Serikali yaahidi msukumo uzalishaji mazao ya nyuki

NA MWANDISHI WETU

WIZARA ya Biashara na Maendeleo ya Viwanda imeeleza kuwa itaendelea kutoa msukumo kwa wafugaji wa nyuki na wazalishaji wa mazao ya nyuki ili kuimarisha uchumi wao na na tija kwenye kilimo.

Hayo yameelezwa na Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Ali Khamis Juma, alipokua akizungumza katika maadhimisho ya Siku ya Nyuki Dulinani yaliyofanyika Kitogani, mkoa wa Kusini Unguja.

Alieleza kuwa kutokana na faida zinazopatikana kwenye ufugaji wa nyuki, ipo haja kwa Wizara ya Kilimo, Umwagiliaji, Maliasili na Mifugo kuweka mkazo wa kuiimarisha sekta hiyo ili isaidie ukuaji wa uchumi wa mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla.

“Kama mlivyoeleza hapa, nyuki ana faida nyingi kiuchumi na kijamii hivyo wakati wizara mnaendelea na mapitio ya sera ya misitu, mnaweza kutunga kanuni za misitu na nyuki ili kulinda makundi ya nyuki yaliyoanza kupotea”, alieleza Juma.

Aidha aliwataka wafugaji hao kufuata maelekezo ya wataalamu sambamba na kulinda uoto wa asili ili kuzalisha bidhaa zitakazotosheleza soko la ndani na nje ya nchi.

“Niwatie moyo na kuwahakikishia kwamba mtakapozalisha bidhaa zinazotokana na nyuki, wizara yetu itawapatia msaada wa kiufundi na kitaalamu ikiwemo kuwapatia alama ya ithibati ubora ili kulifikia soko la kimataifa”, alieleza Katibu Mkuu huyo.

Aidha aliipongeza wizara ya kilimo na wadau mbali mbali kwa juhudi inazochukua kuhakikisha sekta ya nyuki inawanufaisha wananchi kwa kuwajengea uwezo wafugaji nyuki wa Unguja na Pemba.

Akimkaribisha Katibu huyo, Katibu Mkuu wa Wizara ya kilimo, Umwagiliaji, Maliasili na Mifugo, Seif Shaaban Mwinyi, aliwahimiza vijana kujikita katika shughuli za ufugaji nyuki na uhifadhi misitu.

Alieleza kuwa kufanya hivyo kutapunguza tatizo la ajira, kulinda afya zao na kuwaahidi wanachama wa jumuiya za wafugaji nyuki kwamba wizara itaendeleza mikakati ya kuziimarisha ili ziendelee kuwanufaisha wengi.

Nae Mkurugenzi wa Idara ya Misitu, Said Juma Ali, alieleza kuwa sekta ya nyuki na uzalishaji wa asali na mazao mengine ya nyuki imeendelaa kuimarika kiasi cha kufikia wafugaji 1,531 waliosajiliwa na kutambulika rasmi.

Alisema idadi hiyo inaweza kuongezeka na kuongeza uzalishaji wa asali na kufikia malengo yaliyowekwa na ilani ya uchaguzi wa Chama cha Mapinduzi (CCM) ya Zanzibar kuzalisha tani 25 ifikapo mwaka 2025.

“Ili kufikia hatua hiyo wizara imeanza mapitio ya sera ya misitu, kuimarisha mkakati wa elimu ya ufugaji nyuki lakini pia kuandaa rasimu ya sera na kutangaza misitu ya hifadhi ya nyuki ili kuimarisha maisha yao”, alieleza Juma.

Akisoma risala kwa niaba ya wafugaji wenzake, Mtumwa Rashid Khamis, alileza kuwa maadhimisho hayo ni ya saba toka siku hiyo ilipotangazwa na umoja wa mataifa kwa lengo la kuimarisha ulinzi wa nyuki ili kusaidia ukuaji wa uchumi na maisha.

Alieleza kuwa licha ya faida zinazopatikana kupitia nyuki bado ufugaji wake unakabiliwa na changamoto kadhaa ikiwemo ya uharibifu wa misitu na matumizi ya dawa na viatilifu kwenye kilimo.

Alizitaja changamoto nyengijne kuwa ni mabadiliko ya tabia nchi, ughali wa vifaa vya kufugia na kuvunia asali na mazao mengine ya nyuki kama vile chavuo, sumu ya nyuki, nta, maziwa ya nyuki na gundi la nyuki ambazo zina thamani kubwa.

Siku ya nyuki duniani huadhimishwa kila ifikapo Mei 20 ya kila mwaka, ambapo Jumuiya ya Wafugaji Nyuki Zanzibar (ZABA), Jumuiya ya Ufugaji Nyuki Pemba (PEBA) ziliiadhimisha siku hiyo kwa kushirikiana na Wizara ya kilimo kupitia Idara ya Misitu kwa mafunzo ya ufugaji na kuzindua vifaa vya kuvunia mazao ya nyuki na utalii wa nyuki (bee tour).

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango