Wahariri chachu ya maendeleo, ukuaji wa Kiswahili - Hemed

NA MWANDISHI WETU

MAKAMU wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Hemed Suleiman Abdulla, ameeleza kuwa juhudi za wahariri wa vyombo mbali mbali vya habari zimechangia ukuaji na maendeleo ya lugha ya Kiswahili ulimwenguni.

Hemed ameyasema hayo katika mkutano wa wahariri wa vyombo vya habari wa Tanzania kuadhimisha Siku ya Kiswahili Duniani uliofanyika ukumbi wa Sheikh Idriss Abdulwakil Kikwajuni jijini Zanzibar.

Amesema Wahariri Wakuu wana jukumu la kupitisha na kuweka sawa maandishi yote ndani ya vitabu, magazeti, majarida na vipindi vya redio au televisheni hatua iliyosaidia kwa kiasi kikubwa kukuza lugha hiyo ndani na nje ya Tanzania.

Aidha  amewataka kuendelea kuzingatia maadili ya kazi zao na kuibua mambo yasiyoendana na mila, tamaduni na silka za nchi bila ya kumuonea mtu au taasisi muhali.

Hemed pia alitumia jukwaa hilo kueleza fursa zinazopatikana katika lugha ya Kiswahili na kuwataka wenye ujuzi wa lugha hiyo kuzichangamkia ikiwemo ukalimani, utafsiri, uhariri, uandishi na utangazaji wa habari pamoja na ufundishaji wa lugha hiyo kwa wageni.


Aidha ameeleza  kufurahishwa kwake na juhudi zinazochukuliwa na Baraza la Kiswahili la Tanzania (BAKITA) na Baraza la Kiswahili Zanzibar (BAKIZA) ya kuieneza lugha hiyo katika mataifa mbali mbali ulimwenguni.

“Juhudi hizo zinaenda sambamba na mikakati ya kukifikisha Kiswahili katika nchi mbali mbali ikiwemo ya Ujerumani, Uholanzi, Italia, Nigeria, nchi za Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE), Malawi, Rwanda na Zimbabwe hatua ambaZo ni dhahiri zinaongeza umahiri wa watumiaji wa lugha hii katika mataifa yao”, amesema Hemed.

Kwa kuzingatia ukubwa na kuendelea kutapakaa kwa lugha hiyo, Hemed amelitaia Jukwaa la Wahariri Tanzania na wahariri wa vyombo mbali mbali vya habari, kuendelea kushirikiana na mabaraza ya Kiswahili nchini kuhakikisha vyombo vya habari vinatumia  kiswahili fasaha na Sanifu.

Pia ameeleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inayoongozwa na Rais Dk. Hussein Ali Mwinyi imeamua kuifanyia marekebisho Sheria ya Habari ili iendane na mabadiliko yanayotokezea katika sekta ya mawasiliano na teknolojia ya habari nchini.



Kwa upande wake Waziri wa Habari,  Vijana, Utamaduni na Michezo, Tabia Maulid Mwita, ameeleza kuwa serikali zote mbili za Tanzania zina mkakati wa kukifanya Kiswahili kuwa ni bidhaa itakayowanufaisha wataalamu wa lugha hiyo na taifa kwa ujumla.

Alitaja baadhi ya manufaa hayo kuwa ni pamoja na  kupeleka walimu wa kusomesha Kiswahili nje ya Tanzania pamoja na kuwakaribisha wageni kusoma Lugha hiyo katika vyuo na taasisi za elimu zilizopo nchini.

Aidha Tabia amewataka Wahariri Wakuu kukemea tabia ya wachache wanaotumia misamiati kinyume na maana zilizokusudiwa ili kudhibiti ufasaha wa lugha.

Nae Naibu Waziri wa Sanaa, Utamaduni na Michezo wa serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Khamis Mwinjuma, ameeleza kuwa Serikali zote mbili za Tanzania zinachukua jitihada katika kuhakikisha lugha ya Kiswahili inakuwa ni nembo ya taifa la Tanzania.

Amesema ni wajibu wa wananchi kuhakikisha wanaitangaza Lugha ya Kiswahili ikiwemo kuibua Utalii wa Lugha ya Kiswahili ili kuhakikisha wageni wanaotembelea Tanzania wanatumia fursa zitokanazo na Lugha hiyo.

Akitoa maelezo kuhusu jukwaa hilo Katibu Mtendaji wa Baraza la Kiswahili la Tanzania (BAKIZA), Consolata Mushi ameeleza kuwa Jukwaa hilo litakuwa ni chachu ya kupunguza changamoto za Kiswahili zinazojitokeza katika vyombo vya habari na kuchochea usanifu wa lugha.

Katika mkutano huo, pia wahariri na wadau wa lugha ya Kiswahili walipata nafasi ya kuelezea njia na mbinu mbali mbali za kupunguza makosa yanayofanywa na waandiushi na watangazaji wa vyombo vya habari.

Mkurugenzi wa Idara ya Mawasiliano Ikulu Zanzibar ambaye pia ni Msemaji Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Charles Martin Hilary, alieleza haja ya watangazaji wa redio na televisheni kuzingatia usanifu na ufasaha wa lugha wanapokuwa kwenye vipindi kuepusha ubanangaji wa lugha ya Kiswahili.

Aliongeza kuwa wapo watangazaji wanaochanganya lugha ya Kiswahili na kiingereza jambo linaloondoa ladha na kupotosha maana na uhalisia wa maneno ya Kiswahili.   

Comments

Popular posts from this blog

Balozi Mpanda ahimiza ubunifu uhifadhi wa mazingira

Vodacom yawapa uhakika wa matibabu mama, watoto wachanga