SMZ, SMT kushirikiana uhifadhi wa misitu
NA SALAMA MOHAMED, WKUMM
KATIBU Mkuu Wizara ya Kilimo, Umwagiliaji, Maliasili na Mifugo, Seif Shaaban Mwinyi, amesema serikali zote mbili za Tanzania na taasisi zake zitaendelea kuimarisha mashirikiano ili ziweze kuleta maendeleo nchini.
Akizungumza katika hifadhi ya Msitu Pugu kanda ya Mashariki wilaya ya Ilala, Dar es salam wakati wa ziara ya kutembelea msitu wa Jane Goodall iliyojumuisha viongozi na watendaji wa Wizara hiyo.
Mhifadhi wa msitu wa Jane Goodall uliopo Pugu jijini Dar es salam, Rashid Mustafa (kushoto) akitoa maelezo kwa viongozi wa Wizara ya Kilimo, Umwagiliaji, Maliasili na Mifugo Zanzibar walipotembelea msitu huo wakati wa ziara ya kujifunza inayoongozwa na Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Seif Shaaban Mwinyi (wa tatu kulia).
Amesema dhamira ya ziara hiyo ni kuongeza mashirikiano na kujifunza mazingira yaliopo katika msitu huo ambapo taasisi hiyo imeweza kupiga hatua ya maendeleo katika kuwainua vijana kujifunza mbinu mbali mbali za hifadhi ya misitu.
Seif ameeleza kuwa uwepo wa msitu huo umeongeza tija kwa kupata mashirikiano mazuri na wanajamii waliozunguka maeneo hayo kwa kufanya miradi yenye kuwapatia tija kutokana na hifadhi hiyo.
Nae Msimamizi wa Jane msitu Goodall, Rashid Mustafa, amesema msitu huo una vivutio vingi ikiwemo aina 36 za wanyama, ndege 235 na aina 414 za miti na mimea.
Mbali na uwepo wa ndege na wanyama hao pia eneo hilo linatumika kwa tafiti mbali mbali zinazoshirikisha vyuo vikuu vya Tanzania wakiwemo wa Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine na chuo kikuu cha Dar es salaam na vyuo vikuu vya nje ya nchi.
Kwa mujibu wa Rashid hifadhi hiyo yenye ukubwa wa hekta 6 imeanzishwa na Jane Goodall mnamo mwaka 2017 na kupewa jina la 'Nature Center' kwa ajili ya mafunzo kwa klabu na jumuiya za uhifadhi za ndani na nje ya nchi kwa ajili ya uhifadhi endelevu.
Ziara ya Katibu huyo na viongozi wa wizara ya Kilimo, Umwagiliaji, Maliasili na Mifugo Zanzibar akiwemo Mkurugenzi wa Idara ya Misitu ni matokeo ya ushirikiano wa muda mrefu kati ya hifadhi ya Jane Goodall na Wizara hiyo katika kusimamia na kuendeleza hifadhi ya misitu ya Jambiani na Muyuni ambapo matarajio ya ujumbe huo ni kujifunza zaidi katika ambapo ziara hiyo itaendelea mkoani Kigoma kwa kutembelea misitu ya hifadhi ya Gombe.
Comments
Post a Comment