Dkt. Mwinyi ahimiza ubunifu huduma za bima ZIC

NA MWANDISHI WETU

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Hussein Mwinyi (wa pili toka kulia) amezindua huduma ya bima inayofuata misingi ya dini ya Kiislamu (Takaful) inayotolewa na Shirika la Bima Zanzibar (ZIC) na kulipongeza shirika hilo kwa ubunifu wa huduma hiyo hiyo itakayowavutia wananchi waliokua wakiepuka huduma za bima kwa mitazamo ya imani ya kidini.

Uzinduzi huo ulifanyika jijini Zanzibar Julai 5, mwaka huu ambapo huduma hiyo itakuwa inatolewa na ZIC kupitia kampuni yake tanzu inayofahamika kama ZIC Takaful ambapo dkt. Mwinyi alisisitiza azma ya serikali ya mapinduzi Zanzibar kuhakikisha huduma za bima zinawafikia wananchi wote bila ya vikwazo vya kiimani bali matakwa yao.

Dkt. Mwinyi akizungumza na watendaji wa ZIC na wadau mbali mbali wa huduma hiyo wakiwemo viongozi wa serikali, dini, wadau wa bima, taasisi za fedha na wananchi, amesema huduma hiyo imekua ikitolewa maeneo mbali mbali ulimwenguni hivyo itaongeza sifa za uwekezaji nchini.

“Kwa muda mrefu sasa huduma ya Takaful imekuwa ikitumiwa katika nchi mbali mbali za barani Afrika, Ulaya na Asia ili kutoa fursa kwa biashara ambazo zinafuata misingi ya Kiislamu. Ujio wa huduma hii hapa nchini utatusaidia pia kuwavutia wawekezaji wanaoamini katika imani hii hatua ambayo ni muhimu kwa maendeleo ya shirika na taifa kwa ujumla’’ amesema.

Alibainisha kuwa huduma hiyo inatarajiwa kuwa kiungo muhimu katika ukuaji wa huduma za fedha zinazofuata misingi ya kiislamu kwani hutoa fursa kwa mabenki ambayo tayari yanaendeshwa kwa misingi hiyo, kuweza kutoa huduma za bima jambo ambalo halikuwezekana kabla ya uanzishwaji wa Takaful.

Aidha Dkt. Mwinyi alibainisha kuwa lengo la serikali ni kuona kamba wananchi wote bila kuathiri imani zao za kidini wanafikiwa na huduma mbalimbali zi kiuchumi zinazotolewa na taasisi mbalimbali huku akipongeza baadhi ya mashirika na taasisi likiwemo Shirika la Bima Zanzibar kwa namna linavyotafsiri vema nia hiyo ya serikali.

Awali akizungumza kwenye uzinduzi huo Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Zanzibar, Ali Suleiman Ameir, amesema ujanzishwaji wa huduma ya Takaful unakwenda sambamba na jitihada za serikali za kuimarisha sekta ya bima na kuchochea ukuaji wa uchumi wa nchi hatua ambayo ina manufaa makubwa kwa serikali, wananchi na taifa kwa ujumla.

“Kwa upande wa serikali, huduma ya Takaful itasaidia kuongeza mapato ya serikali kupitia kodi na tozo zinazopatikana kutokana na shughuli za bima. Hii itachangia kuimarisha uwezo wa serikali wa kutoa huduma muhimu kwa wananchi na kutekeleza miradi ya maendeleo. Tunawapongeza sana ZIC kwa hatua hii muhimu”, alisema.

Alisema serikali imejipanga kuhakikisha huduma ya Takaful inaendeshwa kwa ufanisi mkubwa na tayari imeanzisha mifumo madhubuti ya udhibiti na ukaguzi ili kuhakikisha uwazi, uwajibikaji, na uaminifu katika shughuli za bima ikiwemo huduma hiyo.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mwendeshaji wa ZIC, Arafat Haji alisema hatua hiyo muendelezo wa mkakati wa msingi wa shirika hilo unaolenga kuhakikisha huduma zake zinawafikia watu wote lengo likiwa ni kuimarisha upatikanaji wa huduma za bima kwa wananchi na hivyo kuongeza kasi ya ukuaji wake na ule wa taifa kwa ujumla.

“Tunaamini kwamba huduma hii Takaful inakwenda kutujengea taswira bora zaidi mbele ya wadau wetu wote imani ambayo tunaamini itatujenga zaidi kibiashara na hivyo kutuhakikishia uwezo wetu katika kulinda miradi, biashara na mali za wawekezaji wetu huku pia tukiongeza ajira kwa wananchi”, amesema Arafat.

Mkurugenzi Arafat ameongeza kuwa, huduma ya Takaful itaongeza kasi, nguvu ya ukuaji na kuunga mkono jitihada mbali mbali zinazoendelea kufanywa na taasisi za kifedha nchini ambazo zinabuni huduma zinazoendana na misingi ya imani ya Kiislamu.

Naye  Kamishna wa Bima Dkt. Baghayo Saqware alisema kwa sasa soko la bima nchini linahudumia asilimia 15 hadi 20 tu ya wananchi wote hivyo ubunifu unaolenga kuongeza watumiaji wa huduma hiyo ni muhimu kwa kuwa ni adhma ya serikali kuwa na mfumo jumuishi wa utoaji wa huduma hiyo muhimu kiuchumi.

“Sekta ya Bima ni muhimu kwa ukuaji wa uchumi wa mtu mmoja mmoja, taasisi na serikali kwa ujumla na hiyo ndio sababu tunalishukuru Shirika la Bima Zanzibar kwa hatua hii, inayolifanya shirika hili kuwa la kwanza nchini kutoa huduma ya bima ya Takaful”, alieleza Kamishna huyo.

Huduma ya Takaful inazingatia misingi na maadili ya dini ya Kiislamu ikiwemo kutohusisha  riba, kamari, huku ikipinga uwekezaji katika biashara zinazokwenda kinyume na misingi ya dini hiyo.

Comments

Popular posts from this blog

Balozi Mpanda ahimiza ubunifu uhifadhi wa mazingira

Vodacom yawapa uhakika wa matibabu mama, watoto wachanga