Polisi, wanahabari wakubaliana kushirikiana

NA MWANDISHI WETU

WAANDISHI wa habari na watendaji wa jeshi la polisi wameahidi kuendelea kushirikiana katika utendaji wa kazi zao kwa maslahi ya taifa.

Makubaliano hayo yalifikiwa katika mdahalo wa kitaaluma ulioyakutanisha makundi mawili hayo na kujadili wajibu na majukumu yao.

Mdahalo huo uliokuwa na maudhui ya usalama kwa waandishi wa habari na mahusiano kati ya waandishi wa Habari na jeshi la polisi, yaliyoandaliwa na Klabu ya Waandishi wa Habari Zanzibar (ZPC) kupitia  mradi wa usalama kwa wandishi wa habari unaotekelezwa na muungano wa klabu za waandishi wa Habari Tanzania (UTPC) na Shirika la International Media Support (IMS).

Akifungua mdahalo huo uliofanyika katika jengo la ZURA mjini Unguja, Mwenyekiti wa ZPC, Abdalla Adulrahman Mfaume, alisema jeshi la polisi lina wajibu wa kuhakikisha waandishi wa habari wanafanya kazi katika mazingira salama na kuhakikishiwa ulinzi.

Hata hivyo, alisema wakati mwengine hujitokeza changamoto zinazosababisha pande hizo mbili kutoaminiana hali inayopaswa kuondoka.

Licha ya changamoto hizo, alisema bado pande hizo mbili zinaendelea kushirikiana kuhakikisha jamii inapata taarifa stahiki na kwa wakati.

Akizingumza kwa niaba ya Kamanda wa Polisi mkoa wa Mjini Magharibi,  mkuu wa utawala wa jeshi la polisi mkoani humo, Kamishna Msaidizi wa Polisi,  Abubakar Khatib Ally, alisema mkutano huo ni fursa muhimu kwa waandishi wa habari na polisi kushirikiana na kujenga uhusiano mwema katika kazi zao.

Alisema licha ya tofauti zinazojitokeza bado pande hizo mbili zinahitaji kufanya kazi kwa pamoja katika kutoa taarifa kwa wananchi.

Hata hivyo, aliiomba ZPC kutumia mafunzo yanayoandaliwa na jeshi la polisi kwa askari wake kutoa mada kuhusu uhusiano mwema wa waandishi na jeshi la polisi ili ushirikiano uliopo uendelee.

Aidha wakiwasilisha mada kwenye mdahalo huo, Mwandishi mwandamizi wa habari, Dk. Saleh Yussuf Mnemo na ASP Ramadhan Himid Haji kutoka makao makuu ya polisi Zanzibar, walisisitiza umuhimu wa pande mbili hizo kushirikiana na  kuvumiliana katika utendaji kazi wa pande hizo mbili.

Walieleza kuwa licha ya kila taaluma kuwa na misingi yake, bado makundi hayo yanategemeana katika kukamilisha majukumu yao hivyo ipo haja ya kushirikiana kikamilifu.


Aidha waliiponeza waandaaji wa mdahalo huo kwa kutoa fursa wa watendaji wa pande zote mbili kujadili kwa pamoja changamoto na mafanikio yaliyopo hatua ambayo itasaidia kufikia malengo ya kuwa na Tanzania yenye amnani, utulivu na Uhuru wa kujieleza.

 

 

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango