaini makubaliano hayo, Fatma alisema benki makubaliano hayo yamelenga kuinua shughuli za vijana wanaotembeza watalii nchini.

Alieleza kuwa mitaani kuna vijana wengi wanaofanya kazi ya kuongoza watalii bila ya ujuzi wa kutosha hivyo kuharibu taswira ya Zanaibar hivyo makakati huo utawasaidia kuimarishawa ujuzi na maarifa yao.

“Wapo vijana wanaojihusisha na utalii mfano ‘beach boys’ ambao wanafanya utalii wa mikobani na mara nyingi wanakuwa kero kwa wageni. Kupitia makubaliano haya, tutawapa mafunzo na kuangalia ni kwa namna gani tunaweza kuwarasimisha na kuwaongoza,” alisema Fatma.

Mbali na hayo alibainisha kuwa wizara ina mpango wa kuimarisha mashamba ya viungo, ambayo yanatumika na vijana wanaojihusisha na shughuli hizo.

“Tutashirikiana kuwapa mafunzo na mikopo kuimarisha bidhaa zao, tutawashika mkono ili kuhakikisha wanatoa huduma nzuri na bidhaa nzuri,” alisema Fatma.

Alieleza kuwa katika ziara waliyofanya hivi karibuni, wamebainoi kuwa yapo mashamba ya viungo yasiyo na viwango hivyo wizara ina mkakati wa kuanza kuhuisha vijiji ili kuwa na vijiji vya utalii.

Nae Afisa Mkuu wa Biashara na Wateja Binafsi wa NMB, Filbert Mponzi, alisema benki hiyo imefanya mambo mengi visiwani Zanzibar kwa lengo la kuinua sekta ya utalii.

Alieleza kuwa katika kuendeleza azma hiyo, wameamua kupeleka vituo vya mauzo 100 na kuiomba Wizara ya Utalii kuwaelekeza vituo watakaposambaza vifaa kwa ajili ya kufanyia malipo.

“NMB ndio benki kubwa zaidi nchini ambayo serikali ni mdau mkubwa lakini pia inaongoza kwa kupata faida yaani kwa ukubwa, tunapoingia kwenye jukumu kama hili hatuna wasiwasi,” alisema Mponzi.

“Tumeamua kujifunga kwa Wizara ya Utalii na Mambo ya Kale Zanzibar maana yake tutafanya kitu kikubwa katika utalii Zanzibar,” alisema Mponzi.

Mponzi alisema kufanya hivyo ni kuunga mkono safari ya kuimarisha uchumi wa bluu na kwenda sambasamba na dunia ili kukuza uchumi kupitia mifumo ya kidigitali katika shughuli za utalii nchini.

Alisema hatua hiyo inalenga kutoa elimu na kuhamasisha watalii wazidi kutembelea vivutio vya kitalii vilivyopo Zanzibar kupitia matamasha na promosheni mbali mbali.

Aliongeza kuwa watasambaza mashine za malipo kwenye vituo vya makusanyo na vivutio vya utalii ili kuwawezesha watalii kulipia ada na tozo zote kupitia kadi zao za kielektroniki za Mastercard, Visa na UnionPay.

Alifafanua kuwa hatua hiyo itapunguza ulazima wa watalii kutembea na fedha taslim hivyo kuwawezesha kufanya malipo kwa njia salama na rahisi.

 

 

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango