ZBS yanasa nyaya ‘feki’ za umeme


NA MWANDISHI WETU

TAASISI ya Viwango Zanzibar (ZBS) imezuia matumizi na usambazaji wa nyaya za umeme (PVC Cable) zenye jina la Kili Cable na namba ya utambulisho TP/EEL/18/2023 baada ya kugundulika kuwa zipo chini ya viwango.

Akitoa taarifa kwa vyombo vya habari katika ofisi za taasisi hiyo Maruhubi, Mkurugenzi Mkuu wa ZBS, Yussuph Majid Nassor, ameeleza kuwa mbali ya kuwa chini ya kiwango, pia mtengenezaji amefoji jina la kibiashara la bidhaa hiyo.

Majid ameeleza kuwa hatua hiyo imekuja baada ya kupata taarifa za kuwepo kwa bidhaa hiyo sokoni zilizoingizwa nchini na mfanyabiashara asiyefahamika jambo ambalo ni kinyume na sheria.

Amesema kuwa baada ya kupata taarifa kutoka kwa wasamaria wema, ZBS ilichukua sampuli za bidhaa hiyo na kuifanyia uchunguzi wa kimaabara na kugundulika kutokidhi viwango vilivyowekwa.

 “Tulipochukua sampuli za waya hizo na kuzipima kwenye mabara zetu, ripoti ya upimaji wa sampuli hizo imenakiliwa kuwa bidhaa hii imefeli  katika kipengele cha ‘sheath’ (unene wa waya wa nje)”, ameeleza Majid.

Amefafanua kuwa waya huo ulitakiwa kuwa na unene wa 1.5mm2 kulingana na matakwa ya kiwango cha ZBS lakini uligundulika  kuwa na 1.05mm2  jambo linaloweza kuleta madhara kwa watumiaji.

Hivyo aliwaomba wananchi kuendelea kushirikiana na taasisi hiyo kwa kutoa taarifa wanapozigundua bidhaa zenye utambulisho huo huku akilishukuru jeshi la polisi na Tume ya Ushindani Halali wa Biashara Zanzibar kwa kushiriki operesheni ya kuondoa bidhaa hizo madukani.

Majid ameeleza kuwa mbali ya hatua zilizochukuliwa, wamelifikisha swala hilo polisi na Mamlaka ya Kuzuia Rushwa na Uhujumu uchumi kwa hatua zaidi kufuatia kunakiliwa kwa bidhaa hiyo jambo ambalo ni kosa kisheria.

“Kwa mujibu wa sheria ya viwango namba 1 ya 2011 pamoja na mambo mengine, ZBS imepewa jukumu la kulinda ubora wa bidhaa zinazoingizwa au kuzalishwa nchini lakini pia kulinda viwanda na wazalishaji halali ndio maana swala hili tumelifikisha huko ili kulinda haki za kampuni ya AfriCab”, ameeleza Mkurugenzi huyo.

Aidha amesema ZBS inaendelea na uchunguzi juu ya bidhaa hizo na taarifa za kuwepo kwa mchele uliioamriwa kurudishwa ulipotoka baada ya kukosa viwango katika masoko ya Zanzibar na kwamba hatua zitachukuliwa kwa wahusika.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi huyo, bidhaa hizo zimegunduliwa kuwepo sokoni mapema mwezi huu kabla ya Mei 11, mwaka huu taasisi hiyo kufanya operesheni ya kuziondoa na kisha kubaini kuwa hazikukaguliwa kabla wala baada hazijaingia nchini kupitia mifumo ya ukaguzi ya taasisi hiyo.

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango