TAARIFA MAALUM KWA WAANDISHI WA HABARI

 Description: letter head

TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI KUHUSU UTEKELEZAJI WA MAOMBI YA WAANDISHI KWA RAIS WA ZANZIBAR NA MWENYEKITI WA BARAZA LA MAPINDUZI DK. HUSSEIN ALI MWINYI

Awali ya yote napenda kutumia fursa hii kwa niaba ya Mwenyekiti wa Klabu ya Waandishi wa Habari Zanzibar (ZPC), kuwajullisha ya kwamba baadhi ya mambo yaliyowasilishwa na waandishi wa habari mbele ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi katika kikao cha tarehe 18/05/2022 yameanza kufanyiwa kazi.

Katika kikao hicho cha faragha kilichofanyika katika Ikulu ya Zanzibar, waandishi wa habari walipata fursa ya kuzungumza na Rais mambo mbali mbali yanayohusu mwendendo na hali halisi inayohusiana na tasnia ya habari nchini, hali tunayoamini imeongeza uelewa wa kiongozi huyo wa nchi na wasaidizi wake juu ya mazingira ambayo waandishi wa habari wa Zanzibar wanayofanyia kazi.

Pamoja na maelezo ya waandishi ambayo baadhi yao yalipatiwa majibu na kutolewa ufafanuzi wakati wa kikao hicho, pia waandishi waliwasilisha ombi mahususi kuhusu nafasi za mafunzo ili kujiongezea ujuzi na utaalamu kuimarisha ufanisi wa kazi zao.

Kuhusiana na ombi hilo, napenda kuwajulisha kwamba jambo hilo limeanza kufanyiwa kazi na kutolewa maelekezo kupitia barua iliyowasilishwa kwa ndugu Abdallah A. Mfaume, Mwenyekiti wa Klabu ya Waandishi wa Habari Zanzibar (ZPC) tarehe 20/08/2022 na kutolewa maelekezo kwamba tunapaswa kutumia fursa za masomo zilizotangazwa na ubalozi mdogo wa India nchini.

Katika barua hiyo iliyoambatanishwa na maelekezo kutoka ubalozi wa India nchini, inawataka waandishi wa habari kutumia fursa zinazotolewa na taasisi ya ITEC kupitia mpango wa ushirikiano baina ya Tanzania na India kwa mwaka 2022/2023 (Aprili 2022 – Machi 2023).

Hivyo waandishi wenye hamu ya kupata mafunzo hayo wanatakiwa kufanya maombi ya masomo wanayotaka kwa kutembelea tovuti ya taasisi hiyo ambayo ni https://www.itecgoi.in ili kupata mpangilio wa masomo na mafunzo yanayotolewa kupitia mpango huo.

Baada ya kukamilisha maombi, muombaji atalazimika kupakua (download) fomu ya maombi na kuiwasilisha katika Wizara ya nchi, Ofisi ya Rais, Katiba, Sheria, Utawala wa Umma na Utawala bora au Wizara ya Mambo ya nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki ofisi ya Zanzibar na tunashauri nakala ya maombi hayo yawasilishwe ZPC kwa ajili ya kumbukumbu.

Kwa taarifa hii, ninawashajihisha waandishi wote wenye utashi, hamu na sifa ikiwemo ya umri wa kati ya miaka 25 – 45 kutumia fursa hii kikamilifu lakini wenye zaidi ya umri huo kupitia tovuti hiyo na kuangalia kozi za mafunzo yanayotolewa na taasisi hiyo.

Aidha kwa niaba ya waandishi wa habari wa Zanzibar, tunashukuru hatua hizi za Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi katika kuiimarisha sekta ya habari na tunamuomba aendelee kutoa kipaumbele kwa sekta hii kama kichocheo cha maendeleo ya nchi na watu wake.

Ni matumaini yangu kwamba, hatua hizi zilizochukuliwa katika kipindi kifupi, kitachochea kasi ya waandishi kujituma na kujitokeza kuomba mafunzo yanayotolewa na taasisi hiyo hata yale yaliyopo nje ya kada ya uandishi wa Habari.

Kwa mara nyengine natoa shukrani na pongezi kwa waandishi wa habari waliohudhuria kikao na mhe. Rais kwa kuonesha haja ya kuijiendeleza na kuiendeleza kada ya uandishi wa habari, jambo ambalo limekuwa likisisitizwa na vyama vyetu vya kitaaluma, hivyo naomba, tusipoteze fursa iliyotolewa.

Ahsanteni.

Imetolewa na:

Mwinyimvua A. Nzukwi,

Katibu Mkuu – ZPC.

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango