ABSA kuendelea kuchangia kampeni uzazi salama Z'bar

 

NA MWANDISHI WETU

BENKI ya ABSA Tanzania imeeleza kuwa itaendelea kushirikian na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) kustawisha afya za wananchi wa Zanzibar kupitia kampeni na programu mbali mbali.


Akizungumza baada ya matembezi ya hiyari na mbio fupi za marathoni (Wogging) zilizoandaliwa na shirika la AMREF Tanzania kwa lengo la kusaidia jamii kupitia sekta ya afya, Mkurugenzi Mtendaji wa benki hiyo, Obedi Laiser, alisema wameamua kudhamini tukio hilo kwa kutambua juhudi zinazochukuliwa na serikali kuiimarisha sekta hiyo.

“Sisi kama benki tunatambua mchango mkubwa mashirika binafsi kama AMREF mnafanya katika kuleta mabadiliko katika jamii na ndio dhumuni kuu kwetu kutamani kushiriki na kuunga jitihada hizi za kuleta mabadiliko katika afya ya uzazi wa mama na mtoto”, alieleza Mkurugenzi huyo.

Aliongeza kuwa dhumuni ya benki hiyo kushiriki kwenye tukio hilo ni kuchangia na utatuzi wa changamoto na vikwazo ambavyo wanawake wajawazito mara nyingi hukumbana nazo wakati wa kujifungua.

Aidha Mkurugenzi huyo alieleza kuwa jitihada ya pamoja kuongeza uelewa na kuelewa kuhusu changamoto na tabu wanazopitia wanawake wajawazito zinahitajika ili pia kutatua dharura zinazowapata watoto pindi wanapozaliwa.

“Lengo la ABSA ni kuiwezesha Afrika ya kesho, pamoja, mtu mmoja baada ya mwengine. Katika kutafuta jamii yenye afya bora na mustakabali mzuri, lazima tukubali umuhimu mkubwa wa afya ya mama na mtoto”, alieleza.

Alifafanua kuwa tukio hili ni jukwaa la wadau wa sekta ya afya kuangazia changamoto zinazowakabili mama wajawazito ili kuhamasisha mabadiliko chanya kwa kuchochea uelewa na huruma kubwa ndani ya jamii yetu.

“Wanawake wajawazito ni msingi wa kizazi chetu cha baadaye. Ustawi wao unaathiri moja kwa moja afya na uwezo wa kizazi kijacho cha watu ambao wataunda nchi yetu na ulimwengu kwa ujumla”, alieleza.

Alifafanua kuwa benki hiyo imedhamini tukio hlo kwa kutoa Shilingi  milioni 100 ambazo zitasaidia upatikanaji wa vifaa tiba vitakavyofanikisha uzazi salama kwa mama na mtoto.

Aidha alipongeza juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, kwa jitihada inazochukua kuleta maendeleo kwa watu wa Zanzibar na Tanzania kwa ujumla.

Akihutubia katika tukio hilo, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi, aliipongeza benki hiyo kwa kudhamini na kufanikisha matembezi na mbio hizo zenye lengo la kuimarisha huduma za afya ya uzazi salama wa mama na mtoto.

“Kwa niaba ya serikali natoa shukurani kwa benki ya ABSA Tanzania na kuwataka waendelee kutupa ushirikiano katika kuhakikisha tunafanikiwa katika malengo yetu ya kupunguza idadi ya vifo vya mama wajawazito na watoto vinavyotokana na uzazi”, alieleza Dk, Mwinyi.

Aidha Dk. Mwinyi alieleza kufurahishwa na kampeni ya miaka mitatu na iliyoanza tokea mwaka jana ikiwa na lengo la kukusanya shilingi bilioni moja ambapo hadi sasa ahadi za jumla ya shilingi milioni 792 zimetolewa huku shilingi milioni 557.

Alisema, kampeni ya Uzazi Salama inaunga mkono juhudi za serikali kupunguza na kuepusha vifo vya mama wajawazito na watoto wachanga kutokana na ukweli kuwa bado takwimu za vifo hivyo bado vipo juu.

“Takwimu zinaonesha vifo vya kina mama 134 kati ya vizazi hai 100 kwa mwaka na vifo 28 vya watoto wachanga kati ya vizazi hai 1,000 kwa mujibu wa takwimu za utafiti wa afya ya uzazi na mtoto na viashiria vya malaria Tanzania (TDHS) za mwaka 2017”, alisema Dk.  Mwinyi.

Aliongeza kuwa kiwango hicho kinasababishwa na changamoto mbali mbali zikiwemo za upungufu wa vifaa tiba, uhaba wa wahudumu pamoja na kukosekana kwa dawa.

Matembezi ya hiyari na mbio fupi za AMREF Wogging Marathon 2023 zimefanyika kwa mara ya pili Zanzibar zimeandaliwa na shirika hilo kwa ushirikiano na serikali huku benki ya ABSA ikiwa mdhamini mkuuu sambamba na taasisi mbalimbali, wananchi pamoja na wadau wengine  waliochangia fedha, vifaa na utaalamu kuzifanikisha.

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango