Dimwa azionesha fursa za kilimo jumuiya CCM

NA mWANDISHI WETU

NAIBU Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar, Dk. Mohammed Said Mohammed ‘Dimwa’, amezishajihisha jumuiya za CCM kuyatumia mashamba ya chama hicho kulima kilimo cha kisasa ili kujipatia ajira.

Dk. Dimwa alieleza hayo mara baada ya kutembelea mabanda ya maonyesho ya wakulima nane nane huko katika viwanja vya Dole Kizimbani, wilaya ya Magharibi ‘A’ Unguja.

Alisema CCM ina mashamba makubwa na moja katika malengo yake ni kuwekekeza katika kilimo hivvo ni fursa sasa kwa vijana na jumuiya zote za chama ambao wanataka kujiunga na kilimo kuyatumia sasa mashamba hayo.

“CCM ina mashamba mengi yakiwemo ya Kilombero, Kiwengwa na Bumbwini lakini la kilimo hasa ni hili la Kilombero na tuna heka nyingi waende kwenye maonesho kupata elimu ili waweze kuyatumia na wajiajiri kama inavyoelekezwa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi ili kuepuka kukaa bila ya kazi maalum,” alisema.

Aidha alisema, chama kimeshazungumza na benki ya kilimo kwa ajili ya kuwafadhili na imekubali kupitia mashamba yao na CCM kwa ujumla inaweza kukopesheka.

"Sasa tunawashajihisha sio tu vijana lakini jumuiya zote kama wazazi na kina mama kwa nafasi yao kwenye mashamba yale kila mtu atakaye taka kulima basi anaruhusiwa na tutaanza hapo katika ajira zetu za chama," alisema.

Akizungumzia maonesho ya wakulima, alisema yanatoa fursa kwa wananchi kupata uelewa juu ya kilimo cha kisasa.

Alisema maonesho hayo yanatoa nafasi kwa Wazanzibari kupata uelewa juu ya kilimo na kutoka katika kilimo cha mkono na kwenda katika kilimo cha kisasa ili kiweze kuwaletea tija.

Hata hivyo, alisema kupitia kilimo cha kisasa basi wakulima watapata mazao mengi na yaliyobora kwa kutumia sehemu ndogo ya shamba au bustani.

"Zanzibar ardhi haikui lakini watu wanaongezeka hivyo kwa kupitia kilimo cha kisasa tutapata kulima mazao yetu katika eneo dogo na kupata mazao yaliyomengi," alisema.

Alibainisha kuwa hivi sasa mambo mengi yanarahisishwa kwani unaweza kupima udongo ili kujua kama udongo huo unafaa kwa kutoa mazao bora.

Sambamba na hayo, alisema maonesho hayo yanaleta hamasa katika sekta na mifugo kwa kuwavutia wananchi wengi kuingia katika sekta hizo kwani kupitia maoenysho hayo wananchi wanapata kuona juu ya kilimo cha kisasa ambacho hakitumii nguvu nyingi.

Hivyo, aliiomba Wizara ya Kilimo, Umwagiliaji, Maliasili na Mifugo kuendelea kuratibu vizuri jambo hilo na kuwashajihisha wananchi kutembelea kwa wingi maonyesho hayo ili waweze kupata elimu ambayo itawasaidia kuingia katika kilimo chenye tija.

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango