Enezeni elimu kupunguza uharibifu wa misitu – Shamata

NA SALAMA MOHAMMED, WKUMM

WAZIRI wa Kilimo Umwagiliaji Maliasili na Mifugo, Shamata Shaame Khamis, ameitaka Idara ya Misitu kuandaa mafunzo maalum kwa wanajamii, Taasisi za Serikali na Zisizo za kiserikali (NGO's) ili kupunguza uharibifu wa misitu.

Ameeleza hayo shehia ya Bwejuu katika eneo la hifadhi ya Msitu wa Jamii Tongole, wilaya ya Kusini Unguja wakati alipokua akizindua zoezi la Upandaji wa miti asili kwenye msitu huo.

Shamata amesema kuna baadhi ya watu wana mwamko mdogo wa kutunza misitu asili na hivyo kusababisha matatizo yakiwemo ya mabadiliko ya tabia nchi hivyo wakipatiwa elimu itawasaidia kuondokana na uharibifu huo.

 Aidha amefahamisha kuwa lengo la hatua hiyo ni kudhibiti uharibifu wa msitu na uvamizi unaofanywa na watu kwa kufyeka miti kuandaa mashamba ya shughuli za kilimo, ujenzi na ujenzi wa makaazi usiozingatia taratibu na sheria za nchi.

 "Nataka kuwakumbusha kwamba msitu huu umehifadhiwa na jamii chini ya sheria ya misitu namba 10 ya mwaka 1996, kifungu cha 34 hadi 47 kupitia mradi wa Jozani Chwaka Bay chini ya Ufadhili wa Sirika la CARE la Austria hivyo ninaiomba jamii izingatie na kuziheshimu sheria zilizopo", alisema Shamata.

Sambamba na hayo alifahamisha kuwa Serikali ya awamu ya nane inayoongozwa na Dk. Hussein Ali Mwinyi ina lengo la kuwasaidia wananchi wake kwa kuwaletea maendeleo hivyo ni wajibu wao kulinda rasilimali zinazopatikana nchini kwa faida ya sasa na baadae.

Hata hivyo alisema licha ya Jumuiya ya Uhifadhi wa Mazingira (JECA) na Idara ya Misitu kuchukua hatua mbali mbali badokuna uharibifu unatokea na kuwaomba watu waliovamia eneo hilo kuondoka na kujisalimisha kabla idara haijachukua hatua.

Nae Mkurugenzi Idara ya Misitu, Said Juma Ali, alifahamisha kuwa upandaji wa miti hiyo unakusudia kurudisha haiba ya eneo hilo ili wananchi waliopo katika eneo hilo kupata kipato na kuwashajihisha kuzingatia sheria kwani atakaekamatwa anafyeka msitu hatua kali za sheria zitachukuliwa.

Kwa Upande wake Naibu Katibu wa Jumuiya Hifadhi ya Mazingira (JECA), Awesu Shaaban Ramadhan, alifafanua kuwa utalii wa misitu ya asili  una faida kwa vile rasilimali nyingi zilizomo kama vile ndege na wanyama wengine wanapatikana katika misitu hiyo.

Aliongeza kuwa pindipo wananchi wakiwekeza katika ulinzi na uhifadhi wa misitu hiyo, wataweza kujiingizia wao na serikali mapato hivyo kuondokana na umaskini.

Katika zoezi hilo, miti  1,300 ya mikunguuni ilipandwa kwa  mashirikiano ya  Idara ya Misitu, JECA na jamii katika eneo hilo, ambapo awali  miti 2,300  ilikusudiwa kupandwa lakini kutokana na baadhi yao kutokukidhi vigezo ya kuwepo katika maeneo ya hifadhi, haikupandwa.

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango