Waandishi watakiwa kuwa makini matumizi mitandao

NA ASYA HASSAN

WAANDISHI wa habari wametakiwa kutanua wigo katika matumizi ya mitandao ya kijamii ili kurahisisha utendaji wao wa kazi na kuleta tija.

MWENYEKITI wa klabu ya waandishi wa Habari Zanzibar (ZPC), Abdallah Abdulrahman Mfaume, alisema hayo alipokuwa akifungua kongamano la wadau wa habari ikiwa ni miongoni mwa shudhuli za maadhimisho ya siku ya uhuru wa vyombo vya habari duniani ngazi ya klabu.


Alieleza kuwa hatua hiyo itasaidia kwa kiasi kikubwa kubadilisha jamii kutumia mitandao hiyo kwa faida badala ya hasara kutokana na jukumu kubwa la kuelimisha jamii na kuleta mabadiliko katika nchi.

Sambamba na hayo Mwenyekiti huyo aliiomba serikali kuendelea kushirikiana na wadau wa habari kufanya mapitio ya sheria, sera na kanuni zinazosimamia sekta ya habari ili kuondosha changamoto zinazokwaza uhuru wa Habari na Uhuru wa kujieleza.

Hata hivyo aliwasisitiza waandishi wa habari kuzalisha habari na vipindi bora ili vyombo vya habari viendelee kuwa daraja la kupashana Habari na kupeana mrejesho kati ya serikali na wananchi.

Akizungumzia mafanikio maadhimisho ya siku hiyo kitaifa na kimataifa, Mfaume alisema yamesaidia kwa kiasi kikubwa kupunguza baadhi ya vikwazo na changamoto zilizokuwa zikiwakabili waandishi na vyombo vya habari.

Akitaja miongoni mwa mafanikio hayo kuwa ni pamoja na mauaji ya waandishi wa habari na watendaji wa vyombo vya habari, kuteswa kinyama, kunyimwa habari, maslahi duni, ukatili na udhalilishaji wa wanahabari hasa wanawake.

Mbali na hayo alisema juhudi zaidi zinahitajika ili kuona vikwazo vyote visivyo vya msingi vinaondolewa ili kuona habari iendelee kuwa bidhaa muhimu kwa umma.

Mapema Katibu wa ZPC, Mwinyimvua Abdi Nzukwi, alisema kupitia siku hiyo, klabu hiyo imekuwa ikifanya kongamano na mikutano mbali mbali kwa waandishi wa habari ili kujadili mafanikio, changamoto na vikwazo vinavyowakwaza waandishi ili ziweze kutafutiwa ufumbuzi hatua kwa hatua.

Wakiwasilisha mada katika kongamano hilo lilihudhuriwa na maofisa habari, waandishi wa habari na wadau wa Habari, muhariri wa shirikia na magazeti ya serikali, Juma Khamis Juma na Katibu wa kamati ya muda ya Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) ofisi ya Zanzibar, Salma Amir Lusangi, waliwataka waandishi kusimamia misingi ya kazi zao ili kujiepusha kuingia katika matatizo.

“Pamoja na kwamba baadhi ya sheria zina mapungufu, ipo haja ya kuchukua juhudi ya kuzisoma ili kujiepusha kuingia kwenye mtego wa kuzivunja,” alieleza Khamis.

Wakichangia mada zilizowasilishwa kwenye kongamano hilo, baadhi ya waandishi hao walipokuwa walisema licha ya kuadhimishwa kwa siku hiyo kila mwaka lakini bado waandishi wa habari wamekuwa wakikabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo kutokua na mikataba ya ajira na stahiki zao za msingi.

Aidha waliiomba ZPC kushirikiana na taasisi nyengine za habari kuendelea kusimamia misingi ya taaluma pamoja na kuanzisha utaratibu wa kukutana na kutathmini hali ya uandishi wa habari kama njia mojawapo ya kuimarisha upatikanaji wa uhuru wa habari.

Kongamano hilo la siku moja liliandaliwa na ZPC kwa ufadhili wa Shirika la kimataifa la Misaada la Sweden (SIDA) kupitia mpango wa kuimarisha klabu za waandishi wa habari unaotekelezwa na Muungano wa Klabu za Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC).  

    

 

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango