'Andikeni habari zitakazochochea maendeleo '

NA MWANDISHI WETU

WANAHABARI nchini wametakiwa kubadilika na kuandika habari zitakazochochea maendeleo ya nchi na watu wake.

Wito huo Umetolewa na Mkurugenzi Idara ya Habari Maelezo Zanzibar, Hassan Khatib Hassan, (wa katitaki pichani) alipokua akifungua mafunzo ya waandishi wa vyombo mbali mbali vya habari yaliyoandaliwa na Klabu ya Waandishi wa Habari Zanzibar (ZPC) kwa kushirikiana na shirika la Internews Tanzania, yaliyofanyika katika ukumbi wa Uhuru, Kariakoo Zanzibar.

Alieleza kuwa vyombo vya habari ni muhimu kwani vinaweza kuandika habari zenye kuibua hamasa ya wananchi kufikia dhamira ya serikali na kufichua maovu dhidi ya maendeleo ya nchi na watu wake.

Hassan aliongeza kuwa wananchi walio wengi wanasikiliza na kufuatilia vyombo vya habari wakiamini kuwa watapata taarifa za ukweli na zinazozingatia weledi na sio taarifa za kubuni ama kughushi.

 “Iwapo mtajikita zaidi kutaka kuwafurahisha wasomaji na wasikilizaji au watazamaji basi tunaweza kufika pahala tukapoteza malengo ya kazi yetu tunayoifanya,” alisema Mkurugenzi huyo.

Aidha aliwataka waandishi wa habari kuacha tabia ya kusubiri habari za kuitwa na wanasiasa au viongozi wa taasisi badala yake waanzishe utaratibu wa kujitafutia habari, jambo linaloongeza thamani na uhalisia wa tasnia hiyo.

Alisema imefika wakati kuhakikisha waandishi wanaandika habari za uchunguzi na kuripoti taarifa kuhusiana na masuala ya rushwa, ubadhirifu wa mali za umma na udhalilishaji kwa kuyakemea kwa kuwa ndio yanayorejesha nyuma maendeleo ya nchi yao.

“Ingelipendeza na kutupa heshima kubwa ndani ya tasnia yetu iwapo sisi waandishi tungekuwa wa mwanzo kubaini mambo au kuwa sababu ya serikaili kutoa ufafanuzi ndani ya serikali kwa kuwa na utaalamu wa kudadisi kuchunguza na hatimae kuibuka na mambo yenye uhakika,” alisema Hassan.

Akimkaribisha Mkurugenzi huyo, Mwenyekiti wa ZPC, Abdallah Abdulrahman Mfaume, aliwasisitiza wanahabari wanapoandika habari zenye takwimu data kuhakikisha zinakua sahihi ili kuleta matokeo chanya na kupata usalama wa nchi badala ya kuwa ndio chanzo cha kuleta taharuki.

Aidha, aliwahimiza kuendelea kuweka mizania kwenye Habari zao kwa kuhusisha pande zote ili kuepusha matatizo yasiyokuwa na tija.

Naye Mratibu wa Internews, Ali Nassor Sultan, alisema miradi ya shirika hilo ililelenga kuwawezesha waandishi wa habari kuandika habari za kila aina na zenye tija hapa nchini.

Aidha aliwaomba washiriki wa mafunzo hayo, kuacha tabia ya kufanyakazi kwa mazoea badala yake wajitolee kwa moyo wa dhati ili kuleta mabadiliko kwa jamii inayowasikiliza na taifa kwa ujumla.

Mafunzo hayo yaliyoshirikisha waandishi wa Habari 30, mada za uandishi wa habari za uchunguzi, usahihi wa takwimu (data), habari za jinsia na namna ya kufungua mashauri ya kimkakati kulinda Uhuru wa Habari ziliwasilishwa na Wakufunzi wa vyombo vya habari, Imane Duwe, Ali Mwadini na Juma Khamis.

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango