Euro 10.1M kuimarisha usalama wa chakula Tanzania

Na Saida Issa,DODOMA

SERIKALI imezindua mradi wa miaka mitatu na miezi sita wa uboreshaji huduma za afya ya mimea Tanzania utakaogharibu kiasi cha EURO milioni 10.1 ikiwa ni hatua za kuimarisha usalama wa chakula nchini.

Hayo yalibainishwa Jijini Dodoma na Naibu waziri wa Kilimo Antony Mavunde,wakati  akizungumza katika uzinduzi huo.
Alisema Februari 16, 2021, serikali ya kupitia Wizara ya Fedha na Mipango iliingia mkataba wa kutekeleza mradi wa Kuimarisha Afya ya Mimea na Jumuiya ya Umoja wa Ulaya (EU).

Mradi huu wa miaka mitatu na miezi sita unafadhiliwa na Jumuiya ya Umoja wa Ulaya (EU) kupitia Mfuko wake wa Maendeleoa (EDF), Shirika la Umoja w a Mataifa la Kilimo na Chakula (FAO) na serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

“Aidha, FAO ni wasimamizi wa mradi na utekelezaji hufanywa na serikali ya Tanzania kupitia Mamlaka ya Afya ya Mimea na Viutilifu (TPHPA) iliyo chini ya Wizara ya Kilimo”alisema Mavunde.

Alisema kuwa mradi huo unatekelezwa kwa bajeti ya jumla EURO Milioni 10.1 ikiwa ni mashirikiano ya ufadhili wa Jumuiya ya Umoja wa Ulaya (EUR Milioni 9.5), Shirika la Umoja wa Mataifa la Kilimo na Chakula – FAO (EUR 350,000) na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (EUR 250,000).

Mavunde, alisema mradi huo unalenga kuhakikisha usalama wa chakula nchini kwa kuimarisha mfumo wa ukaguzi na utoaji wa vyeti vya usafi wa mazao yanayosafirishwa kwenda nje ya nchi.

Pia, mradi huo unalenga kudhibiti visumbufu vigeni kwa kuhakikisha mazao yanayoingia au kutoka nchini yana ubora unaokidhi viwango vya masoko ya kimataifa.

“Nachukua fursa hii kuwashukuru Umoja wa Jumuiya ya Ulaya (EU) na Shirika la Umoja wa Mataifa la Kilimo na Chakula (FAO) kwa kufadhili na kusimamia fedha za mradi huu muhimu. Ni imani yetu kuwa malengo yaliyopangwa yatafikiwa na hivyo kuongeza upatikanaji wa masoko ya kimataifa na kuchochea ukuaji wa uchumi wa Taifa na wa mtu mmoja mmoja,”alisisitiza Mavunde.

Vile vile, alisema mradi huo ulitokana na ukaguzi uliofanyika hapa nchini mwaka 2017, katika mifumo maalum ya udhibiti wa mimea na mazao yanayosafirishwa kwenda nchi za Umoja wa Jumuiya ya Ulaya.

“Ukaguzi huo ulibaini mapungufu yalikuwa sehemu ya Afya ya Mimea katika maeneo yafuatayo, maarifa madogo kwa wakaguzi wa afya ya mimea kuhusu matakwa ya usafi wa mazao na bidhaa za kilimo zinazoingizwa katika nchi za Umoja wa Ulaya,kukosekana kwa mfumo wa kufanya kukusanya takwimu za visumbufu vya mazao,kukosekana kwa maabara maalum zenye uwezo wa kufanya uchunguzi muhimu ili kuthibitisha cheti cha usafi wa mimea kinachotolewa kwa mimea na mazao yanayokidhi vigezo na masharti ili kufikia masoko ya kimataifa,"alisema.

“Kutokuwepo kwa utaratibu wa kutambua masuala ya usafi wa mimea na maarifa madogo kuhusu matakwa yaliyopo ya ubora wa mimea na mazao wakati wa usafirishaji kufikia soko husika”alieleza.

Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Afya ya mimea na Viwatilifu Tanzania (TPHPA), Dk. Efraim Njau, alisema sekta ya kilimo ni muhimu sana ambapo imeajiri zaidi ya asilimia 67 ya watanzania na kuchangia takribani asilimia 29 ya pato la taifa.

“Matokeo tarajiwa ya mradi huu ni kuziongezea uwezo maabara za mamlaka kujenga, kukarabati na kuweka vifaa katika maabara za Mamlaka, kuimarisha mfumo wa ufuatiliaji wa visumbufu na masalia ya viuatilifu katika mnyroro wa thamani ya uzalishaji wa mazao hususan ni yale mbogamboga na matunda,” alisema.

Mwakilishi wa FAO, Nyebenyi Tipo, alisema mradi huo umelenga kuhakikisha usalama wa chakula hasa kwa mazao yanayovuka mipaka kwa kuhakikisha yanakuwa na ubora.



Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango