NMB yakabidhi gawio la 30.7b/- serikalini

NA MWANDISHI WETU, DODOMA

MAKAMU wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Philip Mpango, ameyataka mashirika ambayo serikali ina hisa kuhakikisha yanatoa gawio la serikali pamoja na taasisi zinazotakiwa kutoa asilimia 15 ya mapato ghafi kwa mujibu wa sheria zifanye hivyo kwa wakati.

Makamu wa Rais ametoa wito huo wakati wa hafla ya kupokea gawio la shilingi bilioni 30.7 kutoka kwa benki ya NMB iliyofanyika katika ukumbi wa Hazina jijini Dodoma Juni 15 2022.

Alisema mashirika yanayotegemea ruzuku kutoka mfuko mkuu wa serikali yanapaswa kuwa na  mikakati madhubuti inayotekelezeka ili kupunguza utegemezi kwa serikali na kumuagiza  Msajili wa Hazina kuhakikisha  wakuu wa taasisi hizo wanatekeleza maagizo hayo.

Dk. Mpango alieleza kuwa, serikali itaendelea kuweka mazingira endelevu ya biashara kwa sekta ya fedha nchini na kuipongeza benki ya NMB kwa kuendelea kuchangia maendeleo ya jamii sambamba na kusaidia ukusanyaji wa mapato ya serikali kwa kuimarisha mifumo ya ukusanyaji.

Aidha aliwashauri watendaji wa benki hiyo kuendelea kushirikiana na serikali kwa kuongeza fursa za ajira kwa vijana na wanawake na kuimarisha  huduma za kijamii kwenye sekta mbali mbali kama afya, elimu na utunzaji wa mazingira na  kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabia nchi na tabia watu.

Nae Waziri wa Fedha na Mipango, Dk. Mwigulu Nchemba, amesema Wizara itaendelea kusimamia maelekezo na kuhakikisha taasisi za serikali ambazo serikali ina hisa zinatoa gawio.

“Serikali itaendelea kushirikiana na taasisi zote za sekta binafsi ili kuhakikisha zinafanya kazi vizuri na kuwasilisha gawio la serikali,” alieleza Dk. Nchemba.

Awali akitoa taarifa kwa Makamu wa Rais, Afisa Mtendaji Mkuu wa NMB, Ruth Zaipuna, alisema faida ya benki hiyo baada ya kodi katika kipindi cha 2021 iliongezeka kwa asilimia 41 na kufikia shilingi bilioni 290.

Alieleza kuwa, kiasi hicho ni kikubwa ikilinganishwa na shilingi bilioni 206 za mwaka 2020 ambapo idadi ya akaunti za wateja iliongezeka hadi kufikia shilingi milioni 5 ikilinganishwa na milioni 4 za mwaka 2020.

“Katika kuhakikisha benki inaendelea kuwa na maendeleo endelevu, tumeongeza mtaji wa benki hadi kufikia shilingi trilioni 1.3 na benki iliendelea kuwa na ufanisi na kuweka rekodi ya uwiano wa gharama za uendeshaji na mapato, kufikia asilimia 46,” alisema Zaipuna.

Zaipuna alisema kwa mwaka 2021, benki ilipata tunzo saba za kimataifa, ikiwemo ya benki bora nchini kwa miaka tisa mfululizo iliyotolewa na jarida la kimataifa la ‘Euromoney’.

“Aidha hadi mwishoni mwa mwaka 2021, mikopo yenye thamani ya shilingi trilioni 4.3 imetolewa kwa wakulima, wafanyabiashara wadogowadogo na wa kati na watu binafsi,” aliongeza Zaipuna.

Alisema mafanikio hayo yalitokana na kuimarika kwa uwekezaji katika mifumo ya kidijitali, huduma za wakala, zilizoongezeka na kufikia mawakala 10,194 ukilinganishwa na mawakala 8,410 waliokuwepo 2020.

Nae Mwenyekiti wa bodi ya wadhamini ya NMB, Dk. Edwin Mhede alisema ongezeko la faida kwa benki hiyo linatokana na uimara na umadhubuti wa uongozi na kwamba wanajivunia kuwa na Mtendaji Mkuu, Ruth Zaipuna.

Akitaja mafanikio ya kipindi cha miaka mitano, mhede alieleza kuwa yamekuwa yakipanda kila mwaka ambapo kwa mwaka 2020 benki ilitoa gawio la shilingi 20.8 bilioni, huku mwaka 2019 shilingi bilioni 15.6 zilitolewa.

“Tunatarajia kwa mwaka wa 2022 kuwa na gawio nono zaidi kwani katika kipindi cha miezi mitatu ya mwanzo, benki imepata faida kubwa inayolingana na faida ya mwaka mzima katika kipindi cha miaka ya nyuma,” alieleza Mhede.




Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango