Nsokolo ahimiza ulinzi wa waandishi, vyombo vya habari

NA KHAMISHUU ABDALLAH

RAIS wa Muungano wa Klabu za Waandishi wa Habari Tanzania (UTPC), DeogratIus Nsokolo, amewasisitiza waandishi wa habari kuuelimisha umma juu ya umuhimu wa uhuru wa vyombo vya habari na nafasi ya waandishi katika jamii.

Nsokolo alitoa rai hiyo wakati akifungua mdahalo kuadhimisha siku ya kimataifa ya Kukomesha Uhalifu dhidi ya Waandishi wa Habari uliofanyika wa njia ya mtandao jana, ulioshirikisha waandishi wa habari, viongozi wa klabu za wanahabari, UTPC na wadau wengine.

Alisema hatua hiyo itasaidia kuongeza ufahamu kwa jamii jinsi vyombo vya habari vinavyochangia kujenga jamii yenye habari na taarifa sahihi na uelewa utakaoujenga mazingira bora kwa wanahabari kufanya kazi zao bila ya vitisho na vikwazo.

Aidha alisema pia hatua hiyo inaweza kuzuia misimamo ya upande mmoja na kupotosha habari kwa kuuelimisha umma jinsi waandishi wanavyochunguza na kuripoti masuala yanayowahusu na vitendo visivyo na maadili.

Aliongeza kuwa ili kujenga taifa lenye umoja, mshikamano na amani, vyombo vya Habari vinapaswa kuripoti mambo kwa usawa hivyo vinapaswa kuachwa kufanya kazi zake kwa kuzingatia weledi.

alisema umma ulioelimishwa unaweza kushiriki zaidi katika mchakato wa kisiasa na kijamii hivyo kuwa na mchango mkubwa katika ujenzi wa taifa.

Akizungumzia maadhimisho ya siku hiyo yanayofanyika kila Novemba 2 ya kila mwaka, alisema yamelenga kuongeza uelewa kuhusu changamoto zinazowakabili wanahabari katika utekelezaji wa majukumu yao na hatua za kuchuku kuondoa vitisho na madhila juu yao.

Alisema waandishi wa habari wamekuwa wakishambuliwa, vyombo vya habari kuwekewa vikwazo, matumizi na taratibu za kimahakama dhidi ya waandishi wa habari kutokana na kazi zao za uandishi wa habari zenye maslahi kwa umma.

Aidha aliupongeza Ubalozi wa Uswizi nchini Tanzania, Jeshi la Polisi Tanzania, Baraza la Habari Tanzania (MCT) na wadau wengine kwa kushirikiana na UTPC kuhakikisha usalama wa waandishi wa habari nchini kuwawezesha kuendelea kutimiza majukumu yao kwa mujibu na sheria za nchi.

Wakichangia katika mdahalo huo, waandishi wa habari na viongozi wa Klabu walisisitiza haja ya kuimarishwa mshikamano miongoni mwa wanahabari na taasisi wanazofanyia kazi ili kupunguza uwezekano wa kujiweka kwenye hatari.

Walieleza kuwa pamoja na baadhi ya maeneo kutokabiliwa na vitisho au madhila mara kwa mara, bado waandishi wengi wanafanya kazi katika mazingira hatarishi yanayochangia kutozingatia misingi ya taaluma yao.

Walisema kuwa hali hiyo inatokana na waandishi wengi kufanya kazi bila ya mikataba ya ajira au malipo ya uhakikia na kushauri kutanuliwa kwa wigo wa mijadala juu ya usalama wa waandishi kwa kuwajumuisha wadau zaidi ya vyombo vya ulinzi na usalama, waajiri na wamiliki wa vyombo vya habari.

Hata hivyo walishauri kuimarishwa kwa sheria za habari Tanzania bara na Zanzibar ili zitoe ulinzi kwa waandishi na vyombo vya habari ambao pia wamehimizana pia kujitambua na kusimamia maadili ya taaluma yao.

Akifunga mdahalo huo, Mkurugenzi Mtendaji wa UTPC, Kenneth Simbaya, aliwahimiza wanahabari kuendelea kupaza sauti juu ya madhila wanayopitia ili kupata njia ya kuyapunguza.

Alieleza kuwa UTPC kwa kushirikiana na wadau wengine wanaendelea kutafuta njia zitakazosaidia kujenga uwezo wa mwaandishi na wadaiu wengine ili kupunguza matukio ya uvunjifu wa uhuru wa kujieleza ambao ni sehemu ya haki za binadamu.

Kwa mujibu wa Shirika la Elimu, Sayansi na Utamaduni la Umoja wa Mataifa (UNESCO), waandishi wa habari 117 waliuawa mwaka 2021/2022 ambapo asilimai 38 walitoka katika mabara ya Latini Amerika na Asia huku asilimia 14 ya kesi za uhalifu dhidi ya waandishi wa habari zikiendelea kushughulikiwa.

Comments

Popular posts from this blog

ZALIRI, FLI zaingia makubaliano kuimariusha sekta mifugo

Ibueni changamoto zinazokamisha usawa wa kijinsia - Simbaya

Uislam unakubali uzazi wa mpango